Thursday, May 24, 2018

Jaji Mkuu atoa agizo hili kwa viongozi na watendaji wa Mahakama


Jaji Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahim Juma amewataka viongozi mbalimbali wa mahakama ikiwemo Naibu Wasajili, Mahakimu, Watendaji, Wakuu wa Idara na Vitengo kutenda haki kwa watumishi walio chini yao.

Jaji Mkuu ameyasema hayo leo Mkoani Dodoma wakati akifungua mkutano wa siku mbili wa baraza la wafanyakazi wa mahakama Tanzania.

“Sisi kama wasimamizi wakuu wa haki nchini tunawajibu mkuu wa kutenda haki kwa watumishi kwa vitendo, ni ukweli usiopingika kwamba kimbilio la mtumishi yeyote aliyefikwa na matatizo ni kwa kiongozi wake katika sehemu yake ya kazi, hivyo basi kila kiongozi anapaswa kufungua milango kwa watumishi waliopo chini yake” amesema Jaji Mkuu.

Jaji Mkuu ameongeza kuwa, ubora wa viongozi unapimwa kwa namna wanavyosaidia wafanyakazi walio chini yao, hivyo kuwataka viongozi hao kutokufunga milango yao kwa watumishi wanaowaongoza.

Mkutano wa Baraza la wafanyakazi wa Mahakama Tanzania umewashirikisha wajumbe kutoka kanda zote na menejimenti ya Mahakama Tanzania.

No comments: