Tuesday, December 2, 2014

TMF YAFADHILI WANAHABARI TISA KWENDA ACCRA NCHINI GHANA KUPATA MAFUNZO

 Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Vyombo vya Habari Tanzania (TMF), Ernest Sungura. (Imeandaliwa na mtandao wa habari za jamii.com)
 Mkufunzi wa Masuala ya Biashara za Habari kutoka Accra Ghana,  Nuamah Eshun (katikati), akizungumza katika hafla ya kuwaaga wanahabari hao Dar es Salaam leo asubuhi, kabla ya kuondoka  kwenda nchini humo kwa mafunzo hayo ya siku 10. Eshun atakuwa ni mmoja wa wakufunzi wa mafunzo hayo. Kulia ni Ofisa Mwandamizi wa Misaada wa TMF, Alex Kanyambo na  Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Vyombo vya Habari Tanzania (TMF), Ernest Sungura.
 Baadhi ya wanahabari waliopo katika safari hiyo ya mafunzo.
 Wanahabari hao wanaosafiri wakimsikiliza Mkufunzi wa Masuala ya Biashara za Habari kutoka Ghana,  Nuamah Eshun.
Wanahabari hao wakiwa katika picha ya pamoja kabla ya 
kuanza kwa safari hiyo.
Wanahabari hao wakienda kupanda gari, tayari kwa safari ya kwenda Accra nchini Ghana kwa mafunzo ya siku 10 kwa ufadhili wa Mfuko wa Vyombo vya Habari Tanzania (TMF).

MFUKO wa Vyombo vya Habari Tanzania (TMF), umewafadhili wanahabari kutoka vyombo mbalimbali nchini kwenda Accra nchini Ghana kupata mafunzo. Mafunzo haya yanalenga kuwajengea uwezo katika maeneo ya utawala na uongozi, biashara, masoko na kuboresha maudhui katika vipindi vyao kama namna ya kuchochea mabadiliko ya kimfumo katika vyombo vyao.
Akizungumza katika hafla ya kuwaaga wanahabari hao wapatao 9 iliyofanyika Makao Makuu ya TMF Upanga Dar es Salaam leo, Mkurugenzi Mtendaji wa TMF, Ernest Sungura alisema TMF imekuwa ikiwawezesha wanahabari kupata mafunzo ya aina mbalimbali ndani nan je ya nchi.
Alisema wanahabari hao wanakwenda nchini humo ambapo watapata mafunzo kwa siku 10 kuanzia Disemba 2 hadi 13 mwaka huu.
“Waliochaguliwa kwenda kupata mafunzo hayo ni baadhi ya wakuu wa vitengo kutoka vyombo vya habari, mameneja, wamiliki wa vyombo vya habari na maofisa masoko na mauzo na waandaaji wa vipindi mbalimbali vya redio” alisema Sungura.
Aliongeza kuwa tangu mwaka 2008 TMF imeweza kufadhili vyombo zaidi ya 120 na wanahabari zaidi ya 500 kupitia aina ya ruzuku mbalimbali. Kati ya vyombo 120 vilivyofadhiliwa na TMF, 31 vimepewa ruzuku inayolenga kuimarisha utendaji wao katika masuala ya utawala na uongozi, biashara, masoko na kuboresha maudhui katika vipindi mbalimbali.
Alisema katika safari hiyo vituo vya redio vitano vimebahatika kuchaguliwa ambavyo ni CG Fm (Tabora), Standard FM (Singida), Kahama FM (Kahama), Triple A FM (Arusha) na Jogoo FM (Songea)-

No comments: