Wednesday, February 12, 2014

Watanzania asilimia 33.4 watajwa maskini wa kutopea

umasikini_697ae.png

Dar es Salaam. Utafiti uliofanywa na Taasisi ya Utafiti wa Uchumi na Jamii (ESRF), umebaini asilimia 33.4 ya Watanzania wameghubikwa na umaskini uliokithiri jambo linalosababisha vifo, msongo wa mawazo, afya duni na utegemezi.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Kituo cha Redio cha Maendeleo kwa ajili ya kutoa taarifa za maendeleo kwa umma iliyozinduliwa na ESRF jana, Mhadhiri wa Uchumi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Oswald Mashindano alisema Watanzania wengi wanakabiliwa na umaskini uliokithiri kwa sababu ya kukosa nyenzo, mitaji na uwezo wa kuzalisha.

"Umaskini uliokithiri au umaskini sugu, hautumii kigezo cha kipato cha chini pekee lakini yapo matatizo yanayowakabili Watanzania muda mrefu na hayajapatiwa ufumbuzi," alisema Dk Mashindano.

Alisema mtu anayeshindwa kuyatatua matatizo haya hushindwa kumudu huduma muhimu kama maji, afya, elimu na kuongeza kuwa ni umaskini wa maisha yote kwa baadhi ya watu na huendelea kizazi hata kizazi.

"Utafiti wetu ulitumia kipimo cha kimataifa cha kuangalia umaskini uliokithiri kwenye nchi zinazoendelea (Multi dimensional Poverty Index)," alisema Dk Mashindano.
Aliongeza kuwa umaskini huo ni sugu kwa sababu tangu Tanzania ipate uhuru, Serikali imeshindwa kuuondoa na asilimia kubwa ya Watanzania wameghubikwa na hali hiyo.

Akizindua studio hiyo, Mkurugenzi wa Idara ya Kuondoa Umaskini wa Wizara ya Fedha, Anna Mwasha aliwapongeza ESRF kwa kuzindua studio hiyo ambayo itakuwa daraja muhimu kati ya wananchi na Serikali. Mwasha alisema lengo la kuanzisha kituo hicho ni kuboresha uaandaji na utoaji wa taarifa.

"Ni wakati ambao taarifa nyepesi zinazohitajiwa ziwafikie wanajamii kwa sababu matarajio ya Serikali ni kuona zinawafikia watu kwa urahisi ili kuondoa huo umaskini sugu," alisema Mwasha.
Pia, Mwasha alisema kituo hicho kikitumiwa vyema kitasaidia kuondoa umaskini sugu miongoni mwa Watanzania asilimia 33.4 waliotajwa kwenye utafiti huo wa ESRF.

Mkurugenzi wa ESRF, Dk Bohela Lunogelo alisema kituo hicho cha redio kitaandaa vipindi vya maendeleo kama kilimo, elimu na afya kwa kutumia vyanzo vya habari kama Taasisi ya Utafiti wa Tiba, (NIMR), Chuo cha Kilimo, (Sua) na tafiti zinazofanywa ndani ya nchi. Taarifa hiyo imekuwa ikifanya utafiti mbalimbali nchini
 Na Florence Majani, Mwananchi

No comments: