Tuesday, January 16, 2018

Waziri Biteko achukizwa na utendaji kazi wa STAMICO


Uongozi wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) umetakiwa kutoa maelezo kwa serikali katika kipindi cha muda mfupi kueleza sababu za kuendelea kusalia kuwepo kwa shirika hilo kutokana na kukosa umakini katika utendaji.

Kauli ya kuchukizwa na utendaji wa Shirika hilo imetolewa leo na Naibu Waziri wa Wizara ya Madini, Dotto Mashaka Biteko Wakati akizungumza na Uongozi pamoja na watumishi wa Shirika hilo Jijini Dar es salaam.

Biteko amesema kuwa serikali ilikuwa na makusudi mazuri kufuatia mabadiliko ya Sera za kiuchumi kwa STAMICO kuwekwa kwenye orodha ya mashirika yanayotakiwa kubinafsishwa, lakini katika kipindi chote cha utendaji hakuna msaada wowote ambao Shirika hilo limeipatia serikali zaidi ya kuingiza hasara.

Amesema kuwa pamoja na STAMICO kuwa na jukumu la kuendeleza migodi ya Madini na kufanya biashara za Madini ikiwemo mradi wa dhahabu wa STAMIGOLD uliopo Biharamulo Kagera na mgodi wa Makaa ya Mawe KABULO uliopo Ruvuma lakini Taasisi hiyo imeshindwa kuendeleza migodi kwa ufanisi.

Amesema kuwa Shirika hilo linapaswa kutafakari kwa umakini utendaji wake kwani limeongeza hasara kwa serikali ya deni la shilingi Bilioni 1.77 hivyo serikali haiwezi kuendelea kusalia kuwa na Shirika linalozalisha madeni kuliko matokeo makubwa na faida.

Biteko amesema kuwa imani bila matendo ni uduni wa fikra hivyo kuwa na cheo kikubwa serikalini halafu uzalishaji ni mdogo ni kipimo halisi cha utendaji wa mazoea walionao watumishi wengi ambao wamekosa uzalendo na bidii katika utendaji kazi.

No comments: