Sunday, June 4, 2017

Makamu wa Rais aagiza adhabu kali kwa viwanda, migodi inayoharibu mazingira

Butiama. Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan ameagiza kuchukuliwa kwa hatua kali za kisheria kwa viwanda na migodi inayofanya shughuli zake za uzalishaji kwa kuharibu mazingira ikiwamo utitirishaji wa kemikali  katika makazi ya watu.

 Amesema  kufanya hivyo kunahatarisha usalama wa wananchi na viumbe hai wengine.

Mama Suluhu Hassan ametoa agizo hilo Juni 4, kijijini Butiama mkoani Mara wakati akihutubia wananchi katika kilele cha siku ya mazingira Duniani.

Amesema uharibifu wa mazingira ukiachwa uendee nchini ni hatari kwa usalama wa maisha na viumbe na hivyo ni muhimu kwa viongozi katika ngazi zote kuchukua hatua zitakazosaidia kukabiliana na vitendo hivyo.

“Kutozingatia hifadhi ya mazingira kunaweza kusababisha kuparaganyika kwa mfumo wa ikolojia  na kufanya maisha yetu na ya vizazi vijavyo kuwa mashakani”. amesema

Amesema katika kuadhimisha siku ya mazingira Dunia viongozi wanapaswa kuchukua hatua za kuelimisha wananchi na kuwahamasisha ili kila mtu ashiriki katika juhudi za kuwa na uchumi unaozingatia hifadhi ya mazingira.

No comments: