Thursday, July 9, 2015

TANO BORA YA CCM KUJULIKANA DODOMA

Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye.
Dodoma.
Kisu kikali cha Kamati Kuu ya CCM (CC) leo kitaondoka na vichwa 33 kati ya 38 vya walioomba kuteuliwa kupeperusha bendera ya chama hicho kumrithi Rais Jakaya Kikwete anayemaliza ngwe yake.
Makamu Mwenyekiti wa CCM (Bara) Ndugu Philip Mangula.
Kikao hicho ni hatua ya pili baada ya kukamilika kwa kikao cha Kamati ya Maadili kilichokutana jana usiku chini ya Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete huku kikitawaliwa na usiri mkubwa, kuhama ukumbi na kila dalili za kubadili ratiba iliyopangwa awali ili kuvuruga mipango ya kambi za wagombea.

Habari zilizolifikia gazeti hili zilisema kulikuwa na uwezekano wa kubadili ratiba ili vikao vya Kamati ya Maadili na CC ama vifuatane au vifanyike usiku ili kuyanyima makundi nafasi ya kujipanga.
Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Jakaya Kikwete.
Alipoulizwa jana kuhusu vikao hivyo, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alidai kuwa hata yeye hakuwa na uhakika wa lini na muda gani hasa kikao cha Kamati ya Maadili kingefanyika.

Awali, vifaa vya ukaguzi wa wajumbe vilikuwa vimewekwa katika Makao Makuu ya CCM, White House lakini baadaye jioni viliondolewa na hapakuwa na taarifa zozote zilizotolewa.

Habari zilizopatikana baadaye zilidai kuwa kikao hicho cha Maadili kilitarajiwa kufanyika Ikulu ya Dodoma kuanzia saa nne usiku wa jana.

Haya yanajitokeza wakati macho na masikio ya Watanzania yakiwa hapa Dodoma kusikiliza namna kazi ya kuchuja wagombea itakavyofanyika na kujua ni watu gani 33 watakaoanza kulambwa na kisu cha CC, hasa kwa majina makubwa yanayotazamwa na wengi, mara tu baada ya kujadiliwa na Kamati ya Maadili.
Katibu Mkuu wa CCM Ndugu Abdulrahman Kinana.
Kazi za Kamati Kuu leo

Kikao cha CC kina majukumu matatu leo ambayo ni kufikiria na kutoa mapendekezo kwa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), majina yasiyozidi matatu ya walioona kuwania urais wa Zanzibar ambayo imeombwa na Rais wa sasa, Dk Ali Mohamed Shein pekee, kufikiria na kutoa mapendekezo kwa NEC majina yasiyozidi matano ya walioomba kuwania urais wa Muungano na kuandaa mkutano wa NEC.

Vigezo vya maadili

Kulingana na kanuni za Uongozi na Maadili, toleo la 2012 kifungu cha 4(ii), kuhusu taratibu za kuomba uongozi, wanachama wanaogombea uongozi ambao uteuzi wao hufanywa na vikao vya kitaifa, watachunguzwa kwanza uadilifu wao na chombo cha maadili cha CCM kwa ushirikiano na vyanzo vingine.

Kanuni hizo zinasema mwanachama wa CCM anapoomba uongozi katika ngazi yoyote, itikadi na mwenendo wake vitachunguzwa kwanza na Kamati ya Usalama na Maadili inayohusika, ndipo maombi hayo yaliyoambatanishwa na mapendekezo ya kamati hiyo yatakapofikishwa mbele ya kikao chenye madaraka ya kutoa uamuzi.
Ikiwa mwanachama hakupendekezwa kwa sababu ya kukiuka Katiba ya CCM, Kanuni za CCM na sheria ya nchi, hatakuwa na haki ya kukata rufaa kwa mtu yeyote au kikao chochote. Lakini ikiwa mwanachama atakataliwa kugombea kwa sababu ya madhambi yake katika chama, basi ni wajibu wa Kamati ya Usalama na Maadili kumjulisha makosa yaliyomnyima haki ya kugombea, naye anaweza kukata rufaa kwa mujibu wa haki zake kikatiba.

Mtu yeyote anayetuhumiwa mbele ya Kamati ya Usalama na Maadili ya ngazi yoyote, kwa kosa lolote linalohusiana na maadili au nidhamu ya chama atasomewa na kutakiwa kuzijibu tuhuma hizo mbele ya wajumbe wa kamati hiyo ama kwa kauli yake mwenyewe au kwa maandishi, lakini hataambiwa nani aliyezileta tuhuma hizo, isipokuwa kama imekwishajulikana mapema kutokana na mijadala ya vikao, vyombo vya sheria au vyombo vya habari.

Kanuni ya maadili inaendelea kusema kuwa uchambuzi wa tuhuma hizo utafanywa kwa kutumia njia mbalimbali pamoja na mashahidi watakaopatikana.

Uchunguzi utakapokamilika na endapo itadhihirika kwamba tuhuma zina uzito, mtuhumiwa ataitwa mbele ya kikao cha Kamati ya Usalama na Maadili ya ngazi inayohusika, kama ni lazima, ili apate kuhojiwa ana kwa ana.

Pia, kanuni inasema Kamati ya Usalama na Maadili ya ngazi inayohusika itatoa mapendekezo yake kuhusu suala hilo kwenye kikao cha uamuzi kinachohusika. Mtuhumiwa atapewa nakala ya uamuzi kwa maandishi.

Wagombea wanne kukosa CC

Katika kikao cha CC kinachofanyika leo, wajumbe wanne ambao ni miongoni mwa majina 38 yatakayojadiliwa katika mchujo huo watalazimika kukaa kando ili kukwepa mgongano wa masilahi.

Wajumbe hao ni Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, Waziri wa Sheria na Katiba, Dk Asha-Rose Migiro, Makamu wa Rais, Dk Mohamed Ghalib Bilal na Waziri wa Kilimo na Chakula, Stephen Wasira.

Kwa mujibu wa Kanuni za Uteuzi wa Wagombea wa CCM katika Vyombo vya Dola, Toleo la Pili – Februari, 2005, ukurasa wa 25, kifungu cha 21 (3); wajumbe wa vikao vya uchujaji na uteuzi wa wagombea kwa ngazi inayohusika hawaruhusiwi kuendelea na kazi ya uchujaji na uteuzi iwapo wao ni wagombea katika ngazi hiyo.

Kanuni hiyo pia imetoa miiko ya shughuli za uchujaji na uteuzi wa wagombea na wajumbe wote wanatakiwa na kanuni kuzingatia maadili na nidhamu ya chama katika kusimamia na kutekeleza shughuli za uteuzi.

Kanuni hizo zinasema ni mwiko kwa kiongozi yeyote kwa maneno au vitendo kumpendelea au kumsaidia kupata kura nyingi mwombaji mmoja dhidi ya mwingine, kutumia au kuhusisha ukabila, dini, rushwa, rangi, hila na eneo analoishi au anakotoka katika shughuli yoyote ya uchaguzi.

Pia, ni mwiko kwa kiongozi yeyote au mwombaji yeyote wa nafasi ya uongozi au mwanachama yeyote aliyekabidhiwa dhamana ya usimamizi au uangalizi au uratibu wa kura za maoni, uchujaji na uteuzi, kufanya vitendo vya ukiukwaji wa kanuni.
Kuhusu misaada, kifungu cha tano (a) kinasema ni marufuku kwa mgombea yeyote mtarajiwa au wakala wake, kufanya vitendo vyovyote vinavyoonekana dhahiri kuwa ni sehemu ya kampeni za kuwania nafasi anayoitafuta kabla ya muda rasmi wa uongozi unaohusika haujamalizika.

Kanuni imetoa adhabu kwa watakaovunja miiko hiyo na kwa kiongozi atakayethibitika kuivunja atavuliwa uongozi na kwa mwanachama anayeomba kugombea nafasi yoyote atakayethibitika kuivunja hiyo hatateuliwa kugombea nafasi anayowania.

(CHANZO: MWANANCHI)

No comments: