Monday, September 17, 2018

Matumizi ya dawa za kulevya yapungua kwa asilimia 90


Waziri Kassim Majaliwa amesema matumizi ya dawa za kulevya nchini yamepungua kwa asilimia 90 baada ya Serikali kufanikiwa kudhibiti biashara hiyo.

Ameyasema hayo leo (Jumatatu, Septemba 17, 2018) baada ya kufungua mkutano wa 28 wa wakuu wa vyombo vinavyopambana na dawa za kulevya kutoka nchi za Afrika ujulikanao kama (28th HONLEA- Afrika), jijini Dar es Salaam.

Mkutano huo unaofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere(JNICC), unashirikisha wajumbe zaidi ya 120 kutoka nchi 54 za Afrika unatarajiwa kutoka na maazimio ya namna ya kutokomeza biashara ya dawa za kulevya katika mataifa hizo.

Waziri Mkuu amesema lengo la mkutano huo ni kubadilishana uzoefu na kupanga mikakati ya pamoja kuhusu udhibiti na mapambano dhidi ya biashara ya dawa za kulevya katika nchi hizo.

"Ni lazima tuwe na mikakati ya pamoja ya kudhibiti uzalishaji, usambazaji na matumizi ya dawa za kulevya barani Afrika. Hata hivyo ni muhimu kudhibiti njia zote zinazotumika kusafirisha dawa za kulevya."

Hata hivyo, Waziri Mkuu amesema Tanzania inaendelea na mikakati ya kupambana na uzalishaji wa dawa hizo ikiwemo mirungi na bangi,ambayo inapandwa kwa kuchanganywa na mazao ya chakula.

Hata hivyo, Waziri Mkuu amesema Tanzania ni nchi ya kwanza katika bara la Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara kuanzisha vituo vya utoaji wa matibabu kwa waathirika wa dawa za kulevya mwaka 2011.

No comments: