Monday, December 10, 2012

JK: Atunuku Nishani 40 siku ya miaka 51 ya UHURU



 Bi. Kidude akiveshwa nishani na Rais Jakaya Kikwete Ikulu jana
Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete leo mchana ametunuku  nishani kwa watu kutoka makundi mbalimbali yajamii waliotumikia taifa kwa uadilifu na kutoa mchango wa pekee.Miongoni wa waliotunukiwa nishani jana ni pamoja na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue, Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufaa Eusebia Munuo pamoja na Msanii Mkongwe Bi.Fatma Baraka Khamis(Bi.Kidude).Wengine waliotunikiwa nishani ni pamoja na Watumishi wa umma na askari Jeshi na Polisi.
Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufaa, Eusebia Munuo akivishwa nishani
Rais jakaya Kikwete akimvisha nishani Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue  ikulu Jijini Dar es Salaam.
    Picha na IKULU
 
 

Majambazi Waipora hadi Maiti

Mhudumu wa chumba cha kuhifadhia maiti hospitali ya Mkoa  Singida, akirekebisha mapambo ya jeneza lililokiwa na mwili wa marehemu Munchari Lyoba, mwanafunzi wa SUA , jeneza lililovunjwa na majambazi na maiti kupekuliwa yakitafuta fedha zaidi baada ya kupora wasindikizaji. (Picha na Gasper Andrew)
 
WATU wanaodhaniwa kuwa ni majambazi, wamevamia gari lililokuwa linasafirisha maiti kutoka mjini Morogoro kwenda mkoani Mara kisha kupora  takriban Sh19.8 milioni walizokuwa nazo waombolezaji.
Katika tukio hilo la kusikitisha lililotokea juzi mkoani Singida,  majambazi hao walivunja vioo vyote vya gari pamoja na jeneza lililokuwa na mwili wa Munchari Lyoba aliyekuwa mwanafunzi  wa mwaka wa tatu katika Chuo Kikuu cha Sokoine (SUA) cha Morogoro na kumpekua marehemu.
Akizungumza na waandishi wa habari jana nje ya chumba cha kuhifadhi maiti cha Hospitali ya Mkoa wa Singida, mkuu wa msafara uliokuwa ukisafirisha maiti,  Makaranga alisema kuwa tukio hilo lilitokea juzi saa 7:30 usiku katika gari aina ya Land Cruiser mali ya SUA.
Akisimulia tukio hilo, Makaranga alisema kuwa lilitokea katika Barabara Kuu ya Dodoma – Mwanza nje kidogo ya Mji wa Singida kwenye kona maarufu kwa jina la Mohammed Trans kuelekea mkoani Mara.  
Alisema kuwa gari hilo pamoja na jeneza, lililobeba viongozi wa wanafunzi sita na viongozi wengine wanne lilipofika eneo la tukio, walikuta mawe makubwa yamepangwa barabarani na kuwalazimisha kusimama ndipo wakavamiwa na kundi kubwa la vijana, ambao walibeba bunduki mbili aina ya gobore, marungu, mashoka na mawe.  
“Walipofika walipiga kioo cha gari letu kwa mbele na kumparaza kwa panga usoni dereva wetu. Baada ya hapo walivunja vioo vyote na kutuamuru kutoa kila kitu tulichokuwa nacho,” alisema Makaranga.  
Makaranga alisema kuwa katika tukio hilo, aliporwa Sh2 milioni alizokabidhiwa azihifadhi kwa ajili ya kugharimia msafara huo, Sh8.8 milioni zilizochangwa na wanafunzi kama rambirambi kwa  mwenzao na jumla ya Sh9 milioni ambazo wasindikizaji walikuwa nazo mifukoni mwao.  
“Pia tuliporwa simu  zetu zote  za mikononi, viatu, laptop na mabegi yote ya nguo zetu,” alisema.  
Makaranga aliyeeleza kuwa anafanya kazi za kiutawala SUA, aliwataja walioumizwa na majambazi hao kuwa ni pamoja na yeye, dereva wao na kiongozi wa wanafunzi, Idd Idd ambao walitibiwa katika Hospitali ya Mkoa wa Singida na kuruhusiwa.
Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mwalimu Queen Mlozi, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kuwa amewasiliana na uongozi wa SUA ili watume gari lingine na kukarabati jeneza lililoharibiwa na majambazi hao.
Mlozi aliongeza kuwa kwa ushirikiano wa Jeshi la Polisi na Kamati ya Ulinzi na Usalama, watahakikisha watu waliofanya unyama huo, wanakamatwa haraka iwezekanavyo ili waweze kufikishwa mbele ya vyombo vya sheria.  
“Nimesikitishwa sana na tukio hili, inaelekea sasa binadamu tunaanza kutoka kwenye utu na kuhamia kwenye vitendo ambavyo binadamu wa Mwenyezi Mungu hawezi kuthubutu kuvifanya. Watu wanafikia hata kufungua jeneza na kuanza kulisachi,” alisema  Mlozi akionyesha masikitiko.  

MICHEZO

TIMU YA BUNGE SPORTS CLUB YA TANZANIA YAIKANDAMIZA BUNGE YA KENYA MAGOLI 5-0

     Tanzania Bunge Sports Club Football imefanya maajabu katika uwanja wa Nyayo jijini Nairobi jana kwa kuwabamizwa wenyeji wao timu ya Kenya Bunge Sports Club Football mabao 5 kwa nunge katika michezo ya mabunge ya nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki yanayoendelea jijini Nairobi. Mashindano hayo yaliyofunguliwa rasmi juzi tarehe 7 Disemba na Spika wa Bunge la Afrika Mashariki Mh. Margreth Natongo Zziwa akisisitiza “let the best team win” tayari yamezikutanisha timu ya Bunge la Uganda na timu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ambapo timu hizo zimetoka sare ya
Wakati wa kuhitimisha karamu ya mabao kwa timu ya Kenya, Watanzania walijikuta uwanjani peke yao wakishangilia huku mashabiki-wenyeji wakiwa wameondoka uwanjani hapo. leo Tanzania itapambana na Rwanda kwenye mpira wa miguu katika uwanja wa City Stadium, na  Wabunge wanawake watakutana na Kenya kwenye mpira wa kikapu Nyayo Stadium. Mashindano haya yanalenga kuimarisha ushirikiano na kuitangaza zaidi Jum uiya ya Afrika Mashariki.
Katika mashindano haya ambayo hufanyika kila mwaka huyakutanisha mabunge ya nchi za Tanzania, Kenya, Uganda, Burundi na Rwanda. Waratibu wa michezo hii ni Jumuiya pamoja na Bunge la Afrika Mashariki. Kwa mwaka huu Burundi haikushiriki.
Chini ya ukufunzi wa Naibu Waziri (TAMISEMI) Mhe. Kasim Majaliwa (Mb) .na uongozi wa Mhe. Idd Azzan (Mb) mabao hayo yalifungwa na Mhe Amos Makala (Mb), Yusuf Soka (2), Mark Tanda na Mhe. Joshua Nassari. (Na Prosper Minja)
         Kikosi cha Tanzania
Tanzania yaendeleza ubabe wa kwa timu za mabunge ya nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki baada ya timu ya mpira wa kikapu wananwake kuinyanyasa Kenya Bunge Sports Club kwa mabao 51-25. Wakati huohuo, timu ya wanaume imeedelea kutoa adhabu kali leo ikiwa ni zamu ya Rwanda ambapo hadi kipenga cha mwisho Tanzania 6 Rwanda 0. Jana Kenya ilibamizwa bao 5-0
         Kikosi cha Kenya
     Mwanzo wa karamu ya mabao

No comments: