Thursday, November 14, 2013

Kilichomuua Dk Mvungi


Dk Sengondo Mvungi.PICHA|MAKTABA

Hospitali ya Millpark ya Johannesburg, Afrika Kusini, imesema madaktari waliokuwa wakimtibu aliyekuwa Kamishna wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Dk Sengondo Mvungi walibaini kuharibika kwa ubongo wake kutokana na kumwagika kwa maji yanayoutunza ambayo kitaalamu yanaitwa ‘cerebrospinal fluids’ au CCF.

Msemaji wa Hospitali hiyo, Tebogo Nyembezi alisema Dk Mvungi alicheleweshewa tiba baada ya kupata tatizo la maji hayo yanayotunza ubongo kumwagika mara baada ya kujeruhiwa.
Dk Mvungi (61), alipata majeraha makubwa baada ya kujeruhiwa na watu waliovamia nyumbani kwake Kibamba, Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam, Novemba 3 mwaka huu. Alifariki dunia jana mchana.
SOMA ZAIDI.....

 
“Maji hayo ambayo ni miligramu 50 tu katika ubongo wa mwanadamu ambayo huufanya ubongo uelee yakimwagika nusu tu, basi mgonjwa yupo hatarini, lakini akiwahishwa na kupata tiba sahihi anaweza kupona,” alisema Nyembezi.

Alisema iwapo mgonjwa atapewa tiba sahihi ndani ya saa 48, ubongo wake unaweza kurudi katika hali ya kawaida, lakini saa hizo zikizidi hawezi kupona kabisa kwa sababu maji hayo yanapomwagika ubongo hujigonga kwenye mifupa ya sakafu yake na kuharibika kabisa.

Mtaalamu wa mishipa na neva za fahamu (neurosurgeon) katika Hospitali ya Regency, Dar es Salaam, Dk Hariff Najin alisema kazi kubwa ya maji hayo ni kuulinda ubongo pindi inapotokea ajali ili usidhurike lakini endapo maji hayo yatamwagika nao huharibika.
“Haya maji yanaufanya ubongo uelee na usielemee kichwa. Hivyo inapotokea maji haya yakaisha au kupungua, ubongo hujigonga na kukosa ukinzani na kuharibika,” alisema.
Alisema maji hayo ambayo hufika hadi kwenye uti wa mgongo yakikosekana katika ubongo, husababisha damu isitembee kwenye eneo hilo jambo ambalo pia linaweza kusababisha mishipa katika sehemu ya nyuma ya ubongo kuharibiwa.

Akizungumzia suala hilo, Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Upasuaji wa Mishipa ya Fahamu Muhimbili (Moi), Profesa Lawrence Museru alisema anachofahamu ni kuwa Dk Mvungi alipelekwa Afrika Kusini kwa kuwa alipata madhara makubwa kwenye ubongo na wala si kwa sababu ya kumwagika kwa maji kama ilivyoelezwa Afrika Kusini.
“Majeraha hayo yalisababisha damu kuvilia katika ubongo na kusababisha uvimbe ambao kwa kitaalamu unaitwa ‘traumatic brain injury’ na sisi tulithibitisha vipimo hivyo vya awali na kumsindikiza mpaka huko,” alisema Profesa Maseru.

Profesa Museru alisema Dk Mvungi alipata majeraha makubwa kichwani na sehemu nyingine mwilini ambayo yanaonekana yalisababishwa na kupigwa kwa vitu vyenye ncha kali au magongo na hivyo kuleta madhara katika ubongo.

Alisema hawezi kuthibitisha chanzo hasa cha kifo hicho kwani kinaweza kuwa ni kuharibika kwa ubongo au sababu nyingine zilizotokana na tatizo hilo (secondary causes).
Naye Dk Mugisha Clement ambaye alimuhudumia Dk Mvungi alipofikishwa Moi na baadaye kumsindikiza hadi Afrika Kusini, alisema kitaalamu kumwagika kwa maji yanayolinda ubongo hakuwezi kuleta madhara kama aliyoyapata mwanasheria huyo, bali tatizo lilikuwa ni kuvimba na kuvilia damu katika ubongo.

“Maji ya CSF hayakuwa sababu ya kifo cha Dk Mvungi, sisi tulitambua tatizo la awali kuwa majeraha yalisababisha kuvimba na kuvilia damu. Kitaalamu haiwezekani maji hayo yakasababisha madhara makubwa,” alisema.
Kucheleweshwa kwa matibabu

Kuhusu kutokuwapo kwa opereta wa mashine ya CT Scan inayotumika kupima ubongo siku ambayo Dk Mvungi alipelekwa Moi, Profesa Museru alisema hatua za kinidhamu zitachukuliwa.
Hata hivyo, alisema kukosekana kwake hakukusababisha au kuchochea madhara kwa Dk Mvungi.
“Ni kweli kutokuwapo kwa opereta ni kosa lakini halikuwa na madhara kwa Dk Mvungi kwa sababu hakuwa akihitaji upasuaji wa haraka. Lakini ni kosa limefanyika,” alisema Profesa Maseru.
Alisema matumizi ya CT Scan ni ya muhimu lakini, hata kipindi cha nyuma ambacho wagonjwa walipata matatizo katika ubongo bado walitibiwa bila ya kuwapo ulazima wa kupata huduma ya mashine hiyo.

CHANZO: MWANANCHI
KINGOTANZANIA

No comments: