Friday, November 27, 2015

WAZIRI MKUU AWASIMAMISHA KAZI MAAFISA ​WATANO WA TRA

tr6 
Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa  akisalimiana na Kamishina Mkuu wa  Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Rished Bade na Naibu wake, Lusekelo Mwaseba (wapili kulia ) baada ya kuwasili kwenye bandari ya Dar es salaam kutaka maelezo kuhusu upotevu wa makontena 349 yenye kodi ya serikali ya thamani ya shilingi bilioni 80, Novemba 27, 2015. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
tr7 
Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa  akimwonyesha orodha ya makontena 349 yenye kodi ya serikali ya thamani ya shilingi bilioni 80 yaliyotoka kwenye bandari ya Dar es salaam bila kulipiwa kondi, Kamishina Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania , Rished Bade wakati alipotaka maelezo kuhusu upotevu  wa makontena hayo, bandarini jijini Dar es slaam Novemba 27, 2015. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
tr9 
Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa  akimkabidhi Kamishina Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Rished Bade orodha ya makontena  349 yenye kodi ya serikali ya thamani ya  shilingi bilioni 800 yalitoka kwenye bandari ya Dar es salaam bila kulipiwa kodi. Mheshimiwa Majaliwa alikwenda kwenye bandari ya Dar es salaam Novemba 27, 2015 kutaka maelezo kuhusu kupotea kwa makontena hayo. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
tr10 
Waziri Mkuu, Majliwa Kassim Majaliwa akizungumza kwenye bandari ya Dar es salaam alikokwenda Novemba 27, 2015 kutaka maelezo ya makontena 349 yaliyotoka kwenye bandari ya Dar es salam bila kulipiwa kodi na kuikosesha serikali shilingi billioni 80. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
…………………………………………………………………………
*Ni kwa upotevu wa makontena 349, yana thamani ya sh. bilioni 80/-
WAZIRI MKUU Majaliwa Kassim Majaliwa amewasimamisha kazi maafisa watano na watumishi watatu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kutokana na upotevu wa makontena 349 yenye thamani ya zaidi ya sh. bilioni 80/-.
Akizungumza na viongozi wa Mamlaka ya Bandari pamoja na viongozi wa TRA katika ziara ya kushtukiza leo mchana (Ijumaa, Novemba 27, 2015), Waziri Mkuu amewataka Kamishna Mkuu wa TRA, Bw. Rished Bade na Naibu Kamishna Mkuu wa TRA, Bw. Lusekelo Mwaseba wahahakikishe wanashirikiana na polisi kufuatilia upotevu huo na kwamba fedha hizo zinapatikana na zinarudi Serikalini.
Akitangaza uamuzi huo baada ya kufanya kikao na baadhi ya viongozi wa Serikali bandarini hapo, Waziri Mkuu aliwataja maafisa waliosimamishwa kazi kuwa ni Kamishna wa Forodha, Bw. Tiagi Masamaki na Mkuu wa Kituo cha Huduma kwa Wateja, Bw. Habibu Mponezya.
“Hawa wanasimamishwa kazi. IGP ninaagiza hawa watu wakamatwe na kuisaidia polisi. Hati zao za kusafiria zikamatwe na mali zao zikaguliwe kama zinaendana na utumishi wa umma,” alisema Waziri Mkuu.
Maafisa wengine waliosimamishwa kazi ni Mkuu wa kitengo cha TEHAMA, Bw. Haruni Mpande, Bw. Hamisi Ali Omari (hakutaja ni wa idara gani), na Mkuu wa Kitengo cha Bandari Kavu (ICD In-Charge), Bw. Eliachi Mrema. “Hawa wanasimamishwa kazi hadi uchunguzi utakapokamilika na pia wawe mikononi mwa polisi,” alisema.
Pia aliagiza watumishi watatu wa mamlaka hiyo wahamishwe kutoka Dar es Salaam na kupelekwa mikoani. Watumishi hao ni Bw. Anangisye Mtafya, Bw. Nsajigwa Mwandengele na Bw. Robert Nyoni.
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amemwagiza Katibu Mkuu wa Hazina, Dk. Servacius Likwelile ambaye alikuwepo kwenye kikao hicho, kuhakikisha kuwa anapeleka wataalamu kutoka Wakala wa Serikali Mtandao (e-Govt) haraka iwezekanavyo ili wakakague mifumo ya taarifa na kubaini jinsi ambavyo wizi huo unafanyika.
“Ninataka uchunguzi uanze kufanyika mara moja, tafuteni njia ambazo zinatumika kama mianya ya wizi kutokea hapa bandarini hadi kwenye ICDs. Nataka hayo makontena yatafutwe hadi yajulikane yako wapi, na fedha hiyo ihakikishwe inarudi serikalini,” alisema.
Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Bw. Ernest Mangu, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Dkt. Florens Turuka, Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Dkt. Shaaban Mwinjaka, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya DSM, Suleiman Kova, Mkurugenzi wa Mamlaka ya Bandari (TPA), Bw. Awadh Massawe na viongozi mbalimbali kutoka TRA na TPA.
Mapema akijibu maswali ya Waziri Mkuu, Kamishna Mkuu wa TRA, Bw. Bade alikiri kwamba kuna upotevu wa makontena ambao huwa unafanyika kati ya bandarini na ICDs na hasa ICD ya Ubungo. Akitoa ufafanuzi, alisema kwamba walifanya ukaguzi kwenye ICD moja na kukuta makontena 54 yamepotea kwa njia za wizi. “Hata hivyo, tulipoendelea na ukaguzi, namba iliongezeka na kufikia 327. Tunaendelea kufuatilia kwa kushirikiana na TAKUKURU. Mmiliki wa ICD ametakiwa kulipa faini sh. bilioni 12.6/- na ameshalipa sh. bilioni 2.4/-,” alifafanua.
Alipoulizwa na Waziri Mkuu kama ana majina ya watumishi wanaohusika na wizi huo, Bw. Bade akakiri kwamba anayo lakini siyo kwa wakati huo labda ayapate kutoka kwa wasaidizi wake. Ndipo Waziri Mkuu akamuonyesha orodha ya makontena 349 yenye taarifa zote hadi namba za magari yaliyobeba mizigo hiyo na Bw. Bade akakiri kwamba orodha hiyo ni ya kweli.
“Kwa utaratibu huo hatuwezi kufika, labda baadhi ya watu waondolewe kazini”. Ndipo akaanza kutaja majina ya maafisa hao waliosimamishwa kazi.

No comments: