Thursday, December 12, 2013

Bunge la Tanzania lapitisha Azimio la kuwataka Ghasia, Mwanri na Majaliwa kujipima...

ghasia 6dab3
.Bunge limepitisha azimio la kuwataka mawaziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), kujipima iwapo wanatosha kuendelea kuongoza wizara hiyo nyeti.

Azimio hilo lilipitishwa jana na wabunge kwa kura ya ndiyo bila kupingwa, baada ya kuhojiwa na Spika wa Bunge Anne Makinda iwapo wanaipokea taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (Laac) iliyowasilishwa na Mwenyekiti wake Rajabu Mbaruku.
Soma zaidi...


Moja ya mapendekezo yake ni Waziri wa Tamisemi, Hawa Ghasia na manaibu wake, Aggrey Mwanri na Kassim Majaliwa kujipima kama wanatosha kuendelea kuongoza wizara hiyo kutokana na kugubikwa na vitendo vya ufisadi.

Kwa mujibu wa taratibu za Bunge, taarifa ya kamati inapowasilishwa na kupitishwa pamoja na mapendekezo yake, huwa ni azimio kamili ambapo Serikali hutakiwa kutoa maelezo ya utekelezaji wake.

Kabla ya azimio hilo kupitishwa, Mwenyekiti wa Laac, Rajabu Mbaruku alijibu michango ya wabunge waliochangia katika taarifa ya kamati yake iliyowasilishwa Ijumaa iliyopita, akiwemo Waziri Ghasia.

Akizungumza baadaye, Mbaruku alisema hayo ndiyo mapendekezo na Serikali itatakiwa kuyatolea maelezo ya jinsi yatakavyotekelezwa. "Hata waziri mkuu nimemtaja kwa jina, na nimesisitiza kama ananisikia kuhusu ofisi yake," alisema.
Katika mchango wake, Waziri Ghasia alijaribu kupangua tuhuma mbalimbali zilizoelekezwa katika wizara yake ikiwamo kuwapo ufisadi, ubadhirifu na mtandao wa wizi unaohusisha Hazina, Wizara na Halmashauri.

Ghasia alikiri Halmashauri ya Mbarali ilitumiwa fedha kuliko kiwango kilichoidhinishwa na Bunge na kwamba
suala la halmashauri mbili za Tanga kupewa zaidi ya Sh2 bilioni haikuwa sahihi bali yalikuwa ni makosa ya Mkaguzi Mkuu wa Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (CAG).

Kuhusu ufisadi wa zaidi ya Sh600 milioni zilizotolewa na wafadhili kwa ajili ya mpango wa maboresho ya Serikali za Mitaa, alisema haamini kama maneno yaliyonukuliwa na vyombo vya habari kuhusu fedha hizo yalisemwa na wafadhili.
Wafadhili wa mradi huo walinukuliwa wakilalamikia ufisadi huo na kudai kwa sasa hawana la kufanya na wanamwachia Rais, huku wakieleza kushangazwa na Rais kuteua watu dhaifu kuendesha wizara nyeti kama Tamisemi.

Kuhusu hilo, Ghasia alisema hadhani maneno hayo ni ya wafadhili akisema ni majungu, ni maneno ya waandishi kwa sababu huwa wanatafuta mambo yanayogusa jambo fulani ili kuuza magazeti.Hata hivyo, Ghasia alikiri kwamba ulifanyika ukaguzi na yalibainika matumizi ambayo hayakufuata taratibu na kusisitiza kuwa fedha zilizotumika bila kufuata taratibu zilikuwa Sh444.8 milioni na siyo Sh600 milioni.

Alisema kuwa tuhuma kwamba anawalinda watuhumiwa wa ufisadi na kuwahamisha wale wanaotuhumiwa si za kweli kwani wizara imekuwa ikichukua hatua za kinidhamu dhidi ya watumishi hao na hata kuwafikisha kortini.

Alitolea mfano wa Halmashauri ya Kishapu ambayo watumishi 14 wamesimamishwa kazi na masuala yao hivi sasa yanashughulikiwa na ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) na Ofisi ya Takukuru.

Pamoja na maelezo ya Waziri Ghasia, bado Mwenyekiti wa Kamati alisisitiza kuwapo matatizo makubwa
Tamisemi na ndipo alipowataka Ghasia na Manaibu wake kujipima wenyewe kama bado wanafaa kuongoza wizara hiyo nyeti.

Mwenyekiti huyo alisema si kweli kama alivyosema Waziri Ghasia kuwa hakuna mtandao wa ufisadi na
kusisitiza kuwa fedha zilizopelekwa jijini Tanga hazikurudishwa Hazina na badala yake zilitumiwa na Halmashauri hiyo.

Alisema kinachoonekana ni kwamba ulikuwapo mpango wa kuzipeleka fedha kwenye baadhi ya Halmashauri nje ya fedha zilizoidhinishwa lakini baadaye fedha hurudishwa kwa wanamtandao huo baada ya kutakatishwa.

Mwenyekiti huyo alisema Halmashauri zinazopelekewa fedha hizo zilizo nje ya bajeti, hupelekewa fedha hizo kwa malengo ya kuzitakatisha kisha kuzirejesha Hazina ambapo wahusika hunufaika nazo.
Ijumaa wakati akiwasilisha taarifa ya kamati, kamati hiyo iliilipua Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) ikiituhumu kuwa sehemu ya mtandao wa ufisadi serikalini.

Alisema bado kuna ubadhirifu, ufisadi na utovu wa nidhamu wa hali ya juu wa matumizi ya fedha za umma kutokana na Tamisemi kutosimamia au yenyewe kuhusika moja kwa moja na ufisadi huo.

Mfano wa mwaka 2011/2012 ambapo Sh1.6 bilioni zilitumika nje ya bajeti iliyoidhinishwa katika halmashauri 38 na Sh2.6 bilioni zilihamishwa kutoka akaunti moja kwenda nyingine bila kurudishwa.Kamati hiyo imebaini kwamba upo mtindo wa Serikali kutuma kwa Halmashauri kiasi kikubwa cha fedha kuliko kiasi cha fedha kilichoidhinishwa na Bunge katika fungu husika wakati wa upitishaji wa bajeti.
Kamati hiyo imetolea mfano wa Sh2 bilioni zilizotumwa Halmashauri ya Jiji la Tanga na Sh500 milioni zilizotumwa Halmashauri ya Mji wa Korogwe zikiwa zaidi ya kiasi kilichokuwa kimeidhinishwa na Bunge.

"Kitendo hiki ambacho kinafanyika kwa ushirikiano wa hali ya juu wa Hazina,Tamisemi na Halmashauri kinaashiria kuwapo mtandao wa kutisha wa kifisadi baina ya mamlaka hizo," alisema.

Kamati hiyo imeituhumu pia Tamisemi inayoongozwa na Waziri Hawa Ghasia, kuwahamisha haraka watumishi wanaotuhumiwa kufanya ubadhirifu kutoka halmashauri moja kwenda nyingine.

"Kamati imebaini kwamba Tamisemi imekuwa ikitumia mtindo huu kuwalinda watumishi mafisadi ndani ya halmashauri na kuifanya kamati iamini Tamisemi ni sehemu ya mtandao huu," imesema.


Mwenyekiti wa kamati hiyo alisema kwa makusudi mazima, Tamisemi imekuwa ikieneza saratani hiyo ya ufisadi kwenye halmashauri nyingi iwezekanavyo na kuitaka Serikali kuachana na mtindo huo.

Ubadhirifu Wakurugenzi 70
Itakumbukwa Agosti 19 mwaka huu, Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), ilitoa taarifa yake baada ya kubaini kuwepo kwa mtandao wa ufisadi unaoshirikisha Wakurugenzi 70 wa Halmashauri mbalimbali hapa nchini ambao wanashirikiana na baadhi ya Watendaji wa Ofisi ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) na Kitengo cha Hazina.

Baadhi ya halmashauri hizo ni pamoja na Wilaya ya Monduli, Arusha, Mwanza, Mbeya na Ilala.
Ilielezwa kuwa Tanzania Bara ina halmashauri 134, kwa hiyo ina maana zaidi ya nusu ya wakurugenzi wanajihusisha na mambo hayo.

"Baadhi ya wakurugenzi hao walihamishwa kwenye vituo vyao vya kazi kutokana na kashfa ya matumizi mabaya
ya fedha za Serikali, lakini bado wanajihusisha na mambo haya," alisema Mbarouk alipokuwa akiwasilisha taarifa yake kwa waandishi wa habari."Kuna zaidi ya Wakurugenzi 70 wako kwenye mtandao wa ufisadi kwa kushirikiana na watendaji wa Hazina na Tamisemi, jambo ambalo limesababisha halmashauri zao kupata hati chafu kwa miaka mitano mfululizo," alisema Mbarouk.

Aliongeza wakurugenzi hao wamekuwa wakishirikiana na wahasibu wao katika kutumia vibaya fedha za Serikali zinazotolewa kwa ajili ya kuendeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika halmashauri zao.

Akitolea mfano wa Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza, Wilson Kabwe ambaye halmashauri yake ilifanya vibaya katika ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), lakini hajachukuliwa hatua na badala yake amehamishwa kuwa Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam.
CHANZO MWANANCHI

No comments: