Monday, November 25, 2013

Dk Kitila: Nilishiriki kuandaa, kuhariri waraka


kitila“Nitafuata taratibu zote za chama kama zilivyoelezwa katika Kamati Kuu, nitashiriki kikamilifu katika kutuliza hali ya kisiasa ndani ya chama ili Chadema kibaki imara na kiendelee kuwa tumaini la Watanzania” Prime Dk Kitila. 
…………………………………………………………………….
Dar es Salaam. Aliyekuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Dk Kitila Mkumbo amezungumzia mambo sita yaliyojitokeza baina yake na wajumbe wenzake kabla ya kutimuliwa katika wadhifa huo.
Aidha, alisema alishiriki kuuandaa na kuuhariri ‘Waraka wa Mkakati wa Mabadiliko 2013’ uliokuwa mahususi kumwandaa aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho, Zitto Kabwe kuwa mwenyekiti.
Dk Mkumbo alivuliwa wadhifa huo akituhumiwa kufanya vitendo kinyume cha katiba na taratibu za chama hicho.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mhadhiri huyo wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alisema: “Waraka ulilenga kujenga hoja ya kufanya mabadiliko ya uongozi na kuainisha mikakati ya ushindi kwa mgombea mlengwa katika Uchaguzi Mkuu wa Chadema ambao kwa ratiba ya awali ulikuwa ufanyike Desemba mwaka huu.”
Alisema katika kikao cha Kamati Kuu kilichowavua wadhifa huo, wajumbe walisema waraka huo ulikuwa na upungufu na ulikiuka misingi na kanuni zilizoainishwa katika Katiba ya Chadema.
“Kwa kuwa dhamira yangu imekuwa ni kusukuma mabadiliko ambayo Watanzania wanayatizama nje ya mfumo wa sasa wa utawala, nilikiri makosa na niliomba msamaha na kuomba kujiuzulu nafasi zote za uongozi ombi ambalo lilipingwa na wajumbe. Mwanasheria wetu akawashauri kuwa tukijiuzulu tutaondoka na heshima zetu, akataka tufukuzwe ili tuondoke na aibu,” alisema Dk Mkumbo. Alisema kunapokuwa na uchaguzi ndani au nje ya chama, watu lazima wafanye mikakati akisema hata leo Chadema kunafanyika mikakati ya kuiondoa CCM madarakani mwaka 2015 na kwamba kitendo hicho siyo dhambi.
Alisema katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu wa ndani wa Chadema, kuna haki ya kujiandaa… “Sisi tunaamini mabadiliko, mimi na Mwigamba tulianza kutengeneza mkakati, kwanza tuainishe sababu za kutaka mabadiliko, pili tutafute nani anayefaa kuwa mgombea wetu.”
“Tuliazimia kwamba tukimpata tuchambue nguvu na udhaifu wake na pia kuchambua udhaifu wa mgombea tunayedhani atatoka upande wa pili. Tulifanya hivyo kwa siri na ilikuwa siri kati yangu mimi na Mwigamba kwa sababu mikakati ya uchaguzi ni siri.”
Alisema kuwa baada ya kukamilisha mchakato huo wangemfuata Zitto na kumwomba kuwa mgombea: “Ndiyo maana tulieleza katika waraka kwamba hatuna uhakika kama Zitto atakubali kugombea, tulitaka kufanya haraka kukutana naye, ila uchaguzi ulipohairishwa nasi tukatulia.”
Alisema kikao cha Kamati Kuu kilipokutana Zitto alikuwa hajui lolote kuhusu waraka huo, pia yeye (Dk Kitila), alikuwa hajui kama waraka huo ulikuwa umevuja kwa wanachama wa Chadema, wakiwamo wajumbe wa Kamati Kuu.
“Siamini kama kugombea nafasi yoyote ndani ya chama ni uhaini. Msingi namba moja wa Chadema ni demokrasia ambayo inatakiwa kuruhusu ushindani katika nafasi za uongozi na hasa wa juu. Wanasema uhaini kwa sababu ya wasiwasi wa siasa za ushindani katika chama chetu, hakuna uhaini wala hujuma,” alisema.
Alisema siasa za ushindani nchini hazijaanza leo na kutolea mfano jinsi uchaguzi wa Chama cha Tanu alivyokuwa na ushindani kati ya Mwalimu Julius Nyerere na Ally Sykes.
“Rais Barack Obama wa Marekani alianza mikakati mapema, waliomfikisha pale alipo ni watu wanne waliotengeneza mkakati wa kupata mgombea na kufanya ashinde bila Obama kujua,” alisema.
Alisema yeye na Mwigamba walitumia njia hiyo na kwamba baadaye wangemfuata Zitto, wangembembeleza na wanaamini kuwa angekubali, “Siasa za ushindani ndani ya vyama ndiyo huzaa ushindani wa kweli katika jamii na kujenga demokrasia ya kweli katika jamii.”
Alisema waraka huo ulioandaliwa na watu wawili unaoeleza udhaifu na nguvu ya Chadema ulikuwa siri,  lakini anashangazwa kuona viongozi wa chama hicho kuusambaza, huku akiwataka wanachama wa Chadema kuusoma waraka huo na kueleza uhaini wao ni nini.
Alisema waraka huo haukulenga kukibomoa Chadema, bali kujenga taasisi na kufafanua kuwa aliomba kujiuzulu nafasi yake si kwa sababu ya kuogopa aibu ya kufukuzwa isipokuwa kutambua jinsi wenzake walivyokosa imani naye.
Aliwataka wanachama wa Chadema kupigania kwa dhati misingi mama ya chama ikiwamo demokrasia ya ndani.
“Tutawashawishi Watanzania kwamba chama hiki ni cha demokrasia kwa sisi wenyewe kuonyesha ushindani ndani ya chama. Hakuna namna ya kuweza kudhihirisha hilo zaidi ya kuruhusu uchaguzi huru na watu washindane kwa hoja,” alisema Dk Kitila.
Alisema wanachama wa Chadema wanatakiwa kulaani tabia iliyoibuka ndani ya chama hicho kuwaita watu wenye mtazamo tofauti na viongozi kuwa ni wasaliti. “Kukataa siasa za ushindani ndani ya chama ni kuhujumu demokrasia na ndiyo usaliti, kukataa demokrasia na kukosolewa huo ndiyo usaliti wenyewe.”
Alisema lugha za kuitana wasaliti au wahaini zilitumika katika mataifa ya kikomunisti kunyamazisha upinzani na kuzaa udikteta kwenye mataifa hayo, kwamba utamaduni huo ukilelewa Chadema utajenga udikteta.
CHANZO: MWANANCHI

No comments: