IKULU ya
Rais Jakaya Kikwete imesema kuwa muda wa mwisho wa uhai wa Tume ya
Mabadiliko ya Katiba ulijulikana, hivyo mtu kujitia kwamba ameisahau
siku hiyo ni unafiki wa hali ya juu.Ikulu imetoa kauli hiyo ikijibu
madai yanayodaiwa kutolewa na Mwenyekiti wa Mabadiliko ya Katiba, Jaji
Joseph Warioba, kwenye moja ya vyombo vya habari jana,akidai Ikulu
imeitupia virago tume yake.
Taarifa hiyo ya ufafanuzi ambayo
ilitawaliwa na maneno makali dhidi ya Tume ya Jaji Warioba, ilitolewa
jana na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu na kusainiwa na Mkurugenzi wake
Salva Rweyemamu.
Katika taarifa hiyo, Ikulu ilisema
kuwa muda wa uhai wa tume hiyo ulijulikana, hivyo kwa mtu kujitia
ameisahau siku hiyo ni kiwango cha juu sana cha unafiki.
Ingawa Ikulu haikumtaja moja kwa moja
Jaji Warioba kuwa ni mnafiki, lakini ukweli ni kwamba kauli ya unafiki
ilimlenga Jaji Warioba aliyekaririwa na gazeti moja juzi, akidai kuwa
Ikulu imeitupia virago tume yake.
Madai ya Tume ya Warioba kufukuzwa kazi
Salva alisema kuwa itakumbukwa kuwa
moja ya mijadala mikali ya awali kuhusiana na mchakato wa katiba mpya
ulihusu lini Tume ya Mabadiliko ya Katiba imalize muda wake.
Alisema wengine walitaka tume imalize
muda wake baada ya kukabidhi ripoti ya tume na rasimu ya katiba, wengine
wakitaka tume baada ya Mwenyekiti wake Jaji Warioba kuwasilisha rasimu
yake bungeni na hata wengine wakitaka wajumbe wa tume wawe sehemu ya
Bunge Maalumu la Katiba.
"Hatimaye ilikubaliwa kuwa shughuli za
tume zingefikia ukomo wake baada ya mwenyekiti wake kuwasilisha rasimu
ya katiba kwenye Bunge Maalumu la Katiba kama inavyoelekezwa katika
kifungu cha 31 (1) cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba.
"Kifungu hicho kinasema kuwa baada ya
kuwasilishwa kwa rasimu ya katiba kwenye Bunge Maalumu chini ya kifungu
cha 20(3) (cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba), rais, kwa amri
itakayochapishwa katika Gazeti la Serikali, atavunja tume.
"Mheshimiwa Warioba aliwasilisha
rasimu ya katiba katika Bunge Maalumu la Katiba Jumanne ya Machi 18,
mwaka huu, 2014 na siku iliyofuata Jumatano, Machi 19, 2014 na kwa
mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, rais alitia saini tangazo la
serikali la kuvunja Tume ya Mabadiliko ya Katiba," alisema Salva.
Kwa mujibu wa Salva, tangazo hilo lilichapishwa katika toleo lililofuata la Gazeti la Serikali Machi 21, 2014.
"Hivyo, tokea mwanzo wa mchakato mzima
wa katiba mpya na utendaji kazi wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba
hapakupata kuwepo, hata wakati mmoja, shaka kuhusu siku ya tume hiyo
kumaliza kazi zake.
"Mwenyekiti wa tume, wajumbe wote wa
tume, sekretarieti ya tume na Watanzania wote waliijua fika siku ya
mwisho ya tume kukamilisha shughuli zake. Kwa mtu kujitia ameisahau siku
hiyo leo ni kiwango cha juu sana cha unafiki," alisema Salva.
Wajumbe wa tume kutakiwa kurudisha magari Ikulu
Akijibu madai mengine ya Jaji Warioba
ya wajumbe wa tume yake kutakiwa kurudisha magari Ikulu, Salva alikiri
kuwa kweli wajumbe wa tume walitakiwa kurudisha Ikulu magari ambayo
walikuwa wanatumia kikazi kwa sababu kazi ya tume ilikuwa imemalizika.
Pili, alisema tume ilijua tokea mwanzo
kuwa baada ya kumaliza kazi yao, magari ambayo walikuwa wanatumia
wajumbe na maofisa wa tume hiyo yalikuwa yanatakiwa kupelekwa Dodoma kwa
matumizi ya shughuli za Bunge Maalumu la Katiba ambalo linakabiliwa na
shida kubwa ya usafiri.
"Serikali ilichukua uamuzi kuwa magari
hayo yapelekwe Dodoma kwa sababu lisingekuwa jambo la busara kwa
serikali kutumia fedha za umma kununua magari mengine mapya wakati yale
ya tume bado yanafaa kufanya kazi na wala hakuna bajeti ya kufanya
manunuzi ya magari mapya.
"Hivyo, ni kweli magari hayo yako
Ikulu, Dar es Salaam, yakisubiri kukamilika kwa taratibu za kuyapeleka
Bunge Maalumu la Katiba mjini Dodoma," ilisema Ikulu.
Muda wa kukabidhi nyaraka na ofisi
Akijibu madai mengine ya Jaji Warioba
kwamba hawakupata muda wa kukabidhi ofisi na nyaraka, Ikulu ilisema kuwa
hili nalo ni jambo la kutunga na kuzusha tu.
Alisema Jaji Warioba alikabidhi rasmi
Ripoti ya Tume na Rasimu ya Katiba kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete na Rais wa Zanzibar Mheshimiwa
Dk. Ali Mohamed Shein, Desemba 30, 2014, mbele ya wananchi katika
viwanja vya Ukumbi wa Karimjee, jijini Dar es Salaam.
"Hivyo, toka siku hiyo, tume haikuwa
tena na kazi ya kuandaa ripoti ama rasimu kwa sababu kazi hiyo ilikuwa
imekwisha na wala isingeweza kuibadili tena rasimu ya katiba.
"Kwa maana hiyo, toka Desemba 30,
mwaka jana, kupitia miezi ya Januari, Februari mpaka Machi 18, mwaka
huu, sekretarieti ilikuwa na muda wa siku 77, zaidi ya miezi miwili
unusu, kufanya maandalizi ya kukabidhi nyaraka na ofisi kwa sababu
ilijua kazi yake ilikuwa inamalizika siku ambayo mwenyekiti wa tume hiyo
angewasilisha rasimu ya katiba katika Bunge Maalumu la Katiba.
"Sasa katika muda wote huo,
sekretarieti ya tume ilikuwa inafanya nini badala ya kuandaa ripoti ya
makabidhiano na wakati maofisa wake walikuwa wanaendelea kulipwa
mshahara na serikali? Kwanini walalamike hadharani leo kwa jambo ambalo
lilikuwa ni la wajibu wao na wakashindwa kulifanya kwa wakati?" alihoji
Salva.
Salva katika taarifa hiyo, pia alijibu madai kwamba wajumbe wa tume watalipwa kiinua mgongo cha sh milioni 200 kila mjumbe.
Alisema hakuna shaka kuwa wajumbe wa
Tume ya Mabadiliko ya Katiba wamefanya kazi nzuri sana na wanastahili
pongezi nyingi za wananchi. Lakini kama wanadhani kuwa serikali ina
uwezo wa kumlipa kila mjumbe kiinua mgongo cha sh milioni 200 basi
wanajidanganya kwani wananchi wa Tanzania hawawezi kuelewa maana kabisa
ya malipo hayo makubwa kupindukia.
"Alichokizungumza Rais Kikwete tokea
mwanzo wa mchakato ni kwamba atafikiria kuwalipa wajumbe wa tume aina
fulani ya kifuta jasho ambacho kiwango chake atakiamua yeye na kwa
wakati mwafaka na kulingana na rasilimali za serikali. Mpaka sasa
hajafanya uamuzi juu ya jambo hili," alisema Salva.
Ikulu pia katika taarifa hiyo ilitoa
ufafanuzi wa habari zinazosambazwa na baadhi ya vyombo vya habari kuwa
wajumbe wa tume hiyo walikuwa wanalipwa sh 500,000 (laki tano) kama
posho ya vikao kwa siku.
"Ukweli ni kwamba wajumbe wa tume
walikuwa wanalipwa sh 200,000 kama posho ya vikao kwa siku. Maofisa
waandamizi wa tume hiyo walikuwa pia wanalipwa posho ya sh 200,000 (laki
mbili) kwa siku, maofisa wa kati walikuwa wanalipwa sh 150,000 kutwa na
maofisa wa ngazi za chini walikuwa wanalipwa sh 100,000 kwa siku
kulingana na taratibu za serikali. Anayetangaza vinginevyo anajaribu tu
kuwapotosha wananchi," alisema Salva.
Juzi, Jaji Warioba alikaririwa na moja
ya magazeti akisema kuwa tume yake ilifukuzwa kazi, na kwamba haikupewa
muda wa kuandaa na kuwasilisha nyaraka za kukabidhi ofisi na madaraka.
Kwamba wajumbe wa tume hiyo waliporwa magari ambayo yamewekwa Ikulu.
No comments:
Post a Comment