Mchakato
wa kumpata mgombea urais ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambaye
atabeba jukumu la kupeperusha bendera ya chama hicho ili kukipa ushindi
katika Uchaguzi Mkuu Oktoba mwaka huu, sasa tunahesabu siku.
Baadhi ya
makada wa chama hicho wakiwemo wajumbe wa Kamati Kuu na Halmashauri Kuu
ya Taifa (NEC), wanasema mchakato huo huenda ukaanza Mei mwaka huu.
Akizungumza
na Mwandishi wetu, Mjumbe wa NEC kutoka mkoani Arusha ambaye hakutaka
jina lake liandikwe, alisema katika uchaguzi wa mwaka huu, CCM
kitaandika historia ya kumteua mgombea urais mwenye vigezo vyote.
Alisema
mgombea huyo ni yule ambaye atakidhi vigezo 13 ili aweze kukivusha chama
hicho kiendelee kushika dola si kuteua mgombea anayetokana na shinikizo
la makundi ya watu mbalimbali kama ilivyoanza kujionesha kwa baadhi ya
wagombea wenye dhamira ya kuwania nafasi hiyo.
Mjumbe
huyo alikwenda mbali zaidi na kusisitiza kuwa, chama hicho kina
utaratibu mzuri wa kuchagua wagombea wake kwenye nafasi ya urais, ubunge
na madiwani ambao ndio utazingatiwa katika kuwapata wagombea si
vinginevyo.
"Chama
kikichagua mgombea kwa sababu ya ushabiki na kelele za makundi ya watu
kudai mwanachama fulani ndiye anayefaa kuwa rais na kutaka achukue fomu
watamuunga mkono, nchi haitakuwa salama na sababu tunazo.
"Lazima
tujiulize kwanini iwe yeye wakati kuna baadhi ya makada ndani ya CCM
wanaotajwa kutaka kuwania urais wakiwa na sifa zinazokubalika ndani ya
chama kuliko huyo wanayemtaka...chama hakiwezi kusikiliza maneno ya watu
kwani nafasi yenyewe ni nyeti,"alisema.
Aliongeza
kuwa, uteuzi wa mgombea urais CCM baada ya wagombea wote kuchukua fomu
za kuomba kuwania nafasi hiyo, kila mmoja atatakiwa kutafuta wadhamini
kwenye mikoa 10 na kuzirudisha kwa mchakato mwingine.
Majina ya
wagombea hao yatapelekwa kwenye Kamati ya Maadili ambayo itayapitia na
baadaye kwenda Kamati Kuu kwa ajili ya uteuzi wa majina matano.(V.S)
"Haya
majina matano yatapelekwa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ili yaweze
kupigiwa kura na kupatikana majina matatu ambayo yatapelekwa katika
Mkutano Mkuu ambao nao utapiga kura ili kumpata mgombea mmoja," alisema.
Sifa za wagombea urais
Mjumbe
huyo aliongeza kuwa, ili mgombea urais wa CCM aweze kuchaguliwa katika
nafasi hiyo mbali ya kupitia taratibu alizozitaja awali ndani ya chama:
kwanza ;
anapaswa kuwa na uwezo wa kuliongoza Taifa kwa kuzingatia uzoefu
alionaokatika uongozi wa shughuli za Serikali, umma na taasisi.
Pili; awe mwadilifu, mwenye hekima na busara.
Tatu; awe na elimu ya kiwango cha Chuo Kikuu au inayolingana na hiyo.
nne; awe
mwenye upeo na uwezo mkubwa wa kudumisha, kuimarisha na kuendeleza
Muungano wetu, umoja, amani na utulivu wetu pamoja na mshikamano wa
kitaifa.
Tano; awe
mtu wa kuona mbali, asiyeyumbishwa, mwenye uwezo wa kufanya uamuzi wa
busara kuhusu masuala nyeti na muhimu ya Taifa kwa wakati unaofaa.
sita; awe
na upeo mkubwa usiotiliwa shaka kuhusu masuala ya kimataifaili aweze
kuwa kiungo imara kati ya nchi yetu na Dunia yote kwa jumla.
Saba;
asiwe mtu mwenye hulka ya udikteka au ufashisti bali aheshimu na
kuilinda Katiba ya nchi, sheria, utawala bora, kanuni na taratibu za
utawala bora.
nane; awe
mtetezi wa wanyonge, kusimamia haki za binadamu, mzingatiaji makini wa
maendeleo ya raia wote na asiwe na tamaa ya kujitafutia umaarufu wake
binafsi.
Tisa; awe mstari wa mbele kuzifahamu, kuzieleza, kuzitetea na kuzitekeleza Sera za CCM na Ilani ya CCM ya Uchaguzi.
kumi; awe mpenda haki na jasiri wa kupambana na dhuluma,maovu yote nchini.
kumi na moja; asitumie nafasi yake ya uongozi kujilimbikizia mali.
Kumi na mbili; awe ni mtu anayekubalika na wananchi.
kumi na
tatu; awe makini katika kuzingatia masuala ya uwajibikaji wa uongozi,
watendaji, asiyevumilia uzembe katika utekelezaji wa majukumu ili kuinua
nidhamu ya kazi, tija na ufanisi.
Aliongeza
kuwa, kati ya sifa 13 za mgombea urais CCM zilizotajwa na Mjumbe wa
NEC, kutokana na uchanga wanchi yetu, lazima mgombea awe na upeo mkubwa
usioatiliwa shaka kuhusu masuala ya kimataifa ili aweze kuwa kiungo
imara kati ya nchi yetu na Dunia yote kwa jumla.
No comments:
Post a Comment