Dar es
Salaam. Jeshi la Polisi, Kanda Maalumu ya Dar es Salaam limewakamata
watu sita wanaodaiwa ni viongozi wa kundi la 'Mbwa Mwitu'
linalojihusisha na vitendo vya uvamizi na uporaji wa mali za watu kwenye
nyumba na maduka jijini humo.
Kamanda
wa Polisi kanda hiyo, Kamishna Suleiman Kova alisema kutokana na
kukamatwa kwa viongozi hao na kupatikana kwa taarifa za makundi hayo
jeshi lake litafanya msako wa nyumba kwa nyumba, mtaa kwa mtaa hadi
wahusika wote wakamatwe.
"Hawa
viongozi tunao, tumeshawahoji na wamekiri ni kweli wamekuwa
wakijihusisha na vitendo hivyo kwa kutumia makundi yao," alisema Kova na
kuongeza: "Sisi tunaanza kuwasaka hao vijana kwa sababu tumeshapata
taarifa za kutosha kutoka kwa wenzao...tunafahamu wapi pa kuwapata."
Aliwataja
waliokamatwa kuwa ni Athuman Said (20), Joseph Ponela na Clement Peter
(25) wakazi wa Kigogo, Roma Vitus (37), Mwanshishe Adam(37) na Daniel
Peter (25)wakazi wa Temeke.
Taarifa
hiyo imekuja siku moja baada ya kusambaa kwa taarifa za kundi hilo la
vijana zaidi ya 300 kuvamia mitaa mbalimbali ya jiji hilo, kupora mali
na kujeruhi watu.
Kamishna
Kova alisema kuwa jeshi lake lilifanikiwa kuwakamata viongozi hao baada
ya kupata taarifa kutoka kwa raia wema akisisitiza kwamba hatua
inayofuata ni kuwasaka vijana wanaowatuma kufanya uhalifu huo.
"Hii
itakuwa operesheni endelevu tunayoianza mwezi huu hadi mwezi Julai mpaka
tuhakikishe tumewakamata wahalifu hawa na tatizo hili
limetokomea,"alisema Kova kwa msisitizo.
Alisema
jeshi lake limejipanga kukabiliana na wahalifu hao na kuwa wananchi
waache kuwa na hofu kutokana na taarifa za uvumi zinazosambazwa kwenye
mitandao kuhusu uhalifu unaofanywa na vijama hao.
"Ningependa
kuwatoa hofu wananchi kuhusiana na uvumi unaoendelea kwenye
mitandao...tunaomba wananchi wawe watulivu waendelee na shughuli zao
kama kawaida. Jeshi langu limejipanga vizuri kuwadhibiti hao vijana. Hao
vijana hawana uwezo wa kutushinda sisi" alisema Kova
Kamanda
huyo aliweka wazi kuwa askari wa kutosha wa doria wameshapangwa maeneo
ambayo yametajwa kuwa na mlipuko wa makundi hayo.Maeneo hayo ni pamoja
na Kigogo, Manzese, Magomeni na Mbagala.
CHANZO MWANANCHI
CHANZO MWANANCHI
No comments:
Post a Comment