Friday, December 26, 2014

Ufisadi ni zao la Kutokuwa na hofu ya Mungu

Askofu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dk Alex Malasusa akihubiri katika ibada ya Krisimasi ya kuadhimisha kuzaliwa kwa Yesu Kristo katika Kanisa la Azania Front jijini Dar es Salaam

Askofu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dk Alex Malasusa amesema watanzania wengi hivi sasa wamekosa kitu muhimu na cha thamani katika maisha yao, ambacho ni kutokuwa na hofu ya Mungu.

Amesema kufuatia hali hiyo Tanzania imejikuta ikiingia kwenye vitendo vya rushwa na ufisadi, huku viongozi waliopewa dhamana na wananchi wakiweka mbele maslahi yao binafsi badala ya Taifa.
Askofu Malasusa ameyasema haya leo katika Kanisa la Azania Front jijini Dar es Salaam wakati akitoa salamu na akihubiri katika ibada ya Krisimasi ya kuadhimisha kuzaliwa kwa Yesu Kristo.

Malasusa amesema jamii ya watanzania kwa sasa ni kama vile watu wamepofushwa macho maana wanachokifanya ni kama hawaoni, kwani kila kiongozi amewekeza zaidi katika kujinufaisha yeye binafsi badala ya kufanya kazi kwa uadilifu kwa lengo la kuleta ustawi kwa Taifa na wananchi wake.
"Hofu ya Mungu ikitawala katika maisha yetu, viongozi watatenda mambo mema, hofu ya Mungu ikitawala ndani ya mioyo yetu hakika vitendo vya rushwa na ufisadi havitapata nafasi katika nchini yetu nzuri Tanzania,"anasema Askofu Dk Malasusa.

Askofu Dk Malasusa anasema hakuna faida ya watu kujilimbikizia fedha nyingi huku maelfu ya watanzania wakiendelea kuteseka na kupata tabu kila kukicha, hivyo aliwasahi watanzania na viongozi wote serikali kubadili fikra zao na kumuogopa Mungu ili Tanzania ipone.

"Wakristo tunahitaji kusimama kwa ujasiri na kukemea mabaya yote katika jamii yetu hata kama yanafanywa na marafiki zetu kwa kuwa neno linatuagiza kufanya hivyo. Bwana anasema 'woga ni dhambi', hivyo tuwe makini ili kuepuka dhambi hii yenye madhara kwa watu wengi katika taifa hili," alisisitiza Dk Malasusa.
CHANZO:MWANANCHI

No comments: