
Mheshimiwa Samuel Sitta, Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba;
Mheshimiwa Dkt. Mohamed Gharib Bilal, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
Mheshimiwa Mizengo Peter Pinda, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Maalim Seif Sharif Hamad, Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar;
Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
Mheshimiwa Anne Semamba Makinda; Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano;
Mheshimiwa Pandu Ameir Kificho, Spika wa Baraza la Wawakilishi na Mwenyekiti wa Muda wa Bunge Maalum la Katiba ;
Mheshimiwa Rashid Othman Chande, Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Othman Makungu, Jaji Mkuu wa Zanzibar;
Viongozi Wakuu Wastaafu;
Waheshimiwa Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba;
Waheshimiwa Wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba;
Wageni waalikwa;
Mabibi na Mabwana;
Pongezi
Nakushukuru
 sana Mheshimiwa Mwenyekiti kwa kunipa fursa ya kuja kuzungumza na 
Waheshimiwa Wajumbe wa Bunge letu Maalum la Katiba katika siku hii 
muhimu na ya kihistoria kwa nchi yetu. Nimekuja kuwatakia heri na 
naungana na Watanzania wenzetu wote kuwaombea baraka za Mwenyezi Mungu, 
ili muweze kuifanya kazi yenu kwa utulivu, hekima, umakini mkubwa na 
kuimaliza kwa salama na kwa mafanikio yanayoyatarajiwa na Watanzania.
 
Natoa 
pongezi nyingi kwako na kwa Makamu wako kwa kuchaguliwa kwenu kuongoza 
Bunge hili maalumu na la kihistoria. Ushindi mkubwa mliopata ni 
kielelezo tosha cha imani kubwa na matumaini waliyonayo Wajumbe wenzenu 
kwenu. Matumaini yao ndiyo matumaini ya Watanzania wote, kwamba 
mtaliongoza vizuri Bunge hili, ili liweze kutimiza kwa ufanisi mkubwa 
jukumu lake muhimu sana katika historia ya Jamhuri ya Muungano wa 
Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Niruhusu 
pia niwapongeze kwa dhati Wajumbe wote wa Bunge Maalum la Katiba kwa 
bahati ya aina yake waliyopata ya kutunga Katiba mpya ya Jamhuri ya 
Muungano wa Tanzania. Fursa hii hutokea mara chache sana katika historia
 ya nchi yo yote na watu wake. Mkifanikiwa kuipatia nchi yetu Katiba 
nzuri majina yenu yataandikwa kwa wino wa dhahabu, katika kumbukumbu za 
historia ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
        
Ni 
matarajio ya Watanzania kuwa mtatunga Katiba itakayokubalika na wengi. 
Katiba inayotekelezeka. Katiba itakayoimarisha Muungano wetu kwa kuondoa
 changamoto zilizopo sasa. Katiba itakayoipa nchi yetu mfumo bora wa 
kuongoza na kuendesha mambo yetu. Katiba itakayoimarisha umoja, upendo, 
ushirikiano na mshikamano miongoni mwa wananchi wa Tanzania, licha ya 
tofauti zao za asili za upande wa Muungano na maeneo watokako, au 
tofauti za jinsia, rangi, kabila, dini na ufuasi wa vyama vya siasa. 
Katiba itakayodumisha amani, usalama na utulivu nchini. Katiba 
itakayostawisha zaidi demokrasia, haki za binadamu, utawala wa sheria, 
utawala bora na kudhibiti maovu.
Na, 
mwisho ingawaje siyo mwisho kwa umuhimu, Katiba itakayoweka mazingira 
mazuri kwa uchumi wa nchi kukua, na wananchi wengi kunufaika sawia na 
maendeleo yatayopatikana.
Historia ya Katiba Nchini
Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wajumbe;
Hii 
itakuwa mara ya tatu tangu kuzaliwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania 
Aprili 26, 1964, kwa nchi yetu kuwa na mchakato wa kutunga Katiba mpya. 
Mara ya kwanza ilikuwa mwaka 1965 ilipotungwa Katiba ya Muda na mara ya 
pili ni mwaka 1977 ilipotungwa Katiba ya Kudumu tuliyonao sasa. Tofauti 
na mara mbili zilizopita, safari hii mchakato unahusisha watu wengi 
zaidi. Wananchi wameshiriki moja kwa moja kutoa maoni yao kwa Tume ya 
Mabadiliko ya Katiba, na ndio watakaofanya uamuzi wa mwisho kuhusu 
Katiba mpya kwa kura ya maoni. Wananchi pia walipata nafasi ya kuchagua 
Wajumbe wa Mabaraza ya Katiba ya Wilaya yaliyojadili Rasimu ya Kwanza ya
 Katiba. Pia walipata nafasi ya kutoa maoni yao kupitia Mabaraza ya 
Katiba ya taasisi. Katika Bunge hili wapo wananchi 201 kutoka makundi 
mbalimbali.
Katika 
mchakato wa kutunga Katiba za mwaka 1965 na 1977 kulikuwapo Tume za 
Kuandaa Rasimu na Bunge Maalum la Katiba kama ilivyo katika mchakato 
huu. Hata hivyo, kwa Katiba zilizopita Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya 
Muungano pekee ndio waliounda Bunge Maalum. Safari hii Bunge Maalum 
linajumuisha Wabunge, Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na wananchi 201 
wanaotoka kwenye jamii, wakiwakilisha asasi na makundi mbalimbali ya 
Watanzania kutoka Zanzibar na Tanzania Bara. Mchakato wa sasa utaishia 
kwenye kura ya maoni itakayoshirikisha wananchi wote wa Tanzania 
wanaoruhusiwa kupiga kura. Michakato iliyopita iliishia Bunge Maalum 
pekee.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Tangu 
kutungwa kwake, tarehe 25 Aprili, 1977, mpaka sasa Katiba ya Jamhuri ya 
Muungano ya mwaka 1977 imefanyiwa mabadiliko takriban mara 14. 
Mabadiliko hayo yalitokana na kufanyika au kutokea kwa mabadiliko muhimu
 ya kiuchumi, kisiasa na kijamii katika nyakati mbalimbali hapa nchini 
na katika Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Kwa ruksa yako naomba nitaje baadhi ya mabadiliko yaliyofanywa:-
Mabadiliko
 ya 1979 yaliunda Mahakama ya Rufani ya Tanzania kufuatia kufa kwa 
Mahakama ya Rufani ya Afrika Mashariki baada ya kuvunjika kwa Jumuiya ya
 Afrika Mashariki mwaka 1977.
Mabadiliko
 ya mwaka 1980 yalifanyika baada ya kutungwa kwa Katiba ya Zanzibar, 
hivyo kulazimu Katiba hiyo kutambulika kwenye Katiba ya Jamhuri ya 
Muungano
Mabadiliko
 ya mwaka 1984 yaliweka utaratibu wa ukomo wa vipindi vya Urais ambao 
haukuwepo kabla ya hapo. Aidha, masuala ya Haki za Binadamu (Bill of 
Rights) yaliingizwa kwa mara ya kwanza katika Katiba. Vilevile, Mahakama
 ya Rufani ya Tanzania na mambo mengine ya iliyokuwa Jumuiya ya Afrika 
Mashariki yaliongezwa katika Orodha ya Mambo ya Muungano.
Mwaka 
1992, yalifanyika mabadiliko yaliyoanzisha Mfumo wa Vyama Vingi vya 
Siasa badala ya ule wa Chama kimoja uliokuwepo tangu 1965. Pia utaratibu
 wa uchaguzi wa Rais na Wabunge ulirekebishwa ili uendane na mfumo wa 
vyama vingi vya siasa. Vilevile utaratibu wa kuwa na viti maalum vya 
wanawake katika Bunge ulianzishwa. Wakati ule ilikuwa asilimia 15 ya 
Wabunge wote. Aidha, kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi yetu 
Bunge lilipewa mamlaka ya kumwajibisha Rais na Waziri Mkuu kupitia kura 
ya kutokuwa na imani.
Mabadiliko ya mwaka 1994 yaliweka mfumo mpya wa kumpata Makamu wa Rais kupitia Mgombea Mwenza.
Mwaka 
2000 na 2005, pamoja na mambo mengine yalifanyika mabadiliko yaliyopanua
 wigo wa Haki za Binadamu na kuongeza uwakilishi wa wanawake.
Umuhimu wa Mabadiliko ya Katiba
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Kufanyika
 kwa mabadiliko hayo kunathibitisha utayari wa Serikali kufanya 
mabadiliko kila ilipoonekana inafaa kufanya hivyo. Pamoja na kufanya 
yote hayo na Serikali kuwa na msimamo huo, kumekuwepo na madai 
yaliyokuwa yanajirudia ya kutaka Katiba ya Tanzania iandikwe upya. Wako 
watu walioimithilisha Katiba yetu na nguo yenye viraka vingi mno kiasi 
kwamba ingefaa kununua mpya badala ya kuendelea kuivaa.
Madai ya 
kutaka Katiba mpya yalipazwa sauti baada ya kuanza kwa mfumo wa vyama 
vingi vya siasa. Wapo waliokuwa wanadai Katiba mpya kwa imani, eti 
kwamba, itawawezesha kuishinda CCM. Lakini, si hayo tu, hata katika 
mchakato wa Serikali zetu mbili kushughulikia kero za Muungano, 
imedhihirika kuwa baadhi ya changamoto zilikuwa zinahitaji mabadiliko ya
 Katiba ili kuzipatia ufumbuzi wa uhakika na wa kudumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Kwa 
kutambua ukweli huo na baada ya kushauriana na kukubaliana na viongozi 
wenzangu wakuu wa Chama tawala na Serikali zetu mbili wakati ule, ndipo 
tarehe 31 Desemba, 2010, nikatangaza dhamira ya kuanzisha mchakato wa 
kutunga Katiba mpya. Nilieleza siku ile kuwa katika mchakato huo 
tutakuwa na ushirikishwaji mpana wa wananchi wa Tanzania kwa makundi yao
 ya jinsia, dini, siasa na shughuli wazifanyazo kujipatia riziki na kwa 
maeneo wanayotoka katika pande zetu mbili za Muungano.
Mchakato wa Katiba Mpya
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Tarehe 16
 Machi, 2011 Baraza la Mawaziri liliridhia kutungwa kwa Sheria ya 
Mabadiliko ya Katiba ya kuliongoza taifa katika mchakato wa kutunga 
Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tarehe 18 Novemba, 2011 
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilipitisha Muswada wa Sheria 
ya Mabadiliko ya Katiba. Kwa mujibu wa Sheria hiyo, mchakato wa kutunga 
Katiba Mpya ulikuwa unaanza kwa kuunda Tume ya Mabadiliko ya Katiba. 
Tume hiyo imepewa jukumu la kusikiliza maoni ya wananchi mmoja mmoja na 
kwa makundi yao ya maslahi, taasisi zao na kupitia Mabaraza ya Katiba. 
Mwishowe Tume imetakiwa kutengeneza Rasimu ya Katiba mpya 
itakayofikishwa kwenye Bunge Maalum la Katiba kujadiliwa na Katiba mpya 
kutungwa. Mchakato wa Katiba utahitimishwa kwa wananchi kupiga kura ya 
maoni ya kuamua kama wanaikubali au kuikataa Katiba mpya.
Tarehe 6 
Aprili, 2012 nilifanya uteuzi wa Wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba
 na kuwaapisha tarehe 13 Aprili, 2012. Tume ilianza kazi tarehe 2 Mei, 
2012 na kuikamilisha kwa mafanikio, hatua zote zilizoihusu na kukabidhi 
kwangu na kwa Rais wa Zanzibar, Taarifa ya Tume na Rasimu ya Katiba 
tarehe 30 Desemba, 2013. Kitendo cha Mwenyekiti wa Tume, Mheshimiwa 
Joseph Warioba kuwasilisha Rasimu hiyo mbele ya Bunge hili tukufu tarehe
 18 Machi, 2014, kinahitimisha rasmi kazi ya Tume ya Mabadiliko ya 
Katiba. Kazi inayofuatia ni ya Bunge hili kujadili, kuamua na kutunga 
Katiba mpya. Baada ya hapo Katiba mpya itafikishwa kwa wananchi kwa 
uamuzi wa mwisho kwa njia ya kupiga kura ya NDIYO au HAPANA.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Rasimu ya
 Katiba ilichapishwa kwenye gazeti la Serikali na magazeti mengine 
yanayosomwa na wananchi kama ilivyoagizwa katika Kifungu cha 20(2) cha 
Sheria ya Mabadiliko ya Katiba. Pamoja na hayo, Taarifa ya Tume na 
Rasimu ya Katiba viliwekwa wazi kwenye tovuti ya Tume kwa kila mtu 
kusoma. Inafurahisha kuona kuwa watu wengi wameisoma Taarifa ya Tume na 
Rasimu ya Katiba na kumekuwa na mjadala mpana kuhusu nyaraka zote hizo 
muhimu. Watu wengi wametoa maoni yao na wanaendelea kufanya hivyo. Kwa 
maoni yangu hili ni jambo jema sana na ni kielelezo thabiti kuwa 
demokrasia imestawi na inazidi kuota mizizi Tanzania. Pia, kwamba, 
Watanzania wako huru kushiriki na kutoa maoni yao kwa mambo 
yanayowahusu.
Pongezi kwa Tume
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Kwa mara 
nyingine tena narudia kutoa pongezi za dhati kwa Wajumbe wa Tume ya 
Mabadiliko ya Katiba chini ya uongozi wa Mheshimiwa Jaji Joseph Warioba 
akisaidiwa na Mheshimiwa Jaji Augustino Ramadhani, kwa kazi kubwa na 
nzuri waliyofanya. Kazi yao haikuwa rahisi hasa ukizingatia ukubwa wa 
nchi yetu, wingi wa watu wake, utitiri wa taasisi na pigo la kumpoteza 
Mjumbe mwenzao muhimu Dkt. Sengondo Mvungi aliyetangulia mbele ya haki 
katikati ya mchakato.
Pamoja na
 hayo, kwa bidii kubwa Wajumbe wa Tume wameweza kutembelea mikoa yote 
nchini na kuwafikia watu 351,644 waliotoa maoni yao kwa mdomo na kwa 
maandishi. Halikadhalika, walipokea na kuchambua maoni 772,211 kutoka 
kwa wananchi na taasisi mbalimbali. Baada ya kupokea maoni ya wananchi, 
kufanya utafiti na kwa kutumia maarifa na uzoefu wao, Wajumbe wakafanya 
kazi ngumu, kuliko yote, ya kutengeneza Rasimu ya Katiba iliyoko mbele 
ya Bunge hili. Ni kweli kwamba Wajumbe hawakuweza kuwafikia wananchi 
wote wa Tanzania, lakini wameweza kuwafikia wananchi wengi, ambao kwa 
kiasi kikubwa wanawakilisha taswira na mitazamo mipana ya jamii yetu.
Baadhi ya Masuala Yaliyojitokeza Katika Mjadala wa Mapendekezo ya Tume
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Tume 
imefanya kazi nzuri, yenye thamani kubwa na ya manufaa kwa taifa la 
Tanzania. Rasimu imeandikwa vizuri na kwa weledi wa hali juu. Tume 
imetoa mapendekezo ambayo kwa kiasi kikubwa yanahuisha na kuboresha 
Katiba ya nchi yetu, kwa namna ya pekee. Katiba inayopendekezwa, 
imejumuisha dhana na mambo kadhaa mapya yanayokwenda vyema na wakati 
tulionao na kuweka msingi mzuri kwa huko mbele tuendako. Kwa taratibu za
 kawaida za marekebisho ya Katiba tuliyonayo, isingekuwa rahisi kuingiza
 mambo mengi mapya kiasi hiki.
Wajumbe Wana Kazi Kubwa
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Waheshimiwa Wajumbe;
Rasimu ya
 Katiba ni kitabu kikubwa kilichosheheni mambo mengi. Kina kurasa 106, 
sura 17 na ibara 271. Wajumbe wa Bunge hili mnatakiwa kusoma na kuelewa 
vizuri kila kilichoandikwa ili muweze kufanya uamuzi ulio sahihi. 
Mnawajibika kuchambua kwa kina na umakini mkubwa kila kilichomo, sura 
kwa sura, ibara kwa ibara, sentensi kwa sentensi na hata neno kwa neno. 
Hamna budi kujiridhisha kuhusu uandishi wa vifungu vya Rasimu ya Katiba 
na kufaa kwa dhana mbalimbali zilizoingizwa na kujengeka katika Rasimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Kile 
ambacho Wajumbe mtaona kinastahili kuboreshwa au kurekebishwa au kufutwa
 msisite kufanya hivyo ili Watanzania wapate Katiba iliyo bora. 
Msipofanya hivyo kuna hatari ya kupata Katiba ambayo ni ngumu 
kuitekeleza. Aidha, tunaweza kuwa na Katiba ambayo itanung'unikiwa na 
watu wengi na kusababisha madai ya kutaka ifanyiwe marekebisho muda 
mfupi baada ya kupitishwa. Bunge hili linao wajibu maalum wa kuzuia 
balaa hilo lisitokee katika nchi yetu. Ngazi mbalimbali zilizowekwa 
katika mchakato huu ni kama chujio la kuepusha hali hiyo isitokee. Kile 
ambacho hakikuonekana katika hatua moja kitaonekana katika hatua 
inayofuata na kurekebishwa. Nawaomba fursa mliyonayo muitumie vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Nimekwishaeleza
 kuwa moja ya jambo mnalotegemewa kufanya ninyi wenzetu mliopewa dhamana
 ya kutunga Katiba ya nchi yetu ni kujiridhisha na uandishi wake. Yapo 
maoni yaliyotolewa kuhusu uandishi ambayo naomba myatafakari na kuamua 
ipasavyo. Kwa mfano, kuna baadhi ya vifungu vya Katiba vinayopendekezwa 
vimekuwa na mambo mengi mno kuliko inavyostahili Katiba kuwa (too 
prescriptive). Pia kuna mawazo kwamba baadhi ya mambo hayangetakiwa kuwa
 katika Katiba bali yawe kwenye Sheria zinazotafsiri utekelezaji wa 
Katiba yenyewe.
Yako 
mambo yaliyotajwa kwenye Katiba ambayo yanatakiwa kuelezwa wazi kuwa mtu
 hatakwenda mahakamani kuidai Serikali impatie (non justiciable). Mambo 
yaliyotajwa kwenye Katiba ni mazuri na yanavutia, lakini lazima yaendane
 na uwezo wa nchi na uchumi wake kuhimili. Simaanishi kwamba tuyatoe 
kwenye Katiba, bali yabakie kama dhamira pale uwezo wa nchi 
utakaporuhusu yatekelezwe. Tusipofanya hivyo, kuna hatari ya Serikali 
kujikuta inalaumiwa au hata kufikishwa mahakamani kila wakati kwa madai 
ya jambo moja au jingine ambayo haina uwezo nayo. Ni muhimu sana mambo 
kama hayo muyatazame ili tusije kuwa na Katiba ambayo ni ngumu 
kutekeleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Yapo pia 
maoni kuwa baadhi ya vifungu vina upungufu katika uandishi wake, hivyo 
kuhitaji kufanyiwa marekebisho. Isipofanyika hivyo kunaweza kuwepo 
athari na nyingine zinaweza kuwa mbaya. Kwa mfano, Ibara ya 2 ya Rasimu 
inayotambulisha eneo na mipaka ya nchi yetu. Ibara hiyo inasomeka kuwa 
"Eneo la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni eneo lote la Tanganyika 
likijumuisha sehemu yake ya bahari na eneo lote la Zanzibar likijumuisha
 sehemu yake ya bahari".
Maelezo 
hayo yameacha kutambua, kwa upande wa Tanzania Bara, sehemu yetu ya 
maziwa na mito ambayo ni kubwa sana. Kwa nini tuache kuitaja? Je hatutoi
 nafasi kwa nchi tunazopakana nazo siku moja wakaja kupora sehemu zetu 
hizo na sisi kukosa utetezi kwa kuwa hata Katiba yetu haikuyatambua 
maeneo hayo kuwa ni yetu? Hili ni jambo kubwa ambalo Bunge hili lazima 
mlirekebishe. Wakati ndiyo huu hakuna mwingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Jambo 
jingine kuhusu uandishi ni mgongano kati ya pendekezo la msingi la Tume 
la kuwa na muundo wa Serikali tatu na majukumu ya Serikali ya Muungano 
ambayo kimsingi ni majukumu ya Serikali za nchi washirika. Katika Rasimu
 hii malengo ya taifa yameainishwa na Serikali ya Muungano inatakiwa 
kuhakikisha kuwa malengo hayo yanatekelezwa na itoe taarifa Bungeni. 
Katika mfumo wa Serikali tatu unaopendekezwa na Tume masuala yahusuyo 
uchumi na maendeleo ya jamii kama vile kukuza kilimo, ufugaji, uvuvi, 
viwanda, biashara, pembejeo, elimu, hifadhi ya jamii na kadhalika yako 
chini ya mamlaka ya Serikali za nchi washirika. Mamlaka ya Serikali ya 
Muungano ni kwa mambo saba tu yafuatayo:- Katiba na Mamlaka ya Jamhuri 
ya Muungano, Ulinzi na Usalama wa Jamhuri ya Muungano, Uraia na 
Uhamiaji, Sarafu na Benki Kuu, Mambo ya Nje, Usajili wa Vyama vya Siasa,
 Ushuru wa Bidhaa na Mapato yasiyo ya kodi yatokanayo na Mambo ya 
Muungano.
Kwa 
Rasimu kupendekeza muundo wa Serikali tatu na kuipa Serikali ya Muungano
 majukumu ambayo haina mamlaka nayo, ni kuzusha utata na migongano kati 
ya Serikali ya Muungano na nchi washirika. Mkichagua mfumo wa Serikali 
tatu, inawalazimu muyaondoe mambo hayo kwani Serikali ya Muungano 
haistahili kuyatekeleza na wala haina uwezo wa kuweka masharti kwa 
Serikali za nchi washirika kwa mambo yaliyo kwenye mamlaka ya nchi hizo.
 Lakini kama mtaamua tuendelee na muundo wa Serikali mbili, mambo haya 
mazuri yanatekelezeka na Serikali ya Muungano bila ya matatizo. Katika 
uandishi wa Rasimu Utumishi katika Serikali ya Muungano haumo katika 
Orodha ya Mambo ya Muungano. Ni lazima liwemo. Hayo ni baadhi tu ya 
masuala yahusuyo uandishi katika Rasimu. Naamini mkiisoma Rasimu kwa 
makini mnaweza kuyagundua mengineyo.
Dhana Mpya
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Katika 
Rasimu kuna dhana mpya na mambo mapya kadhaa yaliyoingizwa ambayo 
yanabadili utaratibu wa sasa wa uendeshaji wa nchi na mambo mbalimbali. 
Nawaomba mfanye uchambuzi wa kina kwa kila kinachopendekezwa na 
kujiridhisha kuhusu kufaa kwake na manufaa yake. Fanyeni hivyo ili 
tujihakikishie kuwepo kwa mambo mazuri na uendeshaji mzuri wa shughuli 
katika taifa letu changa.
Mambo ni 
mengi na kwa ufinyu wa muda sitaweza kuyazungumzia yote. Niruhusuni 
nizungumzie baadhi ya dhana na mambo mapya yaliyomo katika Rasimu. Jambo
 la kwanza, kwa mfano, linahusu Ibara ya 128 (2)(d) inayoleta dhana ya 
"Mbunge kupoteza Ubunge iwapo atashindwa kufanya kazi za Mbunge kwa 
miezi sita mfululizo kutokana na maradhi au kizuizi ndani ya gereza".
Watu 
hawana tatizo na Mbunge kuwa kizuizini ndani ya gereza kama amepatikana 
na hatia Mahakamani na kuhukumiwa kifungo. Lakini, isijekuwa yuko 
rumande kwa tuhuma akisubiri kesi kusikilizwa. Je akija kuonekana hana 
hatia na kuachiliwa? Naungana na wale wanaoshauri kuwa jambo hili 
lifafanuliwe vizuri na kutambua Mbunge kutiwa hatiani na kupata adhabu 
ya kifungo cha kipindi hicho. Ni bora ifanyike hivyo sasa ili kuondoa 
mikanganyiko. Hakuna haja ya kusubiri mpaka jambo hili lije kufafanuliwa
 baadaye kwa Sheria itakayotungwa na Bunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Kwa 
upande wa mtu kupoteza Ubunge kwa sababu ya "kuugua kwa miezi sita 
mfululizo" ni maoni ya watu wengi kuwa huu ni ukatili ambao haustahili 
kufanywa na Katiba. Kuugua ndiyo ubinadamu na wakati mwingine Mbunge 
anaweza kupata ajali akiwatumikia wananchi wa Jimbo lake. Anaweza kuugua
 kwa miezi sita au zaidi na kupona kabla ya kipindi chake cha Ubunge 
kufika mwisho. Kwa nini awekewe ukomo wa miezi sita? Katiba ya mwaka 
1977 tunayotumia sasa haina sharti hilo. Watu wanauliza hoja na haja ya 
kuwa na sharti hili kwenye Katiba mpya ni ipi? Wanasema kwa kweli 
anachostahili Mbunge huyu kufanyiwa ni kuuguzwa afya yake iimarike ili 
aendelee kutumikia watu wake, na siyo kupoteza uongozi wake. Tusiwatie 
watu kishawishi cha kukatiza matibabu ili kukwepa sharti hilo. Ni vyema 
jambo hili mkalitazama kwa makini, na muone kama linastahili kuwepo au 
hapana.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Katika 
Rasimu hii imeingizwa dhana mpya ya kuweka ukomo wa vipindi vitatu kwa 
Wabunge. Tena mapendekezo haya hayasemi vipindi vitatu mfululizo au la!.
 Jambo hilo limezua mjadala motomoto katika jamii. Ni vizuri 
mkajiridhisha juu ya sababu za msingi na manufaa ya kufanya hivyo hapa 
Tanzania. Mazoea yetu na ya kwingineko duniani ni kuweka ukomo kwa Wakuu
 wa Nchi kwa sababu nzuri na rahisi kuzielezea. Lakini, kuwawekea ukomo 
Wabunge ni jambo jipya na huenda Tanzania tukawa wa kwanza. Nashawishika
 kuungana na wale wanaopendekeza kuwa pengine ni mapema mno kuanzisha 
utaratibu huo hapa kwetu.
Nachelea 
kuwa tutainyima nchi yetu fursa ya kupata watu wenye maarifa na uzoefu 
mzuri wa uongozi kwa nafasi ya Ubunge au kwa nafasi za uongozi wa Taifa 
bila ya sababu za msingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Jambo 
lingine jipya linalopendekezwa na Tume ni utaratibu wa kumuondoa Mbunge 
katikati ya kipindi chake cha uongozi. Kwa hoja linaonekana kuwa jambo 
jema lakini naomba athari zake mzitafakari vizuri. Kuna hatari ya 
kuanzisha misuguano kwenye Majimbo na kuwaacha Wabunge wasifanye kazi 
zao kwa utulivu bali wawe wanajihami dhidi ya wapinzani wao 
kuwatengenezea fitna za kuwatoa. Utaratibu unaopendekezwa wa Chama chake
 kujaza nafasi ya Mbunge inapokuwa wazi katika mazingira hayo nao 
unaweza kuwa ndicho kichocheo kikubwa cha vuguvugu la kumuondoa Mbunge. 
Walioshindwa kwenye kura ya maoni wanaweza kufanya kazi ya kuwachimba 
wenzao mpaka waondoke. Jipeni muda wa kupima faida na hasa thamani 
inayoongezwa na kuanzisha utaratibu huo. Naomba tujiridhishe kama jambo 
hili jipya lina tija. Hivi kupewa nafasi kila miaka mitano kurudi kwa 
wananchi hakutoshi kumuondoa Mbunge ambaye watu wamemchoka?
Muundo wa Muungano
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Jambo 
lingine kubwa lililopendekezwa na Tume ambalo limevuta hisia za karibu 
watu wote nchini linahusu muundo wa Muungano wetu kuwa wa Serikali tatu 
badala ya mbili za sasa. Pendekezo hili limezua mjadala mkubwa tangu 
lilipotolewa katika Rasimu ya kwanza na kurudiwa katika Rasimu ya pili. 
Wakati mwingine mjadala umekuwa mkali na wa hisia kali kwa kila upande.
Kwa kweli
 hili ndilo jambo kubwa kuliko yote katika Rasimu kwa sababu 
linapendekeza kuanzishwa kwa muundo na mfumo mpya wa kuendesha nchi 
yetu. Hii ndiyo agenda mama ya Bunge hili ambayo kila Mtanzania 
anasubiri kwa hamu uamuzi wenu utakuwa upi. Ombi langu kwenu ni kuwa 
watulivu mnapojadili suala hili. Epukeni jazba ili mfanye uamuzi ulio 
sahihi. Lazima mtambue uamuzi usiokuwa sahihi kwa jambo hili una hasara 
kubwa. Tunaweza kupoteza kitu tulichokijenga kwa gharama kubwa kwa nusu 
karne iliyopita. Tanzania inaweza kuwa nchi iliyojaa migogoro na 
matatizo mengi ambayo hatunayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wajumbe;
Kama 
alivyoeleza Mwenyekiti wa Tume Mheshimiwa Jaji Joseph Sinde Warioba, 
mara kadhaa, mjadala au madai ya kutaka muundo wa Serikali tatu si jambo
 jipya. Ulikuwepo hata wakati wa mazungumzo ya kuunganisha nchi zetu 
mbili mwaka 1964. Ulikuwa kiini cha kuchafuka kwa hali ya hewa ya 
kisiasa Zanzibar mwaka 1984. Muundo huu uliwahi kupendekezwa na Tume ya 
Nyalali mwaka 1992, ndiyo hoja ya G55 mwaka 1993 na umependekezwa pia na
 Tume ya Jaji Kisanga ya mwaka 1998. Lakini mara zote hizo mapendekezo 
hayo hayakukubaliwa.
Waasisi 
wa taifa letu, yaani Mwalimu Julius Nyerere, aliyekuwa Rais wa Jamhuri 
ya Tanganyika wakati ule na Sheikh Abeid Amani Karume, aliyekuwa Rais wa
 Jamhuri ya Watu wa Zanzibar wakati ule, waliamua kuchagua Muungano wa 
Serikali mbili tulionao sasa. Walitoa sababu mbili kuu: "ni muundo 
unaoihakikishia Zanzibar kuwa haimezwi na Tanganyika; na pia unaiepusha 
Tanganyika kubeba mzigo mkubwa wa kugharamia Serikali ya Tanganyika na 
ile ya Muungano".
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Natambua 
kuwepo kwa rai ya kutaka Mwalimu Nyerere asitumiwe katika mjadala huu. 
Nionavyo mimi ni vigumu kuacha kujadili fikra za Mwalimu Nyerere na 
Sheikh Karume katika jambo hili. Wao ndiyo wa mwanzo kujadili na 
kukubaliana kuwa mfumo wa Serikali mbili ndiyo bora kwa nchi yetu. Iweje
 leo tunapozungumzia kuubadili, mawazo yao yawe hayafai kutumika au hata
 kuzungumzwa. Hivi hasa mawazo ya nani pekee ndiyo bora zaidi kutumika? 
Tutakuwa hatuutendei haki mjadala huu na sisi wenyewe tunaoshiriki 
katika mchakato huu. Rai yangu kwenu ni kuwa mzitazame hoja zote kwa 
marefu na mapana yake ili mpime kama zipo sababu za kuubadili muundo wa 
sasa wa Muungano wa Serikali mbili na kuleta wa Serikali tatu. Na, kama 
zipo mabadiliko hayo yaweje! Lazima mfanye uamuzi kwa utambuzi na hoja 
zenye mashiko. (you must make an informed decision).
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Tume 
imetoa sababu mbili kubwa za kupendekeza muundo wa Serikali tatu. Sababu
 ya kwanza ni kwamba ndiyo matakwa ya Watanzania wengi kote Zanzibar na 
Tanzania Bara. Inaeleza kuwa idadi kubwa ya Watanzania waliotoa maoni, 
yaani asilimia 60.2 wa kutoka Zanzibar wanaunga mkono muundo wa Serikali
 ya Mkataba, na asilimia 61.3 wa kutoka Tanzania Bara wanaunga mkono 
muundo wa Serikali tatu. Sababu ya pili ni kwamba muundo huo unatoa 
majawabu ya uhakika na endelevu kwa changamoto za muundo wa sasa wa 
Serikali mbili zinazonung'unikiwa na watu wa pande zetu mbili za 
Muungano.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Sababu 
hizi mbili kuu zilizotolewa na Tume zimezua mjadala mkali katika jamii. 
Wapo wanaokubaliana na Tume na wapo wasiokubaliana nayo. Wapo wanaosema 
Tume imesema kweli kwamba Watanzania wengi wanaunga mkono muundo wa 
Serikali tatu, hivyo muundo wa Serikali tatu hauepukiki. Ndiyo matakwa 
ya wengi hivyo msemo wa Kiswahili usemao wengi wape uheshimiwe.
Lakini 
wapo wanaodai kuwa takwimu za Tume hazionyeshi ukweli huo. Wanasema kuwa
 taarifa ya Tume imeonesha kuwa Watanzania waliotoa maoni yao kwa Tume 
kwa mdomo na maandishi walikuwa 351,664. Kati yao ni wananchi 47,820 au 
sawa na asilimia 13.6 ndiyo waliokerwa na muundo wa Muungano hivyo 
wakauzungumzia. Wananchi 303,844 au sawa na asilimia 86.4 muundo wa 
Muungano kwao halikuwa tatizo, ndiyo maana hawakuuzungumzia kabisa. 
Wanahoji kuwa iweje leo asilimia 13.6 ya Watanzania wote waliotoa maoni 
wageuke kuwa ndiyo Watanzania walio wengi!
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Wanasema 
pia, kwamba mbona Taarifa ya Tume yenyewe, kuhusu takwimu (uk. 66 na 
67), inaonesha kwamba kati ya hao watu 47,820 waliotoa maoni kuhusu 
Muungano, ni watu 17,280 tu ambao ni sawa na asilimia 37.2 ndiyo 
waliotaka muundo wa Serikali tatu, asilimia 29.8 walitaka Serikali 
mbili, asilimia 25.3 walipendekeza Serikali ya Mkataba na asilimia 7.7 
walipendekeza Serikali moja. Hii hoja ya Watanzania wengi kutaka 
Serikali tatu msingi wake upi?
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Takwimu 
za Tume (uk. 57) zinaonyesha, vilevile kuwa Tume ilipokea maoni 772,211.
 Kati ya hayo asilimia 10.4 tu ndiyo yaliyozungumzia muundo wa Muungano 
na asilimia 88.6 hayakuzungumzia Muungano bali mambo mengine. Hivyo basi
 wanahoji pia kwamba kama muundo wa Muungano ungekuwa ni jambo 
linalowakera Watanzania wengi, lingedhihirika kwenye idadi ya watu 
waliotoa maoni na kwenye idadi ya maoni yaliyotolewa. Yote hayo 
hayakujitokeza. Waliouzungumzia Muungano walikuwa asilimia 13.6 tu ya 
watu wote waliotoa maoni na maoni yanayohusu Muungano yalikuwa asilimia 
10.4 ya maoni yote. Hivyo basi, wanauliza "usahihi wa hoja ya Watanzania
 wengi kutaka Serikali tatu uko wapi?"
Changamoto za Muundo wa Serikali Mbili
Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wajumbe;
Kama 
nilivyokwishagusia awali, sababu ya pili ambayo Tume inatoa kuhusu kufaa
 kwa muundo wa Serikali tatu ni kwamba mfumo huu unajibu changamoto 
nyingi za muundo wa Serikali mbili. Tume imeainisha vizuri changamoto za
 muundo wa Serikali mbili. Kwa upande wa Zanzibar wanalalamikia kile 
kinachoitwa Tanzania Bara kuvaa koti la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania 
na hivyo kutumia mamlaka ya Serikali ya Muungano kujinufaisha yenyewe. 
Fursa hiyo Zanzibar hainayo. Aidha, wanasema mipaka na mamlaka ya 
Serikali ya Muungano kwa mambo ya Muungano, na kwa mambo ya Tanzania 
Bara haijaainishwa vizuri ikaeleweka. Wazanzibari pia, wanazungumzia 
mkanganyiko kuhusu ugawanaji wa mapato, na jinsi ya kuchangia shughuli 
za Muungano baina ya Serikali ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya 
Zanzibar. Vilevile, wanalalamikia Rais wa Zanzibar kuondolewa kuwa 
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano.
Aidha, 
kuna malalamiko kuwa orodha ya mambo ya Muungano iliyoongezwa kutoka 
mambo 11 mwaka 1964 mpaka 22 mwaka 1992 imepunguza uhuru wa Zanzibar kwa
 mambo yake ya ndani.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Kwa 
upande wa Tanzania Bara, Tume inaeleza kuwepo kwa manung'uniko kuwa 
Muungano wa Serikali mbili umepoteza utambulisho wa kihistoria wa 
Tanganyika na fursa ya watu wa upande wa Tanzania Bara kutetea maslahi 
yao ndani ya Muungano. Wanasema Zanzibar sasa imekuwa nchi huru; ina 
bendera yake, wimbo wake wa taifa na Serikali yake. Aidha, wanasema 
Zanzibar imebadili Katiba na kujitambulisha kama nchi na kuchukua 
madaraka ya Bunge la Muungano, kwa vile Sheria zinazotungwa na Bunge 
lazima zipelekwe kwenye Baraza la Wawakilishi kupata kibali cha kutumika
 Zanzibar. Wananchi wa Tanzania Bara pia wanalalamikia kutokuwa na haki 
ya kumiliki ardhi Zanzibar wakati wenzao wa kutoka Zanzibar wanayo haki 
hiyo Tanzania Bara. Na wao vilevile wananung'unikia mkanganyiko kuhusu 
ugawaji wa mapato na jinsi ya kuchangia gharama za uendeshaji wa 
shughuli za Muungano baina ya Serikali ya Muungano na Serikali ya 
Zanzibar. Hizi ndizo baadhi ya changamoto ambazo Tume inaona jawabu lake
 ili kuzitanzua ni kubadili muundo wa Muungano kuwa wa Serikali tatu 
badala ya mbili za sasa.
Faida za Muundo wa Serikali Tatu
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Tume ya 
Mabadiliko ya Katiba imefafanua kwamba mfumo wa Serikali tatu utagawanya
 vizuri madaraka kati ya mamlaka tatu za Muungano. Unawezesha Washirika 
wa Muungano kubaki na utambulisho wao wa kihistoria na kiutamaduni na 
hivyo, utawezesha kuondoa hisia za Zanzibar kumezwa na Muungano. Pia 
unawezesha kila upande wa Tanzania kuendesha mambo yake yasiyo ya 
Muungano kadri wanavyoona inafaa. Vile vile unaweza ukaleta ushindani wa
 kimaendeleo baina ya washirika na hivyo kusaidia kukuza maendeleo ya 
nchi.
Faida za Muundo wa Serikali Mbili
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Pamoja na
 kuainisha changamoto za muundo wa Serikali mbili na kupendekeza kuwa 
muundo wa Serikali tatu ndio utakaosaidia kuzitatua, Tume haikuacha 
kutambua manufaa na mchango muhimu uliotolewa na muundo wa Serikali 
mbili kwa nchi yetu. Tume inasema kuwa muundo wa Serikali mbili 
unapunguza gharama za uendeshaji wa shughuli za umma. Umesaidia kujenga 
uhusiano na ushirikiano mzuri katika nyanja mbalimbali baina ya wananchi
 wa pande zetu mbili za Muungano. Umezuia mkubwa kummeza mdogo; na 
umedumisha Muungano mpaka kuufikisha hapa ulipo tangu kuasisiwa kwake 
takriban miaka 50 iliyopita (1964). Aidha, umesaidia kudumisha amani, 
umoja na utulivu hapa nchini.
Changamoto za Muundo wa Serikali Tatu
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Pamoja na
 kuelezea ubora wa muundo wa Serikali tatu kama jawabu kwa changamoto za
 Serikali mbili, Tume inakiri kuwa hata muundo huu nao una changamoto 
zake. Kwanza kabisa, Taarifa ya Tume inaeleza kuwa kutakuwa na gharama 
kubwa za uendeshaji wa shughuli za umma. Mheshimiwa Jaji Joseph Warioba 
alitutoa hofu kuhusu gharama ingawaje mwaka 1993, Mwalimu alikuwa na 
mawazo tofauti. Alisema kwamba: "watu ...wanaodhani kuwa gharama ya 
Serikali yo yote kati ya hizo ingekuwa ndogo, (Waulizeni Wazanzibari) na
 wala gharama ya Serikali ya Shirikisho isingekuwa ndogo hata bila 
gharama ya mambo yasiyo ya Shirikisho". Ni matumaini yangu kwamba katika
 mjadala wenu mtajipa nafasi ya kulitafakari suala hili kubwa na nyeti.
Tume 
imesema pia kwamba, Muundo huu, unaweza kuibua tatizo la uchangiaji wa 
gharama za uendeshaji wa shughuli za umma baina ya nchi washirika. 
Vilevile, kuna uwezekano wa kuwepo sera zinazokinzana au kutofautiana 
juu ya masuala ya msingi ya nchi na kuzua mgogoro kati ya washirika wa 
Muungano na baina ya nchi washirika na Serikali ya Muungano. Aidha, upo 
uwezekano mkubwa kwa muundo huu kuleta tofauti za kimaendeleo baina ya 
pande mbili za Muungano kutokana na kila upande kuwa na sera na mipango 
tofauti.
Tume pia 
imeelezea hatari ya muundo wa Serikali tatu kukuza hisia za utaifa 
(nationalistic feelings) kwa nchi washirika, hivyo kuweza kudhoofisha 
Muungano. Muundo huu pia unaweza kuleta misuguano (paralysis and 
deadklocs in decision making) katika kufanya uamuzi juu ya masuala 
muhimu ya kitaifa. Changamoto hizo si tu zinaweza kuwa tishio kwa ustawi
 wa Muungano bali pia hata uhai wake. Kwa ajili hiyo kuchagua muundo wa 
Serikali tatu kuna maana ya kufanya kazi ya ziada ya kuzikabili 
changamoto hizi ili zisiue Muungano wenyewe. Changamoto ambazo si ndogo 
hata kidogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Wanaounga
 mkono muundo wa Serikali mbili wanasema kuwa kwa mlolongo huu wa 
changamoto zilizoainishwa na Tume yenyewe, unadhihirisha kuwa muundo wa 
Serikali tatu hautapunguza matatizo ya Muungano wetu bali utayaongeza 
maradufu kuliko ilivyo sasa. Wanakiri kuwepo kwa changamoto katika 
muundo wa sasa wa Muungano. Hata hivyo, wanaamini zinaweza kushugulikiwa
 na kupatiwa ufumbuzi bila ya kuhitaji kuwa na Serikali ya tatu. Wanatoa
 mifano kadhaa ya jinsi Serikali zetu zilivyoshughulikia changamoto za 
Muungano katika kipindi cha uhai wake na mafanikio yaliyopatikana.
Katika 
kushughulikia kero za Muungano, Serikali zetu mbili ziliunda Tume ya 
Shelukindo mwaka 1992 na Kamati ya Pamoja ya Serikali zetu mbili mwaka 
1993. Mambo mengi yaliyoainishwa katika Tume ya Shelukindo na Kamati ya 
Pamoja yameshughulikiwa na kupatiwa ufumbuzi. Kwa upande wa kero 
zilizoelezwa kwenye Tume ya Shelukindo, ilipofikia mwaka 2006 yalikuwa 
yamebakia mambo 13 kati ya 31. Kwa jumla, kwa kero zilizoibuliwa na Tume
 ya Shelukindo na Kamati ya Pamoja, hivi sasa yamesalia mambo sita tu. 
Kimsingi ni mambo yahusuyo maslahi ya kiuchumi na yote yapo katika hatua
 nzuri za kuyamaliza. Mambo hayo ni:
Mgawanyo wa mapato:
Hisa za SMZ zilizokuwa katika Bodi ya Sarafu ya Afrika Mashariki
Mgawanyo wa Mapato yatokanayo na faida ya Benki Kuu.
Utafutaji na uchimbaji mafuta na gesi asili.
Ushirikiano wa Zanzibar na taasisi za nje.
Ajira kwa watumishi wa Zanzibar katika taasisi za Muungano.
Usajili wa vyombo vya moto.
Tume ya Pamoja ya Fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Serikali 
zetu mbili zimeamua kwa dhati kutumia fursa ya mchakato huu wa 
mabadiliko ya Katiba kuyamaliza yale yanayohitaji kuingizwa kwenye 
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mambo hayo ni matatu 
yafuatayo:
Utafutaji na uchimbaji mafuta na gesi asili.
Ushirikiano wa Zanzibar na taasisi za nje.
Tume ya Pamoja ya Fedha.
Matatu 
mengine yatamalizwa kwa kutumia taratibu za kiutawala. Hali kadhalika, 
katika kipindi cha mpito kinachopendekezwa na Tume yaani 2015 – 2018 ni 
nafasi nzuri ya kushughulikia masuala yenye migongano kati ya Katiba ya 
Zanzibar na ile ya Jamhuri ya Muungano. Mimi naishi kwa matumaini na kwa
 vile tunayo dhamira njema ya kuimarisha Muungano wetu, naamini tutaweza
 kuziondoa tofauti zilizopo.
Orodha ya Mambo ya Muungano
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Kuhusu 
orodha ya mambo ya Muungano kuwa 22 badala ya 11 ya awali, napenda 
kuwahakikishia kuwa Serikali ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya 
Zanzibar hazina kigugumizi wala upungufu wa dhamira ya kisiasa ya 
kuyapunguza yale yanayopunguzika. Napenda kwanza kabisa, ieleweke kuwa 
kilichoongeza orodha hiyo si hila za Serikali ya Muungano kutaka 
kupunguza madaraka ya Zanzibar kwa mambo yake ya ndani. Na, wala siyo 
udhaifu wa viongozi wa Zanzibar katika kutetea maslahi ya nchi yao. La 
hasha.
Pili, 
naomba ieleweke kuwa, kila kilichoongezwa katika Orodha ya Mambo ya 
Muungano kilikuwa na sababu inayoeleweka, inayoelezeka na iliyokubalika 
na pande zote mbili za Muungano. Hakuna hata jambo moja lililoingizwa 
kwenye Katiba kwa kificho. Taratibu stahiki za kikatiba na kisheria 
zilifuatwa. Hoja ziliwasilishwa Bungeni na kujadiliwa kwa uwazi na 
uamuzi ulifanywa na Bunge kwa kuzingatia kanuni ya theluthi mbili ya 
kura za kila upande wa Muungano. Kumbukumbu zipo katika Hansard za Bunge
 la Muungano, ambazo ziko wazi kwa kila mtu anayetaka kuzisoma asome. 
Nashauri mkazisome ili mpate kujua ukweli na undani wa kila 
kilichoongezwa na sababu za kufanya hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Nchi zetu
 mbili zilipoungana mwaka 1964 na kuzaa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
 kulikuwa na mambo 11 kwenye Orodha ya Mambo ya Muungano. Mambo hayo ni 
haya yafuatayo:
Katiba ya Jamhuri ya Muungano,
Mambo ya Nje,
Ulinzi,
Polisi,
Hali ya Hatari,
Uraia,
Uhamiaji,
Biashara ya nje na mikopo,
Utumishi katika Serikali ya Muungano,
Kodi ya Mapato, Kodi ya Makampuni, Ushuru wa Forodha na Ushuru wa Bidhaa,
Bandari, Mambo ya Anga, Posta na Simu.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Kati ya 
mwaka 1965 na 1992 mambo ya Muungano yaliongezeka kutoka 11 hadi kufikia
 22, kimsingi kutokana na mambo mbalimbali yaliyotokea nchini na kwenye 
ukanda wetu wa Afrika Mashariki. Pande zetu mbili za Muungano 
zilikubaliana kuwa mambo hayo yaongezwe katika Katiba na taratibu za 
kisheria na Kikatiba zilifuatwa. Kwa idhini yako naomba nitoe maelezo 
kwa ufupi kwa yale yaliyoongezwa na kitu kilichosababisha mabadiliko 
hayo kufanywa.
Jambo la 
kwanza kuongezwa, yaani la 12 lilikuwa ni "sarafu, mabenki na fedha za 
kigeni". Hii ilifanyika tarehe 10 Juni, 1965 kufuatia kuvunjika kwa Bodi
 ya Sarafu ya Afrika Mashariki (East African Currency Board) mwaka 1964.
 Kwa ajili hiyo, kila nchi mwanachama wa Jumuiya ililazimika kuwa na 
sarafu yake na mipango yake ya kusimamia mambo yake ya kibenki na fedha.
 Serikali zetu mbili zilikubaliana masuala hayo yashughulikiwe na 
Serikali ya Muungano na Muswada husika wa Bunge uliidhinishwa kuwa 
Sheria na Mzee Abeid Amani Karume aliyekuwa akikaimu Urais tarehe 10 
Juni, 1965.
Tarehe 11 Agosti, 1967 yaliongezwa mambo yafuatayo kwenye Orodha ya Mambo ya Muungano:-
Leseni za Viwanda na Takwimu, (Jambo la 13)
Elimu ya Juu, (Jambo la 14)
Jambo la 
15 lilikuwa ni mambo yote yaliyokuwa kwenye Nyongeza ya 10 ya Mkataba wa
 Jumuiya ya Afrika Mashariki. Nyongeza hiyo ilikuwa na mambo 27 ambayo 
Serikali ya Muungano ilipewa jukumu la uratibu. Mambo hayo ni pamoja na 
Mahakama ya Rufani ya Afrika Mashariki, Utabiri wa Hali ya Hewa, 
Utafiti, Vipimo na Mizani, Huduma ya Usafiri wa Reli, Barabara, Usafiri 
wa Majini na kadhalika.
Tarehe 22
 Julai, 1968 "rasilimali ya mafuta, petroli na gesi asilia" iliongezwa 
kwenye Orodha ya Mambo ya Muungano na kuwa jambo la 16. Kimsingi 
Serikali ya Muungano ilipewa jukumu la kuagiza mafuta ya petroli na gesi
 asilia kwa ajili ya nchi nzima. Baada ya kupanga upya Orodha ya Mambo 
ya Muungano, suala la rasilimali ya mafuta likawa la 15.
Tarehe 22
 Novemba, 1973 Baraza la Mitihani la Taifa liliongezwa na kuwa jambo la 
16. Hii ilifuatia kuvunjika kwa Baraza la Mitihani la Afrika Mashariki 
mwaka 1971 na hivyo nchi yetu kulazimika kuunda Baraza la Mitihani la 
Taifa mwaka 1973.
Mwaka 
1984 yalipofanyika mabadiliko makubwa katika Katiba ya mwaka 1977, 
Orodha ya Mambo ya Muungano ilipangwa upya. Mambo yaliyokuwemo kwenye 
Nyongeza ya 10 ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na kuorodheshwa kama Jambo
 la 15 katika Orodha ya Mambo ya Muungano yalipunguzwa na kubaki matano.
 Mambo hayo yalipewa namba kama ifatavyo:- Usafirishaji wa Anga kuwa 
Jambo la 17, Utafiti kuwa la 18, Utabiri wa Hali ya Hewa kuwa la 19 na 
Takwimu kuwa la 20 na Mahakama ya Rufani ya Tanzania ikawa jambo la 21.
Tarehe 17
 Mei, 1992 likaongezwa jambo la "Uandikishaji wa Vyama vya Siasa" na 
kuwa jambo la 22. Hii ilifuatia kuanzishwa kwa Mfumo wa Vyama Vingi vya 
Siasa na hasa uamuzi kuwa vyama vitakuwa vya kitaifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Bila ya 
shaka maelezo haya yatasaidia kuelezea nini kimeongezwa na mazingira ya 
kuongezwa kwake ni yepi. Kulikuwepo na sababu za msingi na wala siyo 
hila ya namna yo yote ile iliyofanywa na mtu ye yote mwenye nia mbaya na
 Zanzibar. Kama tulivyoona mambo mengi yalihusu kilichokuwa kinatokea 
ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Kila yalipotokea mabadiliko katika
 uendeshaji wa shughuli za Jumuiya ya Afrika Mashariki, huduma 
zilizokuwa zikitolewa na Jumuiya zilikabidhiwa Serikali ya Muungano 
kubeba kwa sababu ya uwezo wake mkubwa wa kiuchumi. Yale yaliyokuwa 
yanagusa sehemu zetu mbili za Muungano yaliingizwa katika Orodha ya 
Mambo ya Muungano. Mengineyo yaliachiwa kila upande kushughulikia 
ilivyoona inafaa. Kwa maana hii basi, mambo ambayo yalitokana na uamuzi 
wetu wenyewe ni mawili tu. Mambo hayo ni rasimali ya mafuta na gesi 
asilia (1968), na uandikishaji wa vyama vya siasa (1992).
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Ni 
msimamo wa Serikali zetu mbili, tangu mwanzo mpaka leo kwamba, iwapo 
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeshajenga uwezo wake wa kufanya 
baadhi ya mambo katika Orodha ya Mambo ya Muungano ipewe uhuru wa 
kufanya hivyo. Lililo muhimu ni kuwa zisiondolewe tunu zenyewe za 
Muungano wetu. Ndiyo maana, mambo kama vile bandari, takwimu, kodi ya 
mapato, leseni za biashara, utafiti na mengineyo, yanasimamiwa na 
kuendeshwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na kuwemo kwenye 
Orodha ya Mambo ya Muungano. Imekuwa hivyo kwa miaka kadhaa sasa na 
imethibitika kuwa Zanzibar inayamudu. Ni makusudio yetu kutumia fursa ya
 mchakato huu sasa kuyaondoa rasmi mambo hayo na mengineyo 
tutakayokubaliana kutoka kwenye Orodha ya Mambo ya Muungano.
Rasilimali ya Mafuta na Gesi Asilia
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Kwa ajili
 hiyo tumekubaliana kuliondoa suala la rasilimali ya mafuta na gesi 
asilia lisiwe jambo la Muungano. Jambo hili tulishakubaliana tangu 
wakati wa Rais Amani Abeid Karume tuliondoe na hata alipokuja Rais Shein
 msimamo haukubadilika. Kilichotuchelewesha kutekeleza ni kuibuka kwa 
fikra za kuwa na mchakato huu wa Katiba mpya. Tuliona kuwasilisha 
Bungeni Muswada wa Sheria wa kuondoa jambo hili katikati ya mchakato 
huu, ingeweza kuzua matatizo yasiyokuwa ya lazima. Tungeulizwa haraka ni
 ya nini tungeweza kukosa majibu.
Hatimaye 
wakati wake wa kulimaliza suala hili sasa umefika. Misemo ya wahenga ya 
"subira yavuta heri" na "kawia ufike" imetuongoza vyema tumefika mahali 
tunaweza kufanya hivyo. Zipo sababu mbili zilizotushawishi kuamua kuitoa
 rasilimali hii kwenye Orodha ya Mambo ya Muungano. Kwanza kwamba, siku 
hizi Serikali haiagizi mafuta. Kazi hiyo hufanywa na makampuni binafsi. 
Pili, kwamba, rasilimali ya mafuta na gesi yakipatikana Zanzibar ni 
suala la kiuchumi ambalo lipo kwenye mamlaka ya Zanzibar kama ilivyo 
karafuu, hiliki, mwani na kadhalika. Au kama ilivyo dhahabu, gesi, 
pamba, kahawa na kadhalika kwa upande wa Tanzania Bara. Hivyo, Zanzibar 
iachwe kumiliki rasilimali yake ya kiuchumi.
Zanzibar na Ushirikiano wa Kimataifa
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Jambo 
lingine muhimu ambalo Serikali zetu mbili zimelizungumza na kukubaliana 
tulitafutie ufumbuzi ni kuhusu Zanzibar kupata fursa ya kujiunga na 
mashirika ya kimataifa, kukopa na kupata misaada kutoka nchi za nje bila
 kizuizi. Kwa sasa fursa hiyo ina vikwazo vya namna mbalimbali. Ni 
ukweli usiopingika kuwa jambo hili limechangia kwa kiasi kikubwa kujenga
 hisia hasi kuhusu Muungano kwa upande wa Zanzibar. Aidha, limechangia 
sana kuchafua hali ya hewa ya kisiasa Zanzibar kwa nyakati mbalimbali. 
Hata zile kauli kwamba Tanzania Bara imejificha kwenye koti la Serikali 
ya Muungano, na kutaka itoke ionekane ili iache kunufaika isivyostahili,
 zinazochangiwa sana na mazingira haya iliyonayo Zanzibar. Serikali zetu
 mbili zinaamini kuwa mambo haya yakipatiwa ufumbuzi tutakuwa tumeondoa 
kizingiti kikubwa katika ustawi wa Muungano wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Serikali 
ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar 
tumekubaliana kuwa, tutumie fursa za mchakato huu kuyamaliza mambo haya 
yaishe! Bahati nzuri dhana iliyopo katika Ibara ya 65(2) ya Rasimu 
inatoa jawabu mwafaka kwa tatizo hili. Tukikubaliana, itaipa Zanzibar 
"uwezo na uhuru wa kuanzisha uhusiano na ushirikiano na jumuiya au 
taasisi yo yote ya kikanda na kimataifa kwa mambo yaliyo chini ya 
mamlaka yake kwa mujibu wa Katiba ya nchi" bila kizuizi. Ni maoni ya 
Serikali zetu mbili kuwa fursa hiyo inaweza kutolewa kwa Zanzibar bila 
ya kulazimika kuwa na muundo wa Serikali tatu. Hatuuoni ulazima huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Kwa maoni
 yangu kitu kingine muhimu cha kufanya ni kuongeza msukumo, 
utakaohakikisha kuwa Tume ya Pamoja ya Fedha inatimiza ipasavyo majukumu
 yake. Wanaohusika na utekelezaji wa maamuzi yake wabanwe ipasavyo 
kutimiza wajibu wao. Iwekwe mifumo na masharti katika sheria au Katiba 
ya kuwabana watekelezaji kwa ajili hiyo. Hali kadhalika ihakikishwe 
kuwa, Akaunti ya Pamoja inaanzishwa bila ajizi na kutumika na pande 
zote. Aidha, mfumo wa mawasiliano na ushirikiano baina ya Serikali zetu 
mbili yaani Kamati ya Pamoja ya Serikali ya Muungano na Serikali ya 
Mapinduzi Zanzibar, upewe nguvu ya kisheria na kama hapana budi upewe 
nguvu ya Kikatiba. Tukifanya hivyo tutafanikiwa kuyaweka mambo yote sawa
 hata bila ya kuhitaji kuunda Serikali ya tatu.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Waheshimiwa Wajumbe;
Katika 
mjadala kuhusu mapendekezo ya kuwa na muundo wa Muungano wenye Serikali 
tatu, wananchi wametoa maoni na mapendekezo mengi mazuri kuhusu 
changamoto za Serikali tatu zilizoainishwa na Tume na namna ya 
kuzitatua. Tena yapo maoni ya watu wanaopenda muundo wa Serikali tatu na
 wasiopenda muundo wa Serikali tatu. Nawaomba myatafakari kwa uzito 
unaostahili. Yapo mambo muhimu ya kuyatafutia ufumbuzi. Kwanza, kwa 
mfano ni ile hoja kwamba Serikali ya Muungano inayopendekezwa 
haikujengeka kwenye msingi imara. Haina nguvu yake yenyewe za kusimama. 
Inategemea mno ihsani ya nchi washirika. Kwa sababu hiyo inaweza 
kuanguka wakati wowote, na Muungano kusambaratika, iwapo itakosa ihsani 
ya nchi washirika. Tena inaweza kuwa hivyo hata kama ni mmoja wa 
washirika amefanya hivyo.
Pili, 
kwamba, haielekei Serikali hiyo ina chanzo cha uhakika cha mapato ya 
kuiwezesha kusimama yenyewe na kutekeleza majukumu yake. Ushuru wa 
bidhaa unaopendekezwa unatiliwa shaka kuwa hautatosheleza mahitaji. Pia,
 kwamba, hakuna uhakika wa fedha hizo kupatikana kwa vile, Serikali ya 
Muungano haina chombo chake chenyewe cha kukusanya mapato hayo. 
Itategemea vyombo vya nchi washirika kuikusanyia na kuipelekea. Kuna 
hatari ya shughuli za Serikali ya Muungano kusimama wakati wo wote au 
hata kusimama kabisa kwa sababu ya nchi washirika kuchelewa au kushindwa
 kuwasilisha makusanyo ya kutoka kwao.
Bahati 
mbaya Serikali ya Muungano haina uwezo wala nyenzo za kuhakikisha kuwa 
mapato yake yanawasilishwa. Serikali hiyo haina mamlaka ya kuzibana nchi
 washirika kuwasilisha au kuziwajibisha zisipofanya hivyo. Katika 
mazingira hayo ni rahisi kwa Serikali ya Muungano kukwama na kushindwa 
kutekeleza majukumu yake. Huu ni muundo ambao inakuwa ni rahisi sana kwa
 Muungano kuvunjika.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Katika 
Rasimu ya Katiba, Serikali ya Muungano inapewa fursa ya kukopa kama 
chanzo cha kujipatia mapato ya kuendesha shughuli zake. Lakini, kwa 
sababu ya kukosa rasilimali zake yenyewe, huenda ikawa vigumu kwa 
Serikali hiyo kukopesheka. Kwa jumla hii ni Serikali ambayo ukuu wake 
hauna nguvu iliyo thabiti, na watu wengine wanaona kama vile ukuu huo 
haupo kabisa. Akitokea kiongozi ye yote wa nchi washirika akatunisha 
misuli dhidi ya Rais wa Muungano au kupinga maamuzi ya Serikali au 
chombo cha Muungano, Rais na Serikali yake watakuwa hawana lo lote la 
kufanya. Kwa kweli uhai wa Muungano katika muundo wa Serikali tatu ni wa
 mashaka makubwa.
Hofu hizi
 kuhusu udhaifu wa Serikali ya Muungano chini ya mfumo wa Serikali tatu 
unaopendekezwa, zinawasumbua hata wale wanaopendelea mfumo wa Serikali 
tatu kuwepo. Wao wangependa iwepo Serikali ya Muungano yenye nguvu na 
inayoweza kusimama yenyewe kwa kujitegemea. Wanaona kilichopendekezwa 
hakitoi matumaini hayo. Hii ina maana kuwa lazima mawazo bora zaidi 
yatolewe ili kupata Serikali ya tatu yenye ukuu unaoonekana na inayoweza
 kusimama yenyewe bila kuwa tegemezi na egemezi kwa nchi washirika. Pia 
inaweza kuwa nguzo ya kutegemewa na nchi washirika. Bila ya shaka Bunge 
hili likiamua tufuate mfumo huo linaweza kuonyesha njia ya kuondoa hofu 
hizo. Kwa waumini wa Serikali mbili wanaona kuwa huu ni uthibitisho wa 
ubora wa muundo wa Serikali mbili.
Changamoto za Hisia za Utaifa
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Katika 
kuainisha changamoto za muundo wa Serikali tatu, Tume ya Mabadiliko ya 
Katiba imeyataja mambo mengine mawili makubwa ambayo ningependa 
Waheshimiwa Wajumbe muyape tafakuri stahiki. Mambo hayo ni mosi, 
misuguano na mikwamo (deadlocks and paralysis) katika kujadili na 
kufanya uamuzi kuhusu mambo muhimu ya Muungano. Na pili, ni kuibuka kwa 
hisia za utaifa (nationalistic sentiments) wa zamani kwa nchi washirika.
 Nawaomba myatafakari kwa makini sana mambo haya, kwa sababu ya uwezo 
wake mkubwa wa kuhatarisha siyo tu ustawi na uhai wa Muungano, bali hata
 usalama wa raia na mali zao. Naona hata Tume haikuweza kupata ufumbuzi 
ulio mwafaka kabisa kwa changamoto hizi. Bila ya shaka katika mijadala 
yenu Waheshimiwa Wajumbe mnaweza kusaidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Ni lazima
 lifanyike kila linalowezekana kuhakikisha kuwa maamuzi hayakwami kwani 
yakikwama maana yake shughuli za Muungano zitakuwa zimekwama. Kama 
hazitakwamuliwa kwa wakati ustawi wa Muungano utaathirika. Ikishindikana
 kabisa kupatikana ufumbuzi Muungano unaweza kuvunjika. Kuibuka na kukua
 kwa hisia za utaifa (nationalistic feelings) kwa nchi washirika, yaani 
Utanganyika na Uzanzibari ni tishio kubwa sana kwa uhai wa Muungano. 
Hebu fikiria, watu walioishi pamoja kidugu na kwa kushirikiana, kama 
watu wamoja na raia wa nchi moja yaani Watanzania kwa miaka 50, kuja 
kujikuta uhusiano wao kuwa ni kati ya Watanganyika na Wazanzibari na 
siyo kati ya Watanznaia. Kwa mujibu wa sensa iliyopita takriban asilimia
 90 ya Watanzania waliopo sasa wamezaliwa baada ya mwaka 1964. Nchi 
wanayoijua ni Tanzania. Litakuwa ni jambo lenye mshtuko mkubwa na athari
 zisizoweza kutabirika, watu hao watakapojikuta ni wageni wanaotakiwa 
kutengenezewa utaratibu maalum wa kusafiri na kuishi wakiwa upande wa 
Muungano ambao siyo kwao kwa asili. Wanakuwa wageni na fursa walizokuwa 
wanazipata waendapo popote haiwi rahisi tena kuzipata.
Katika 
mazingira hayo ni rahisi sana chuki kupandikizwa na watu waliokuwa ndugu
 mara moja watajikuta maadui. Aidha, watu wanaweza kujikuta wakilazimika
 kurudi kwao kwa asili ama kwa kufukuzwa au kwa sababu ya mazingira kuwa
 magumu kiasi cha kuona bora waondoke. Watu hao wanaweza kulazimika 
kuondoka huku wakiacha nyuma kila kitu walichokichuma maishani.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Changamoto
 hizi kubwa mbili za mfumo wa Serikali tatu ambazo Tume imeziona, ni za 
kweli. Si mambo ya kufikirika. Yale yaliyowakuta watu wenye asili ya 
Tanzania Bara ya kuchomewa moto biashara zao Zanzibar mwaka 2012 na watu
 wenye hisia kali za Uzanzibari, na kuwataka watu wa Bara waondoke 
Zanzibar, huenda yakawa madogo. Matukio ya namna hii yanaweza kutokea 
pande zote mbili na kusababisha maafa makubwa. Itaanza baina ya watu, 
baadaye itakuwa baina ya Serikali zetu mbili na kuzifikisha nchi zetu 
mbili zilizokuwa ndugu na rafiki, kwa nusu karne, ghafla kuwa maadui 
wasioombana chumvi na wasiotakiana heri. Umoja wetu utatetereka na 
Muungano wetu unaweza kuvunjika. Kwa nini tufike huko?
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Sisi 
viongozi tuliopewa dhamana ya kuamua kwa niaba ya wananchi wetu, hatuna 
budi kuyapima mambo haya kwa umakini mkubwa ili tufanye uamuzi ulio 
sahihi. Tusije tukajutia uamuzi wetu tutakapoona watu wanafukuzana, 
wanauana na mali zao kuporwa. Na, tukifikia hatua hiyo Muungano 
kusambaratika halitakuwa jambo la ajabu.
Kwa 
kweli, unapoyatafakari haya, ni rahisi kuelewa kwa nini wazee wetu 
waasisi waliamua walivyoamua. Waliona mbali. Tusipuuze fikra zao na 
maono yao. Kuna hatari ya nchi yetu na watu wake kupoteza kila kitu 
tulichokijenga kwa miaka 50. Badala ya kujenga tunaweza kujikuta 
tumebomoa hata msingi katika nchi washirika. Baba wa Taifa, Mwalimu 
Julius Nyerere mwaka 1993 alituasa kuhusu hatari hiyo: "Hamuwezi kutenda
 dhambi kubwa namna hiyo bila adhabu... na adhabu nyingine zimo mle mle 
ndani ya kitendo hazisubiri."
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Siku moja
 kiongozi mmoja wa juu wa madhehebu ya dini nchini aliniuliza: "Hivi 
Serikali mbili zikiwa na matatizo jawabu ni kuongeza ya tatu? Si 
matatizo ndiyo yatazidi? Je, matatizo yakizielemea hizo Serikali tatu si
 kila mtu atachukua njia yake? Mtakuwa mmepoteza kila kitu. Mimi 
nawashauri msichoke kutafuta majawabu kwa matatizo ya hizi mbili! Huko 
mnakotaka kwenda kuna hatari nyingi".
Pengine na ushauri huu wa mtu wa Mungu nao ni vyema kuupa nafasi na kuutafakari.
Kazi Yenu Kubwa
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Mambo ya 
kuyasemea ni mengi mno lakini kwa sababu ya ufinyu wa muda, nisingeweza 
kuyazungumzia yote. Naamini, mtayaona katika kuipitia Rasimu na kwenye 
majadiliano yenu. Napenda kusisitiza kwenu kuwa kazi iliyo mbele yenu ni
 kubwa sana. Ni kubwa kwa maana mbili. Kwanza, jukumu lenyewe la kutunga
 Katiba ya nchi ni zito sana. Taswira ya nchi yetu itakuwaje na 
itaendeshwa vipi kwa miaka mingi ijayo iko mikononi mwenu. Ipeni nchi 
yetu hatima njema. Pili, ni kubwa kwa maana ya uzito wa mambo ya 
kujadili na kuyafanyia uamuzi. Kwa ajili hiyo, ni muhimu sana kuisoma 
Rasimu na Taarifa ya Tume kwa makini na kuzielewa. Jipeni muda wa 
kutafakari kila neno, kila sentensi, na kila dhana ili muweze kufanya 
uamuzi ulio sahihi. Mkifanya hayo mtakuwa mmeisaidia nchi yetu na 
Watanzania wote kupata Katiba nzuri.
Nimefarijika
 sana kusikia kuwa mtajigawa kwenye Kamati 12 wakati wa kujadili Rasimu.
 Huu ni utaratibu mzuri kwani mkiwa katika vikundi vya watu wachache, 
mtakuwa na mijadala ya kina zaidi. Watu wote wanaweza kupata fursa ya 
kutoa maoni yao, kwa kila kifungu na kila jambo linaloibuliwa na 
kuzungumzwa. Kwa kufanya hivyo, mtatimiza kwa ukamilifu jukumu lenu la 
kutunga Katiba. Wote mtakuwa mmeshiriki kujadili kila sura na vipengele 
vyake vyote. Mkimaliza kazi yenu mtapokea kwa haki sifa nzuri kama 
Katiba itakuwa nzuri, au lawama stahiki iwapo itakuwa kinyume chake.
Pongezi kwa Mwenyekiti wa Muda
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Nitakuwa 
mwizi wa fadhila kama nitamaliza hotuba yangu bila ya kutambua kazi 
nzuri iliyofanywa na Mheshimiwa Pandu Ameir Kificho, Spika wa Baraza la 
Wawakilishi, alipokuwa Mwenyekiti wa Muda wa Bunge hili. Kazi yake 
haikuwa rahisi hata kidogo, lakini kwa umahiri na ustadi mkubwa ameweza 
kufanikisha mambo kwa kiasi ambacho anastahili pongezi zetu sote. 
Anastahili pongezi kwa sababu yeye aliendesha Bunge hili bila ya kuwepo 
kwa kanuni. Tatizo hili hatakuwa nalo Mwenyekiti wa Kudumu kaka yangu 
Mheshimiwa Samuel Sitta.
Napenda 
pia kuwapongeza Waheshimiwa Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba kwa hatua 
mliyofikia. Hata hivyo, mmechukua muda mwingi katika hatua ya awali 
hivyo hamna budi kuongeza kasi. Naomba niwakumbushe kuwa mijadala yenu 
hii inafuatiliwa kwa karibu sana na Watanzania. Wamewekeza sana 
matarajio yao kwenu. Hamna budi, haiba na taswira ya uongozi muionyeshe 
wakati wote wa kuendesha mijadala yenu kwa lugha na vitendo vyenu. 
Wakati wa semina na mjadala wa kupitisha Kanuni za Bunge hili, baadhi ya
 wananchi wamekwazika sana na mwenendo wa baadhi ya Wajumbe. 
Hawakutegemea kuyaona matendo waliyoyaona mkifanya na kusikia maneno 
waliyoyasikia kutoka kwenye vinywa vya baadhi yenu.
Ni 
matumaini yangu na ya Watanzania wote kuwa hali ile haitajirudia tena 
katika awamu hii. Tusiwafikishe mahali Watanzania wakakata tamaa na 
Wajumbe wao au na hata chombo hiki muhimu sana kwa mustakabali wao na wa
 nchi yao. Tutoe hoja badala ya kupiga kelele (argue don't shout) au 
kuzomea. Hakuna haja ya kutumia lugha isiyokuwa ya staha katika 
kujieleza. Hakuna haja ya kukingiana ngumi, kutishiana hili na lile au 
hata kugombana. Ni utovu wa uungwana usiotegemewa kutoka kwenu. 
Tusiwaangushe wananchi wa Tanzania wanaotutegemea sana.
Wekeni Maslahi ya Taifa Mbele
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Ombi 
langu la mwisho kwenu ni kuwasihi kuwa wakati wote muongozwe na kujali 
maslahi mapana ya nchi yetu na watu wake badala ya kujali maslahi yenu 
binafsi au ya makundi yenu. Naomba kaulimbiu yenu iwe "Tanzania Kwanza".
 Najua kila mmoja wenu amekuja na maoni yake au atakuwa nayo kwa kila 
jambo litakalojadiliwa. Wengine wamepewa misimamo na vyama vyao au 
makundi yao. Si jambo baya na ni hatua muhimu ya kuleta mafanikio, kama 
misimamo hiyo na mawazo hayo ni ya kujenga.
Hata 
hivyo, mnachotegemewa kufanya ni kuwa tayari kuwianisha na kuunganisha 
mawazo yenu mazuri na ya wenzenu, ili kupata msimamo wa pamoja na uamuzi
 wa pamoja ulio bora. Kwa sababu hiyo, hamna budi kuwa tayari kusikiliza
 mawazo ya wengine, hata kama ni tofauti na yenu mliyokuja nayo. 
Tafuteni kilicho chema kwa yale yanayosemwa na watu wengine hata kama ni
 watu usiokubaliana nao au huwapendi au hampendani. Kunaweza kuwepo kitu
 chenye manufaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wajumbe;
Nawaomba 
muwe hodari wa kushawishi badala ya kulazimisha. Mkifanya hivyo 
hamtalazimika kutumia muda mwingi wa kula njama za namna ya kuwazidi 
maarifa wale mnaotofautiana nao kwa mawazo. Lazima pia mtafute namna ya 
kushirikiana na kuwasiliana na makundi mengine. Msitafute kushindana, 
hili ni jambo ambalo lazima wote mtoke hapa mkiwa washindi. Yaani lazima
 Watanzania wote washinde kwani wao ndiyo wenye Katiba yao. Nawapongeza 
viongozi wa vyama vya siasa na asasi mbalimbali kwa kutambua na 
kuthamini umuhimu wa kuwa na taratibu za mawasiliano, mashauriano na 
ushirikiano. Daima muwe watu wa kutafuta maridhiano. Mmefanya vizuri 
katika hatua ya awali. Mmejiwekea taratibu nzuri za kufanya hayo, 
tafadhalini zitumieni. Jengeni madaraja imara zaidi katika awamu hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Naomba 
nimalize kwa kuwaomba Watanzania wote tukiongozwa na viongozi wetu wa 
dini tumuombe Mola wetu ajalie rehema zake ili mchakato wa kutunga 
Katiba uende salama. Aliongoze Bunge hili na Wajumbe wake waweze kufanya
 uamuzi ulio sahihi na wenye manufaa kwa taifa letu kwa kila 
watakaloliamua.
Baada ya 
kusema maneno yangu mengi hayo, nirudie kukushukuru Mheshimiwa 
Mwenyekiti kwa kunipa fursa hii adhimu ya kulihutubia Bunge Maalum la 
Katiba. Nawatakieni kila la heri na mafanikio mema. Katiba Mpya 
Inawezekana, Timiza Wajibu Wako.
Mungu Ibariki Tanzania!
Mungu Libariki Bunge Maalumu la Katiba!
Asanteni sana kwa kunisikiliza! 
 
 
 
No comments:
Post a Comment