Tuesday, July 15, 2014

SERIKALI YANUSURU KUFUNGWA KWA OFISI YA KANISA LA MORAVIAN JIMBO LA KUSINI MAGHARIBI MBEYA

Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Dk. Norman Sigalla akiongea na baadhi ya wachungaji na waumini wa kanisa la Moravian kuwaomba wafunguo ofisi hizo ili mazungumzo yafanyike



 Mmoja wa wachungaji hao, Edward Chilale akiongea na Baadhi ya waandishi wa habari

Makamu Mwenyekiti jimbo hilo, Sichone, alisema kuwa amesikitishwa na kitendo kilichofanywa na kundi hilo ndani ya kanisa kwa kuwa kimeenda tofauti na taratibu za kanisa, ambapo mambo yote hufanywa kupitia vikao.





Moja ya waumini wa kanisa hilo akifungua mnyororo uliofungwa ofisini kwa Askofu 



Add caption



BUNDI mweusi amezidi kulikumba Kanisa la Moravian Jimbo la Kusini Magharibi kufuatia mgogoro wa muda mrefu ambapo safari hii baadhi ya waumini na wachungaji walitaka kufunga ofisi za Jimbo hilo wakishinikiza kujiuzulu kwa Askofu, Alinikisa Cheyo.
Tukio la kufunga ofisi za Jimbo hilo limetokea leo majira ya saa 12 asubuhi  ambapo baadhi ya Wachungaji na waumini wa kanisa hilo walifika katika makao makuu ya Jimbo yaliyoko Jakaranda jijini Mbeya wakiwa na makufuri yao.
Kanisa la Moraviani Tanzania, jimbo la kusini Magharibi kwa zaidi ya mwaka mmoja limekuwa katika mgogoro wa kiuongozi, baada ya kamati tendaji (KTM-JKM) kumsimamisha Mwenyekiti aliyechaguliwa kihalali kupitia mkutano Mkuu (Sinod), Nosigwe Buya kwa madai ya kushindwa kulisimamia kanisa na kumpandisha aliyekuwa Makamu wake, Zacharia Sichone, jambo lililoibua mpasuko.
Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Dk. Norman Sigalla King ndiye aliyenusuru kufungwa kwa kanisa hilo  baada ya kuwasihi wachungaji na Waumini wenye jazba kuwa na subira wakati Serikali ikijaribu kuona namna ya kutatua mgogoro huo.
Akizungumza na kundi hilo, Mkuu wa Wilaya, Dk. Sigalla aliyefika eneo hilo majira ya saa 3:20 aliwaomba wachungaji hao, kusitisha azima yao hiyo ya kuzifunga ofisi za Makao Makuu ya kanisa na kuwa na subira kwani siku inayofuata  serikali ingetoa msimamo juu ya mgogoro huo.
Akizungumza baada ya kukubali ombi la Mkuu wa Wilaya, mmoja wa wachungaji hao, Edward Chilale, alisema wamefika hatua hiyo baada ya Askofu Mkuu wa kanisa hilo,kupuuza madai yao ya kutaka kuitishwa kwa Mkutano Mkuu wa kanisa (Sinod) utakaoamua hatima ya mgogoro baada ya kusimamishwa kwa aliyekuwa Mwenyekiti wa jimbo hilo, Mwenyekiti Buya.
Mchungaji Chilale alisema licha ya kuheshimu kauli ya serikali ya kutaka kusitisha mpango wao wa kulifunga kanisa, bado shinikizo lao la kutaka Askofu Cheyo kujiuzulu bado liko palepale, kwani yeye ndio chanzo cha yote.
Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti jimbo hilo, Sichone, alisema kuwa amesikitishwa na kitendo kilichofanywa na kundi hilo ndani ya kanisa kwa kuwa kimeenda tofauti na taratibu za kanisa, ambapo mambo yote hufanywa kupitia vikao.
Alisema tayari wametoa taarifa jeshi la polisi na kwamba tukio hilo liliongozwa na wachungaji sita wa ushirika wa Bethlehemu ambalo kwa muda mrefu limekuwa likiendesha mambo kinyume na taratibu za kanisa.
Wachungaji hao pamoja na kukubali kufungua ofisi waliweka misimamo yao ambayo Miongoni mwa maazimio hayo ni kuutaka uongozi huo wa kanisa kubatilisha mara moja maamuzi yake ya kumsimamisha kazi Mwenyekiti huyo na asibughudhiwe hadi Mkutano Mkuu wa Sinodi.
Pia waliitaka halmashauri kuu iwe imeitisha Mkutano Mkuu wa Sinodi  Machi 3 mwaka huu na kwamba isipotii maazimio hayo ya wakristo watachukua hatua ya kuzifunga ofisi zote za jimbo na kufanya maandamano ya amani kwa kibali cha vyombo vya dola.
Mwisho.

Na Mbeya  yetu

No comments: