Saturday, February 14, 2015

Elimu ya msingi sasa ni miaka kumi


Rais Jakaya Kikwete akipitia kitabu cha Sera ya Elimu na Mafunzo baada ya uzindua jijini Dar es Salaam .Picha na Venance Nestory

Serikali imetangaza Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 inayohuisha na kufuta sera kadhaa zilizosimamia sekta hiyo, huku elimu ya msingi ikitakiwa kuwa ya bure na kuishia kidato cha nne, lakini wadau wa elimu nchini wana shaka kama utekelezaji wake utafanyika kwa ufanisi.

Sera hiyo inaweka msingi wa kutatua matatizo mengi ambayo yamekuwa yakilalamikiwa na wadau wa elimu kuanzia ufundishaji hadi maslahi ya walimu, ikitoa matamko ambayo Serikali inatakiwa iyatekeleze, mengi katika kipindi kifupi.

Katika sera hiyo, kutakuwa na mabadiliko makubwa kwenye mfumo wa elimu ya awali, msingi na sekondari utakaokuwa wa muundo wa 1+6+4+2+3+, mfumo ambao utamaanisha kuwa elimu ya msingi ambayo itaanzia chekechea hadi kidato cha nne, itakuwa ni lazima na ya bure, badala badala ya unaotumika sasa wa 2+7+4+2+3+, ikimaanisha chekechea ni miaka miwili, msingi saba, sekondari minne, elimu ya juu ya sekondari miaka miwili na elimu ya juu miaka mitatu na zaidi.

Katika mabadiliko hayo, umri wa kuanza shule pia utabadilika, sanjari na muda wa elimu msingi ya lazima kuwa miaka kumi.
Mabadiliko mengine ni kujumuishwa kwa mitalaa ya mafunzo ya ufundi, teknolojia ya habari ili kuwezesha wahitimu kupata au kuwa na soko nchini au nje.

Pia, sera hiyo imeainisha kuwapo kwa mkinzano baina yake na Sera ya Ajira na Utumishi wa Umma ya mwaka 1999 inayotamka kuwa sifa ya kuajiriwa katika utumishi wa umma kwa masharti ya kudumu ni kiwango cha elimu kisichopungua elimu ya sekondari ya kidato cha nne.

Pia, inaainisha sera hiyo kuwa ushirikiano wa Tanzania na nchi nyingine kikanda na kimataifa umeleta msukumo wa kurekebisha Sera ili kuzingatia masuala ya ushirikiano na utangamano.
Masuala hayo ni pamoja na kuoanisha mitalaa; ulinganifu wa viwango vya elimu na mafunzo; upimaji na utoaji tuzo;
Kutokomeza kutojua kusoma na kuandika pamoja na ulinganifu wa sifa za kujiunga na vyuo vya elimu na mafunzo; na kuleta ulinganifu wa mifumo ya elimu na sifa za wahitimu kikanda.
Kwa kuwa Tanzania siyo kisiwa, sera hiyo inajikita katika kuimarisha utangamano katika elimu na mafunzo ili kumjengea Mtanzania ujuzi, umahiri na uwezo wa kukabiliana na mahitaji yanayojitokeza katika ulimwengu wa kazi na maisha kwa ujumla.
Inasema sera hiyo mpya kuwa tangu kuanza kutekelezwa kwa Sera ya Elimu na Mafunzo (1995), Sera ya Elimu ya Ufundi na Mafunzo (1996) na Sera ya Taifa ya Elimu ya Juu (1999) kumekuwa na mabadiliko mbalimbali ya kisiasa, kijamii, kiuchumi, kisayansi na kiteknolojia ambayo yameleta changamoto na kuzifanya Sera hizo zipitwe na wakati.
Inaeleza sera hiyo kuwa mabadiliko ya kiuchumi duniani yamesababisha msukumo kwa nchi zinazoendelea na zilizoendelea ama kubadilisha au kuimarisha sera, programu na mikakati yake ili ziweze kuhimili ushindani wa kiuchumi na kuleta maendeleo endelevu ya kijamii, kisayansi na kiteknolojia.

No comments: