Wednesday, June 14, 2017

AFYA YAKO. Jinsi Ya Kupunguza Uzito Kwa Kutumia Saladi

Ulaji saladi ya spinachi, matunda ya apple na parachichi unaweza kumsaidia mtu kuwa na uzito unaotakiwa kiafya.

Kabla mtu hajaanza kula mlo wake wa asubuhi, mchana au usiku anashauriwa aanze na mboga za majani za spinachi au aina nyingine.  Ulaji wa aina hii unamwezesha mtu kula kidogo vyakula vyenye wanga, sukari au mafuta ambavyo vinasababisha kuongezeka uzito na unene.

Saladi ya mboga za majani hujaza tumbo na kumfanya mtu ajihisi ameshiba na hivyo kuzuia tabia ya kutamani kula hasa vyakula vya wanga au sukari.  Mboga za majani za spinachi pia, zina kirutubisho kinachoitwa thylakoids, ambacho kinachochea mwili kuzalisha homoni inayopunguza hamu ya mtu kutaka kula hasa vyakula vyenye sukari.

Kuhusu matunda ya apple, kwa siku mtu akila tunda moja ni jambo zuri.  Matunda ya apple yana maji na nyuzi lishe ambazo zinalifanya tumbo kujisikia limeshiba.  Matunda ya epo pia yana kirutubisho cha pectin, ambacho kinakifanya chakula kilichomo tumboni kusagwa kwa muda mrefu na kumfanya mtu kujisikia ameshiba.

Mtu akila tunda zima la epo (siyo juisi), kabla ya mlo atajisikia hali ya kushiba na hivyo atakula kidogo chakula cha wanga au sukari.
Kwa upande wa matunda ya parachichi, kula nusu ya tunda hilo kwa siku kunaupa mwili mafuta bora kiafya na nyuzi lishe ambazo zinamfanya mtu ajisikie ameshiba muda mwingi na kutokutamani chakula mara kwa mara.

Anachopaswa kufahamu mtu ni kwamba kula vyakula vya wanga, sukari au mafuta kwa wingi ndipo mwili unaongezeka uzito na unene kupita kiasi. 

No comments: