Thursday, February 22, 2018

Father Raymond: Aliyetekeleza mauaji ya Akwilina aliombe msamaha Taifa

Father Raymond Mayanga wa Parokia ya Yohana Mbatizaji Ruhanga ambaye ameendesha ibada ya kuaga mwili wa marehemu Akwilina katika Chuo cha Usafirishaji (NIT) amemtaka aliyetekeleza mauaji ya mwanafunzi huyo aliombe msamaha Taifa.

Father Raymond amesema hayo leo Februari 22, 2018 na kudai kuwa jukumu hilo wameiachia serikali ya awamu ya tano na vyombo vyake vya usalama kuwa endapo watampata mtu huyo wahakikishe kuwa analiomba taifa msamaha kwani kitendo alichofanya kimewaumiza Watanzania hivyo hata akifungwa miaka 30 haitasaidia kwa kuwa tayari Akwilina ametangulia mbele ya haki na hatoweza kurudi.

"Mimi kama mtoto wa Mungu kama wengine walivyo watoto wa Mungu niwaombe tufanye kazi ya upatanishi na naomba wale ambao wana hiyo nafasi na kwa hili lililotokea kwa mwanetu Akwilina limetuumiza na kwa jinsi lilivyotuumiza nafikiri linahitaji kuponywa na namna moja tu ya kuliponya tunawaomba wale wahusika ambao wana madaraka ya kuweza kulisaidia. Huyu aliyefanya kitendo hiki baada ya kujulikana aliombe taifa hili msamaha ni hicho tu hatuna namna nyingine hata tukimfunga miaka 30 au 40 Akwilina hawezi kurudi amekwenda lakini aliyefanya huenda kwa nia nzuri ikitakoea bahati mbaya tunaomba vyombo vinavyohusika vikimaliza utaratibu wake akajulikana huyo mtu hata kwa kupitia TV awaombe wana Mungu msamaha" alisema Father Raymond

Father Raymond aliendelea kusema kuwa

"Kheri wapatanishi maana hao wataitwa wana wa Mungu vinginevyo hatutafika mbali, tumuombe Mungu kila mmoja wetu katika imani yake leo ni Akwilina huenda kesho itakuwa ni wewe sasa hatutaki hilo liendelee, na hilo halitaendelea tu kama mtu atakubali kuomba msamaha kujinyenyekeza, kuwa mnyenyekevu na kukubali nimekosa mimi, nimekosa sana nawaomba msamaha kwisha tunaendelea kama familia hakuna asiyekosea. Lakini unapojaribu kutafuta mbinu ukaliweka hivi unaliweka vile unazidi kuumiza kwa sababu mimi kama mzazi sitaelewa

"Naomba nisema hapa bila hata kigugumizi nafikiri wenye nafasi hii si wengine ni serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tunaiomba kama ilivyojitolea kuweka haya mazishi katika level hiyo, tunawaomba pia watusaidie kwa sababu wao ndiyo wamepewa dhamana ya maisha yetu wote hapa, na sisi kama watoto wa familia hatulingani kama vidole vyetu tunaimani kwamba serikali yetu itatusaidia katika kulipatanisha, katika kurudi kufanya kazi kama watoto wa familia moja"

No comments: