Friday, March 21, 2014

Tufanyekazi, Watanzania wana matarajio makubwa na gesi –Muhongo

1 (16) 
Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo akisisitiza jambo wakati wa kikao baina ya Wizara ya Nishati na Madini, Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) na makampuni washirika ya StatOil, BG Tanzania, Exxon Mobil na Orphir Energy. Katikati ni Rais na Meneja Mkuu wa Kampuni ya BG Kanda ya Afrika Mashariki Bw. Derek Hudson. 
2 (10) 
Rais  na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Exxon Mobil Bw. Rolf Michael de Jong   kwa niaba ya washirika  wa  makampuni  yanayofanya maandalizi ya utekelezaji wa Mradi huo wa gesi iliyosindikwa (LNG)  akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wakati wa kikao hicho.
3 (9) 
Mkuu wa Mashauriano wa Kampuni ya StatOil Tanzania Bw. Ole- Johan Lydersen wa kwanza mwishoni akiongea jambo wakati wa kikao hicho.
4 (9) 
Afisa Mipango Miji Bw. Daniel Nguno kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi akiongea jambo wakati wa kikao hicho cha majadiliano ya utekelezaji wa mradi wa LNG.

Na Asteria Muhozya, Dar es Salaam
Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo ameeleza kuwa, Watanzania wana matarajio makubwa kutokana na kugunduliwa kwa hazina kubwa ya gesi katika maeneo ya kina kirefu cha bahari.
Profesa Muhongo ameyasema hayo wakati wa kikao kati ya Wizara ya Nishati na Madini, Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) na makampuni washirika ya Statoil, BG Tanzania, Exxon mobil na Orphir Energy yanayofanya maandalizi ya utekelezaji wa mradi wa   gesi  iliyosindikwa (LNG).
Ameongeza kuwa, Serikali inayo nia ya dhati katika kutekeleza mradi huo ili kuhakikisha kwamba uchumi wa gesi unakuwa wa manufaa kwa Watanzania wote. Hivyo, wenye jukumu la utekelezaji wametakiwa kutekeleza mipango mikakati yao kwa kuzingatia muda husika, wakati huo huo wakifanyakazi kwa ushirikiano na mamlaka husika na kwa uwazi.
“Wananchi wana matarajio makubwa na gesi, msiiangushe Tanzania katika hili, hatutaki kuonekana waongo, mkichelewa mnatupa wakati mgumu. Sisi sote tunatakiwa kuongea lugha moja kwa wananchi. Tumejipanga vizuri tunachotaka ni kutekeleza mipango yetu”. Amesema Profesa Muhongo.
Katika hatua nyingine, Waziri Muhongo na Katibu Mkuu wa Wizara Bw. Eliakim Maswi, wamesisitiza kuwa makampuni hayo,  yanapaswa kuhakikisha kwamba mipango yao  ya utekelezaji wa mradi huo  inapaswa kwenda sambamba na matakwa   ya Sera ya  Gesi Asilia.
Katika kikao hicho, makampuni hayo washirika yamewasilisha  taarifa ya hatua waliyofikia katika  maandalizi ya utekelezaji wa mpango kazi wa mradi huo  na kueleza hatua mbalimbali ambazo zimefikiwa na zinazotakiwa kuchukuliwa ili utekelezaji wa mradi  ufanyike kama ulivyopangwa.
Aidha, katika taarifa hiyo wameainisha hatua mbalimbali ambazo watatekeleza katika maeneo ambayo gesi imegunduliwa vikiwemo vyanzo vya Zafarani, Lavani na Tangawizi katika kitalu namba 2 kilichopo mashariki mwa Mkoa wa Lindi.

No comments: