Thursday, February 6, 2014

Mbeya City wapigwa ‘stop’ kunyoa kiduku

mbeya city 56205
WACHEZAJI wa timu ya soka ya Mbeya City, wamepigwa marufuku kunyoa nywele za pembeni na kuziacha za katikati 'kiduku' na wameambiwa atakayejitosa kunyoa hivyo itakula kwake.

Mbali ya hilo, pia wamepigwa marufuku kufuga nywele na kuzisokota 'rasta'.
Kauli ya marufuku hiyo imetolewa na Kocha Msaidizi wa timu hiyo, Maka Mwalwisi na kuungwa mkono na Katibu Mkuu, Emmanuel Kimbe, waliosema wachezaji wa timu yao hawajafikia hatua ya kunyoa nywele kwa mfumo huo kama wanavyofanya wachezaji wa timu nyingine.

Mwalwisi alisema kuwa wachezaji wa Kitanzania wameiga mfumo huo kutoka kwa wachezaji wa nje jambo ambalo kwao imekuwa ni vigumu kuhudumia nywele zao kutokana na kipato kidogo wanachokipata.

"Kilichoruhusiwa ni kunyoa upara, hayo mambo mengine ya 'kiduku' na 'dread' kwetu hayana nafasi, kwanza uwezo wenyewe wa kuzihudumia hawana maana wakiweka hizo 'dread' zao wanakuwa kama wachafu," alisema. "Nywele zinahitaji matunzo kama wanavyofanya wachezaji wa nje pia muda wa kwenda kuzihudumia saluni, hapa Tanzania hata hao wanaofuga na kunyoa viduku uwezo wao kifedha sio mkubwa, tumewaambia atakayenyoa hivyo atapewa adhabu kwa mujibu wa taratibu zetu."

Alisema kuwa kwao nidhamu ya ndani na nje ya uwanja ndiyo wanaipa kipaumbele kuliko mambo mengine yoyote, suala ambalo liliungwa mkono na aliyekuwa mwamuzi wa soka, Othman Kazi.
Kazi alisema: "Tangu wapande daraja nimebahatika kuangalia mechi zao ila sijawahi kuona timu yenye nidhamu kama Mbeya City, ingawa siwezi kuzungumzia kiundani mechi yao na Yanga.
"Wachezaji wa Mbeya City hawana tabia ya kumzonga mwamuzi pale anapotoa uamuzi wake na hiyo ndiyo nidhamu inayotakiwa kwa wachezaji."

Katika mechi ya timu hiyo dhidi ya Yanga iliyochezwa Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, Yanga ilishinda bao 1-0. Hicho kilikuwa kipigo cha kwanza cha Mbeya City katika msimu wao wa kwanza wa Ligi Kuu Tanzania Bara

No comments: