Wednesday, August 20, 2014

Serikali kulipia wanafunzi wa sayansi wapatao 5000 ngazi ya stashahada mwaka wa masomo 2014/15

Mkurugenzi-Msaidizi-wa-Habari-Elimu-na-Mawasiliano-wa-Bodi-ya-mikopo-Tanzania-Cosmas-Mwaisobwa.
NA SULEIMAN MSUYA
KATIKA juhudi za Serikali za kukabiliana na upungufu wa uchache wa waalimu wa masomo ya sayansi na hisabati kwenye shule mbalimbali za msingi na sekondari hapa nchini imesema italipia wanafunzi wapatao 5000 wa ngazi ya stashahada katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kwa mwaka wa masomo 2014/15.
Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi wa Habari, Elimu na Mawasiliano wa Bodi ya Mikopo Tanzania Cosmas Mwaisobwa wakati akiongea na mwandishi wa habari hii leo jijini Dar es Salaam.
Alisema uamuzi huo unakuja kutokana na ukweli kuwa waalimu wa masomo hayo wamekuwa wachache jambo ambalo linakwamisha juhudi za serikali katika kukuza sekta hiyo kwa siku za karibuni na zijazo.
Mwaisobwa alisema mpango huo utakuwa endelevu hadi hapo ambapo tatizo hilo litakapokwisha ili kuhakisha kuwa shule zote za serikali ziweze kukidhi mahitaji hayo.
Mkurugenzi huyo wa Habari, Elimu na Mawasiliano alisema serikali imekichagua chuo kikuu cha Dodoma kutokana na kuwepo na nafasi ambayo inaweza kupokea idadi hiyo ya wanafunzi.
“Nadhani kila mtu ni shahidi kuwa waalimu wa sayansi na hisabati wapo wachache sana hivyo tumeamua kuwakopesha wanafunzi wa stashahada ili waweze kuziba pengo kubwa lililopo”, alisema.
Akizungumzia juu ya mwitikio wa wafaidika na mikopo kurejesha mikopo waliyokopeshwa na Bodi hiyo alisema ni mkubwa ambapo kwa mwezi zaidi ya shilingi bilioni 3 hurejeshwa.
Mwaisobwa alisema mrejesho huo ni mzuri ila bado wanatoa rai kwa wafaidika wote kuendelelea kurejesha ili kuhakikisha kuwa wanafunzi wengine wanafaidika na mkopo ili waweze kusoma elimu ya juu.
Alisema pamoja na mwitikio huo bado kuna changamoto kubwa kwa baadhi ya wafaidika ambao wamekuwa hawatoi ushirikiano mzuri jambo ambalo linakwamisha juhudi zao za kukusanya fedha hizo.
Mkurugenzi huyo wa Habari, Elimu na Mawasiliano alisema katika kuhakikisha kuwa wanakabiliana na changamoto hiyo wameingia mikataba na wakala mbalimbali katika kanda tofauti ili kusaidia ukusanyaji wa madeni.
Alisema zoezi hilo la ukusanyaji limekuwa rahisi kutokana na uwepo wa mfumo ambao unaonyesha wahusika wote ambao wamefaidika na wanaofaidika kwa sasa.
Kuhusiana na wanafunzi ambao walichelewa kupata fedha za mafunzo alisema bodi inafanyia kazi na matarajio yao ni kwamba mwishoni mwa wiki hii watakuwa wamepata fedha hizo.
Alivitaja vyuo ambavyo wanafunzi wake wamechelewa kupata mikopo ni St. Augustine, Stephano Memorial, IFM, Teofelo Kisanji.

No comments: