Friday, July 25, 2014

TAIFA STARS YAANZA WINDO TUKUYU

zoezi_stars

KOCHA mkuu wa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Mholanzi Mart Nooij ameanza kuwavutia kasi Msumbiji (Black Mambas) kuelekea mchezo wa marudiano wa kuwania kupangwa hatua ya makundi, kusaka tiketi ya kucheza fainali za mataifa ya Afrika, AFCON, mwakani nchini Morocco.
Stars iliyotoka sare ya 2-2 mwishoni mwa wiki iliyopita, uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam, itakabiliana na 'Black Mambas' katika mechi hiyo ya marudiano kati ya Agosti 2 na 3 ndani ya uwanja wa Taifa wa Zimpeto, mjini Maputo.

Meneja wa Taifa Stars, Boniface Clemence amesema timu imewasili jana Mkoani Mbeya kwa ndege ya Fastjet tayari kwa kuanza kambi ya kijiwinda na mechi hiyo muhimu.
"Tuliwasili uwanja wa ndege wa kimataifa wa Songwe kwa ndege ya Fastjet na moja kwa moja tukaenda Tukuyu na jioni timu ilifanya mazoeni". Alisema Clemence.

Meneja huyo aliongeza kuwa kwasasa kocha mkuu, Nooij anafanyia marekebisho makosa yote yaliyojitokeza kwenye mechi ya kwanza iliyopigwa julai 20 mwaka huu jijini Dar es salaam.
"Mwalimu anafanya kazi ya kuangalia wapi kuna mapungufu na kuongezea mbinu zaidi za kuwafungwa Mambas". Alisema Clemence.

Kuhusu wachezaji wa kimataifa, Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu wanaocheza TP Mazembe ya DR Congo pamoja na Mwinyi Kazimoto anayecheza klabu ya Al Markhiya ya nchini Qatar, Clemence alisema wote walikuwa na tiketi za kurudi siku ile ile baada ya mechi, hivyo hawapo kambini.

Meneja huyo alisema nyota hao wataungana na timu moja kwa moja Mjini Maputo siku moja kabla ya mechi, lakini wachezaji wengine wote wapo kambini na wana morali kubwa.
Kwasababu Mbeya hakuna ndege ya moja kwa moja kwenda mjini Maputo, Taifa Stars watarudi jijini Dar es salaam, Julai 30, tayari kwa safari ya ya kwenda Msumbiji.
Kuhusu kupitia Afrika kusini, Clemence alisema muda umewabana na hawana uhakika wa kwenda huko.

No comments: