Monday, September 17, 2018

Warejeshwa kwao DRC Walioingia nchini kwa hofu ya ebola


IDARA ya Uhamiaji mkoani Rukwa imewarudisha nchini kwao watu 15 kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), kwa tuhuma za kuingia nchini  bila sababu maalum ya hofu ya ugonjwa wa ebola.

Hayo yalibainishwa mwishoni mwa wiki na Kaimu Ofisa wa Uhamiaji mkoa wa Rukwa, Lezius Mushongi, alipozungumza na vyombo vya  habari  katika Kijiji cha Wampembe wilayani Nkasi.

Alisema kutokana na Mkoa wa Rukwa kupakana na nchi mbalimbali ikiwamo DRC, Idara ya Uhamiaji imekuwa makini katika kuhakikisha watu wanaoingia mkoani hapa kutoka nchi za nje wanakuwa na sababu za msingi.

Alisema katika kipindi cha mwezi huu raia 15 kutoka DRC  wamerudishwa kwao licha ya kuwa waliingia kwa kufuata taratibu, lakini sababu za kuingia nchini hazikutosheleza.

Baada ya kuwahoji sababu za kuja nchini mwetu na hazikuwa za msingi sana, tuliwasiliana na mamlaka za upande wa nchi yao kisha tuliwarudisha kwa nia njema," alisema.

“Sio kwao tu, hata raia wa nchi yetu kama hawana sababu za msingi za kwenda katika nchi hiyo hatuwapi vibali, kama lengo ni kusalimia na kufanya biashara wasubiri mpaka hapo ugonjwa huo utakapo kuwa umemalizika na hali itakapokuwa nzuri tutawaruhusu," alisema Mushongi.

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Joachim Wangabo, aliwapiga marufuku wakazi wa mkoa huo hususani wanaoishi katika vijiji vilivyo mwambao mwa Ziwa Tanganyika kupokea wageni, kwa sababu wanaweza kuingia mkoani humo na vimelea vya ugonjwa huo.

Mganga Mkuu wa Mkoa huo, Dk. Boniface Kasululu, alisema mpaka sasa hakuna mtu aliyeripotiwa kuugua ebola wala kuonyesha dalili na kwamba Idara ya Afya imeshachukua tahadhari iwapo lolote litatokea.

Aliwashauri wavuvi wanaofanya shughuli katika Ziwa Tanganyika kuwa makini na wasijaribu kushika wala kufanya maziko ya mtu ambaye wameukuta mwili ndani ya maji na hawajui sababu za kifo chake.

No comments: