Sunday, April 27, 2014

KAMATI ZA BUNGE KUANZA KAZI JUMATATU TAREHE 28 APRILI 2014 JIJINI DAR ES SALAAM

0D6A1769 
Afisa Habari wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Owen Mwandumbya akielezea kuhusu kufanyika kwa vikao vya Kamati za Bunge vinavyotarajia kuanza tarehe 28 Aprili hadi 4 Mei, 2014, Jijini Dar es Salaam kabla ya kuanza Mkutano wa Bunge wa Bajeti tarehe 6 Mei, 2014.  

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA 
BUNGE LA TANZANIA
TAARIFA KWA UMMA

KAMATI ZA KUDUMU ZA BUNGE KUKUTANA DAR ES SALAAM KUANZIA TAREHE 28 APRILI HADI 4 MEI, 2014

1.0       UTANGULIZI
Kamati za Kudumu za Bunge zitaanza kukutana tarehe 28 Aprili hadi tarehe 4 Mei 2014 Jijini Dar es Salaam, kutekeleza Majukumu yake, kabla ya Mkutano wa Bunge Bajeti uliopangwa kuanza mjini Dodoma tarehe 6 Mei na kudumu hadi tarehe 27 Juni, 2014.

Kwa kawaida, Kamati za Kudumu za Bunge hupaswa hukutana wiki mbili kabla ya Mkutano wa Bunge, ama Dar es Salaam, Dodoma au Zanzibar kuendana na matakwa ya Kanuni za Kudumu za Bunge, Toleo la Aprili 2013.
Hivyo, Wabunge wote wanapaswa kuwa wamewasili jijini Dar es Salaam ifikapo Jumapili tarehe 27 Aprili 2014 tayari kwa kuanza vikao siku  ya Jumatatu tarehe 28 Aprili, 2014.
2.0       SHUGHULI ZITAKAZOTEKELEZWA

Wakati wa vikao vya Kamati, zitatekelezwa kazi zifuatazo:-
2.1       Siku ya Jumatatu na Jumanne Tarehe 28 na 29 Aprili, 2014 Kamati zote za sekta pamoja na majukumu mengine, zitapitia masuala yote yaliyojitokeza wakati wa ukaguzi wa miradi mbalimbali ya Maendeleo

2.2       Siku ya Jumatano tarehe 30 Aprili, 2014 Wabunge wote kwa ujumla wao watakutana katika Ukumbi wa Julius Kambarage Nyerere kupokea Mapendekezo ya Mpango, Kiwango na Ukomo wa Bajeti ya Serikali ya 2014/2015 kwa mujibu ya matakwa ya Kanuni ya 97 ya kanuni za Kudumu za Bunge Toleo la 2013. Baada ya shughuli hiyo, Kamati zote za Kisekta zitaendelea na uchambuzi wa Bajeti kuanzia tarehe 1 hadi 4 Mei, 2014

2.3       Kamati zisizo za kisekta zikiwemo Kamati ya Bajeti, Kamati ya Masuala ya UKIMWI, Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) na Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) zitaendelea na utekelezaji wa Majukumu yake kama yalivyoainishwa katika Kanuni za Kudumu za Bunge Toleo la 2013.

2.4       Tofauti na kamati nyingine, Kamati ya Serikali za Mitaa na Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) zitaanza kazi zake mapema ambapo zitatakiwa kuwasili Dar es Salaam tarehe 25 April na kuanza kazi zake tarehe 26 Aprili, 2014
 3.0 SHUGHULI NYINGINE

Shughuli za Kamati zitamalizika tarehe 4 Mei, 2014 Jijini Dar es Salaam ambapo Mkutano wa Bunge wa Bajeti utaanza tarehe 6 Mei, 2014 Mjini Dodoma na unategemewa kumalizika tarehe 27 Juni, 2014.
Aidha, Bunge linatarajiwa kupitisha Mapendekezo kwamba Bunge liwe likikutana kuanzia saa Tatu Asubuhi hadi saa Saba Mchana kila siku na kisha kuendelea Jioni saa Kumi hadi saa Mbili Usiku ikiwa ni pamoja na Siku za Jumamosi.

Hata hivyo, siku ya Ijumaa Bunge litakutana kuanzia saa Tatu asubuhi hadi saa Sita Mchana na kuendelea saa kumi Jioni hadi saa Mbili Usiku. Utaratibu huu ukiafikiwa utawezesha muda wa kujadili Bajeti kuongezeka zaidi licha ya siku kupungua

 Ratiba za shughuli za Kamati zote zitapatikana kwenye tovuti ya Bunge ambayo ni www.parliament.go.tz
 Imetolewa na:
Idara ya Habari, Elimu kwa Umma na Uhusiano wa Kimataifa,
Ofisi ya Bunge
DODOMA

No comments: