Tuesday, April 1, 2014

Jaji Warioba atukanwa kongamano la Muungano

warioba_f27d9.jpg
Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba, juzi alishambuliwa katika kongamano la kujadili Muungano lililoandaliwa na Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kwa wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu huku mmoja wa washiriki akidiriki kumtukana.
Kongamano hilo lililohudhuriwa na wanafunzi takribani 300 kutoka Tanzania Bara ba Visiwani, liliandaliwa kujadili namna ya vijana wanavyoweza kuulinda Muungano usivunjike.

Peter Magoti, mwanafunzi wa Chuo cha Diplomasia, alimshambulia Jaji Warioba kwa kudai asubiri afe ndipo Muungano uvunjike kwani amebakiza miaka mitano kufa na kwamba hawezi kuishi zaidi ya miaka mitano.

"Huyu Warioba amekuwa kiongozi katika serikali ya Muungano, alikuwa waziri mkuu pamoja na mwanasheria mkuu wa serikali na ameona faida ndio maana mpaka leo yupo na anaendelea kupata mshahara kama waziri mkuu mstafu, haoni hayo ni matunda ya serikali ya Muungano?" alihoji.
Magoti aliendelea kudai: "Warioba anatakiwa kujua kwa sasa serikali ipo mikononi mwa vijana ambao hawataki Muungano uvunjike kama anavyofikiria yeye."

Mwanafunzi mwingine kutoka Zanzibar, Juma Juma, alisema kumekuwa na upotoshaji wa kuhusu maoni yaliyotolewa na wananchi wa Zanzibar kuwa wanataka Muungano uvunjike, lakini ukweli Wazanzibari wanachotaka ni kwamba Muungano uboreshwe kwa maslahi ya pande zote mbili.

"Katika kila nchi lazima wanakuwapo wasaliti na hawa wanatumia mbinu nyingi kuwahadaa wananchi ili wawaamini, Maalim Seif Sharif Hamad ameonekana kuwa msaliti na mpenda madaraka toka kipindi akiwa CCM mpaka hivi sasa, anatumia uongo wa dhahiri kwa wananchi katika mikutano yake kuhusu maslahi ya Zanzibar katika Muungano," alidai.

Juma alisema viongozi wanatakiwa kujua kuwa kuwapo Muungano ndiyo heshima iliyonayo Tanzania, hivyo kama Muungano ukivunjia, nchi itakosa heshima hiyo.

Tangu Jaji Warioba alipowasilisha Rasimu ya Katiba ambayo pamoja na mambo mengine, ilipendekeza muundo wa Muungano wa serikali tatu, amekuwa akishambuliwa yeye binafsi na wanasiasa wa chama tawala-CCM na baadhi ya watu binafsi, wakidai anataka kuuvunja Muungano, ingawa tume hiyo ilikuwa na wajumbe 30.

No comments: