1. Historia ya Mradi
Mheshimiwa Spika, Katika
miaka ya tisini (1990s), Tanzania ilikuwa ikikabiliwa na tatizo la uhaba
wa maji katika mabwawa ya kuzalisha umeme, hali iliyopelekea kuwepo kwa
upungufu wa umeme na kuathiri shughuli za maendeleo ya kiuchumi na
kijamii nchini. Ili kukabiliana na tatizo hilo, Serikali ilichukua hatua
za dharura za kuanzisha mradi wa kufua umeme wenye uwezo wa kuzalisha
Megawati (MW) 100.
Mheshimiwa Spika, Mwaka 1994 Serikali ilitoa kazi ya uwekezaji kwa Kampuni ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL) iliyokuwa inamilikiwa na Kampuni za VIP Engineering and Marketing Ltd ya Tanzania iliyokuwa na Asilimia 30 na MECHMAR Corporation ya Malaysia (MECHMAR) iliyokuwa na Asilimia 70. Kampuni ya IPTL ilipewa leseni ya kujenga, kumiliki na kuendesha (Build-Own-Operate) Mtambo wenye uwezo wa kuzalisha umeme wa MW 100 kwa kutumia mafuta mazito eneo la Tegeta-Salasala, Dar es Salaam.
Katika Ukurasa wa 52 Aya ya 2 ya Taarifa ya PAC, Kamati imependekeza Mtambo huo utaifishwe.
Ufafanuzi:
Mheshimiwa Spika, Kulingana na Mkataba wa PPA kati ya
TANESCO na IPTL, majukumu ya IPTL yalikuwa ni kujenga, kumiliki na
kuendesha (Build, Own and Operate – BOO). Hivyo, kutaifisha Mtambo huo
ni kukiuka makubaliano katika Mkataba wa PPA wa tarehe 26 Mei 1995,
ukiukwaji wa aina hii ukitokea unaweza kuingiza Serikali katika mgogoro
mkubwa ikiwa ni pamoja na kushtakiwa kwenye Mahakama za kibiashara za
kimataifa. Aidha utaifishaji wa miradi ya uwekezaji binafsi itakuwa ni
njia ya kufukuza wawekezaji binafsi.
|
Mheshimiwa Spika, Tarehe
26 Mei, 1995, TANESCO na IPTL walisaini Mkataba wa PPA kwa muda wa miaka
ishirini (20), kwa ajili ya kununua umeme utakaozalishwa na IPTL. Kwa
mujibu wa Mkataba huo, IPTL ilitakiwa kuiuzia TANESCO umeme usiopungua
Asilimia 85 ya uwezo wa Mtambo (minimum off take). Hata hivyo,
uzalishaji wa umeme haukuanza mara moja kutokana na mgogoro uliotokea
kati ya TANESCO na IPTL kuhusu gharama halisi za uwekezaji na namna ya
kukokotoa Capacity Charges. Hivyo, IPTL ilianza kuzalisha umeme
tarehe 15 Januari, 2002. Kutokana na hali hiyo muda wa miaka 20 ya
Mkataba ulianza kuhesabiwa tarehe 15 Januari, 2002 baada ya kuanza
uzalishaji (Commercial Operation Date).
Mheshimiwa Spika, Pamoja
na mambo mengine muhimu yaliyokuwemo katika PPA, Kifungu Na. 6 cha
Mkataba huo kinaipa TANESCO wajibu wa kulipa malipo yaliyotajwa hapo juu
na kwamba endapo kutakuwa na mgogoro wowote kuhusiana na malipo hayo (Disputed Amount), itafunguliwa Akaunti maalum (Escrow Account)
ya kuhifadhi fedha hizo hadi pale pande mbili zitakapokubaliana juu ya
uhalali wa malipo yanayobishaniwa. Aidha chini ya PPA, migogoro yote
kuhusiana na masuala ya utekelezaji wa Mkataba huo ilitakiwa
kuwasilishwa na kuamuliwa na Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa
Migogoro ya Uwekezaji (ICSID) ya London. Hivyo, ilikuwa ni jukumu la
kila mhusika katika Mkataba huu kuwasilisha malalamiko yake ICSID
yanapotokea.
Katika Ukurasa wa 8 Aya ya 2 ya Taarifa ya PAC imeelezwa
kuwa mwaka 2004 TANESCO ilifungua shauri la ICSID 2 kupinga kiasi
kikubwa cha tozo ya Capacity Charge.
Ufafanuzi
Mheshimiwa Spika, Taarifa hiyo siyo kweli kwani TANESCO
haijawahi kufungua shauri lolote ICSID ya London au Mahakama yo yote
dhidi ya Standard Charterd Bank kupinga kiasi kikubwa cha Capacity Charge
kama inavyoelezwa katika Taarifa ya PAC. Shauri la ICSID 2
lilifunguliwa tarehe 31 Oktoba 2010 na Standard Chatered Bank Hong Kong
(SCBHK) kwa ajili ya kudai malipo ya deni ililonunua kutokana na mkopo
uliotolewa na mabenki ya ushirika ya Malaysia kwa IPTL. Wahusika katika
Shauri hilo la ICSID 2 ni SCBHK na TANESCO na wala siyo TANESCO na
IPTL.
Mheshimiwa Spika, Tarehe 12 Februari, 2014 ICSID ilitoa
uamuzi kuhusiana na Shauri la SCBHK na TANESCO na kuwashauri wakae
kukokotoa upya malipo ya Capacity Charge. Hata hivyo, ilikuwa
vigumu kwa pande hizo kutekeleza uamuzi huo kutokana na pande hizo
kutokuwa na Mkataba wa kibiashara baina yao. Vile vile, kupitia Shauri
la Madai Na. 60/2014, lililofunguliwa Mahakama Kuu ya Tanzania na IPTL
tarehe 4 Aprili, 2014 ilizuia utekelezaji wa maelekezo hayo.
|
3. Mgogoro kati ya IPTL na TANESCO
Mheshimiwa Spika,
Migogoro kati ya TANESCO na IPTL ilianza muda mfupi baada ya PPA
kusainiwa tarehe 26 Mei 1995. IPTL waliitaka TANESCO wakubaliane bei za
kununua umeme kwa kuzingatia gharama za uwekezaji. Pande hizo mbili
zilishindwa kukubaliana gharama za Capacity Charge kwa vile TANESCO
walidai kuwa gharama zilizoainishwa na IPTL ni kubwa kuliko gharama
halisi za uwekezaji. Mwaka 1998, TANESCO iliajiri Kampuni ya Mawakili ya
Mkono & Co Advocates kutoa huduma za kisheria kwa kushirikiana na Huntons & Williams
ya Marekani. Kutokana na tofauti za gharama za Uwekezaji, Mawakili hawa
waliishauri TANESCO ifungue Kesi ICSID nchini Uingereza dhidi ya IPTL
ili kupinga gharama hizo.
Mheshimiwa Spika, Kwa
kuzingatia ushauri huo wa Mawakili, TANESCO ilifungua Kesi Na.ARB/98/8
ya mwezi Agosti, 1998 ikidai kuwa gharama halisi za uwekezaji ni Dola za
Marekani milioni 90 na siyo milioni 163.53 kama ilivyodaiwa na IPTL.
Aidha, IPTL ilidai kuwa kiwango cha marejesho ya uwekezaji (Internal Rate of Return-IRR) ni Asilimia 23.10 ambacho pia kilipingwa na TANESCO.
Mheshimiwa Spika, Tarehe 12 Julai, 2001, ICSID ilitoa uamuzi wa Kesi hiyo pamoja na mambo mengine kwamba:-
i. Gharama halisi za
uwekezaji zikiwemo Mtambo na nyumba za wafanyakazi wa IPTL
zilizoainishwa katika hesabu ya IPTL zilikuwa ni Dola za Marekani
milioni 163.53 lakini ICSID iliona kuwa gharama halisi ni Dola za
Marekani milioni 127.20;
ii. Kiwango cha marejesho ya uwekezaji (Internal Rate of Return-IRR) ilikuwa Asilimia 22.31 badala ya Asilimia 23.10 iliyodaiwa na IPTL; na
iii. TANESCO na IPTL
wakubaliane mfumo wa malipo ya kununua umeme ukizingatia gharama halisi
za uwekezaji na kiwango cha marejesho ya uwekezaji (IRR) cha Asilimia
22.31 kwa kutumia financial model iliyokubalika na ICSID.
Katika Ukurasa wa 11 Aya ya 2 ya Taarifa ya PAC, imeelezwa
kuwa mtaji wa uwekezaji katika Mtambo wa IPTL ni Shilingi 50,000/= na
kwamba huo ndio ungetumika kukokotoa Capacity Charges ili kulipa tozo ndogo kuliko ilivyo sasa.
Ufafanuzi
Mheshimiwa Spika, Maelezo hayo siyo sahihi. Ukweli
ni kwamba kutokana na maamuzi ya ICSID 1 ya tarehe 12 Julai, 2001,
gharama za ujenzi wa Mtambo wa Tegeta ni Dola za Marekani 127.20 kama
ilivyoelezwa katika Ukurasa wa 47 Aya ya 4 ya Taarifa ya Mdhibiti
na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. Katika Taarifa hiyo, pia
imeelezwa kuwa ilikubalika kuwa uwiano wa deni na mtaji utakuwa 70:30.
Hii ikiwa na maana kwamba, deni ni Dola za Marekani milioni 89.04 na
mtaji ni Dola za Marekani milioni 38.16. Uamuzi huo haujabadilishwa na
Mahakama yo yote au mtu ye yote.
Mheshimiwa Spika, Tunakubaliana kwamba fedha
iliyopokelewa kutoka Mabenki ya Ushirika ya Malaysia kama mkopo ni Dola
za Marekani milioni 85.86 ambazo kati ya Dola za Marekani milioni 105
zilizokuwa zimeidhinishwa. Swali la kujiuliza, je Mtambo huo
ulikamilikaje kwa gharama ya Dola za Marekani milioni 85.86, huku
gharama halisi ya ujenzi wa Mtambo wa Tegeta ikawa Dola za Marekani
milioni 127.20?
Mheshimiwa Spika, Ni dhahiri kwamba kuna matumizi ya
zaidi ya Dola za Marekani milioni 38.16 ambazo pia zimetumika kwenye
uwekezaji. Taarifa ya Kamati ya PAC haikuonesha fedha hiyo kuwa sehemu
ya uwekezaji.
|
Mheshimiwa Spika, Tarehe
30 Juni, 2004, Kampuni ya Mawakili iliyokuwa ikiiwakilisha TANESCO
katika kesi ya kwanza ya usuluhishi, Kampuni ya Mkono & Co
Advocates, iliishauri TANESCO iendelee kupinga kiwango cha malipo ya Capacity Charge
kilichokuwa kimeafikiwa tarehe 12 Julai, 2001 na pande hizi mbili
katika Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Migogoro ya Kibiashara
(ICSID) ya London. Hii ilikuwa ni miaka miwili tu baada ya usuluhishi
uliochukua miaka minne kukamilika na Mtambo kuanza kuzalisha umeme
tarehe 15 Januari, 2002.
Mheshimiwa Spika, Hata
hivyo, baada ya ushauri huu, Mawakili hawa (Mkono & Co. Advocates)
hawakuishauri TANESCO ifungue kesi katika Mahakama za Tanzania wala
katika Mahakama ya Usuluhishi wa Migogoro ya Kimataifa (ICSID) ya
London.
Mheshimiwa Spika, Hadi
kufikia tarehe 5 Septemba, 2013 wakati Mheshimiwa Jaji Utamwa anatoa
hukumu yake juu ya mgogoro wa Wanahisa wa IPTL hapakuwepo na kesi yo
yote kwenye Mahakama yo yote ya kupinga gharama za Capacity Charge kati ya TANESCO na IPTL, iwe katika Mahakama za ndani au za nje. Kwa kutokuwepo Msuluhishi (Broker)
katika suala hili, madai yo yote ya TANESCO yanakuwa ni madai ya upande
mmoja ambayo kisheria hayawezi kuchukuliwa kuwa ndiyo madai halisi.
Kwa sababu hiyo haikuwepo formula rasmi ya kuutatua mgogoro huo zaidi ya majadiliano na maafikiano kati ya pande mbili (TANESCO na IPTL).
4. Uuzaji wa Hisa za VIP
MATUKIO YA PICHA KUTOKA BUNGENI DODOMA
Waziri
Mkuu, Mizengo Pinda akizungumza na Mbunge wa Bariadi Mashariki, John
Cheyo kwenye viwanja vya Bunge mjini Dodoma Novemba 27, 2014.
Spika wa Bunge Anne Makinda akizungumza, Bungeni Mjini Dodoma Novemba 27, 2014.
Waziri
Mkuu, Mizengo Pinda akizungumza na Mbunge wa Bariadi Mashariki, John
Cheyo kwenye viwanja vya Bunge mjini Dodoma Novemba 27, 2014.
Waziri
Mizengo Pinda akizungumza na Mbunge wa Maswa Magaribi, John Cheyo,
kwenye viwanja vya Bunge Mjini Dodoma Novemba 27, 2014. (Picha na Ofisi
ya Waziri Mkuu)
Waziri
Mkuu, Mizengo Pinda akiteta na Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole-
Sendeka kwenye viwanja vya Bunge Mjini Dodoma Novemba 27, 2014. (Picha
na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Waziri
Mkuu, Mizengo Pinda akizungumza na Waziri wa Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe (katikati) na Mbunge wa Lshoto,
Henry Shekifu kwenye jengo la Utawala la Bunge mjini Dodoma Novemba 27,
2013. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
No comments:
Post a Comment