Wednesday, April 2, 2014

Wabunge CCM wazidi kumwandama Warioba

warioba_b4bf6.jpg
Jaji Joseph Warioba
Dodoma. Wabunge wa CCM wameendelea kuirarua Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa bungeni na Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba.
Wabunge hao ni Diana Chilolo na Dk Haji Mponda ambao kwa nyakati tofauti walisema mjadala usingefika hapa kama sio mawazo binafsi ya Warioba.
Chilolo alimtuhumu Warioba kuwa aliingiza mawazo yake na kuacha walichochangia wananchi.

"Unaweza kuona hata mawazo ya wananchi wangu wa Singida hayakuingizwa kwenye Rasimu, lakini leo wanasema ni mawazo ya Watanzania wote, hakuna kitu kama hicho, ni mawazo yake tu," alisema Chilolo, ambaye ni Mbunge wa Viti Maalumu.
Mjumbe huyo alisema kuwa mawazo yaliyoingizwa katika Rasimu ya Pili ya Katiba kwa sehemu kubwa yameacha mawazo ya wananchi na badala yake yameingizwa mawazo ya watu wengine wenye utashi wao.

Kwa upande wake, Mbunge wa Ulanga Magharibi, Dk. Haji Mponda alisema kinacholisumbua Bunge la Katiba ni mawazo ya Warioba ambayo hayakuzingatia Utaifa na Uzalendo.

Dk. Mponda aliiponda Rasimu ya Katiba kwamba imejaa mambo binafsi ambayo hayawezi kutekelezeka na kuyaacha yale ambayo wengi walitarajia yangeibuka.
Tangu kuanza kwa mchakato wa mabadiliko ya Katiba, CCM imekuwa ikitoa miongozo mbalimbali kwa wanachama wake na kuwataka waitetee katika mijadala ya Bunge.
Baadhi ya miongozo hiyo ni Muundo wa Muungano kuwa wa serikali mbili na kura za wazi katika kupitisha uamuzi bungeni.

Katika kutetea misimamo hiyo, baadhi ya wajumbe wa CCM wamekuwa wakipingana na Rasimu ya Pili iliyowasilishwa bungeni na Jaji Warioba.
Hata hivyo, msimamo huo wa CCM umekuwa ukipingwa vikali na baadhi ya vyama vya upinzani.

No comments: