Thursday, December 14, 2017

Rais Mnangagwa aomba Zimbabwe iondolewe vikwazo

Rais mpya wa Zimbabwe Emmerson Mnangagwa, ametoa wito wa kuondolewa vikwazo vilivyowekwa na mataifa ya magharibi dhidi ya taifa hilo.

Kadhalika, amesema kwamba huenda uchaguzi ulioratibiwa kufanyika Julai mwaka ujao ukafanyika mapema.

Akizungumza na viongozi wa chama tawala cha ZANU-PF, Bw Mnangagwa amesema vikwazo hivyo vinalemaza ufanisi wa taifa hilo, na kusema vinafaa kuondolewa bila masharti yoyote.

Amesema serikali ya taifa hilo itahakikisha kwamba uchaguzi umefanyika kwa njia huru na haki.

"Tunataka kuondolewa vikwazo vya kiuchumi na kisiasa ambavyo vimelemaza maendeleo ya taifa hili bila masharti yoyote.

"Tunafahamu kwamba kutengwa sio jambo la kujitosheleza, kwani kuna mengi ya kuafikia kupitia umoja na ushirikiano unaofaidi pande zote, ambao unatambua mahitaji ya kipekee ya taifa letu.

"Serikali yetu itaanza upatanisho mpya ili kudhibitisha kwamba tuko miongoni mwa jamii ya kimataifa."

Bw Mnangagwa alichukua uongozi mwezi jana baada ya Robert Mugabe aliyekuwa ameongoza taifa hilo kwa miaka 37 kuondolewa madarakani kwa usaidizi wa jeshi.

No comments: