Tuesday, December 16, 2014

WALIOVURUGA UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA WAADHIBIWE, UKAWA BADO NI KIINIMACHO: NAPE

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimetaka watendaji wote waliosababisha kuharibika kwa uchaguzi wa Serikali za Mitaa katika baadhi ya maeneo nchini wachukuliwe hatua kali.
Kimesema, watendaji hao wanastahili kuchukuliwa hatua kali kwa sababu kilichotokea ni uzembe wa hali ya juu uliofanyika huku ikifahamika wazi kwamba tukio la uchaguzi huo ni kubwa na muhimu sana kwa taifa.
Akizungumza na waandishi wa habari leo, katika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba jijini Dar es Salaam, Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye (pichani) amesema, kulingana na kosa lililojitokeza kuwa la wazi hakuna haja ya kupoteza fedha na muda kufanya uchunguzi kabla ya kuwachukulia hatua waliohusika.
“Kwa mfano, Mkurugenzi wa Halmashauri ana kila kitu na alijua mapema kuwa uchaguzi utafanyika lini kwa kuwa halikuwa jambo la dharura, inakuwaje anaruhusu karatasi ziende kwenye vituo zikiwa zimechapishwa hovyo au mahali pengine vifaa viwe vicheche?” alihoji Nape na kuongeza “Sasa hapa unahitajika uchunguzi gani tena kubaini aliyevurunda?”.
“Mahali pengine zimefika karatasi za kupigia kura jina la mgombea wa CCM nembo ya CUF, au mgombea wa CUF nembo ya CCM! huu ni uzembe wa hali ya juu sana na adhabu yake haistahili kusubiri uchunguzi”, alisema Nape.
Akizungumzia matokeo ya awali ya Uchaguzi huo, Nape alisema licha ya vyama vya upinzani kuwa na umri wa miaka 22 sasa, huku vikifanya harakati za kujaribu kuungana katika umoja wanaouita Ukawa, bado CCM imewagaragaraza vibaya.
Nape amesema, katika uchaguzi huo, CCM imepata zaidi ya asilimia 80 ya ushindi kwa nchi nzima, huku Dar es Salaam, ikiwa na asilimia zaidi ya 70 licha ya kwamba Chadema wanao wabunge wawili katika mkoa huo.
“Katika mazingira ya sasa ambayo vyama vya upinzani vina miaka 22, na vinafanya hata harakati za kujaribu kuungana, asilimia 80 si ndogo kwa CCM, na tunaamini huu ni mwanzo mzuri, na hatuoni namna ambavyo asilimia hii itabadilika katika uchaguzi mkuu mwakani, maana uchaguzi huu ni kama kura za maoni”, alisema Nape.
“Wanaosema, asilimia ya CCM imeshuka, wajue kwamba tuliposema tunataka mfumo wa vyama vingi maana yake tulitaka ushindani katika demokrasia, katika demokrasia ya ushindani ni vema kuruhusu vyama vya upinzani vikakua ili ushindani huo uonekane”, alisema Nape nakuongeza.
“Hata hivyo inasikitisha kwamba licha ya vyama vya upinzani kuwa na umri wa miakaa 22 sasa, bado havijaweza kujenga imani ya kutosha kwa Watanzania kuwa vinaweza kuongoza, lazima wapinzania wazidi kujijenga ili Watanzania wawaamini, asilimia hii 14 waliyopata karika uchaguzi huu wa serikali za mitaa bado ni ndogo sana kwa uhai wa miaka hiyo”.
Amesema, asilimia iliyopata CCM wakati matokeo mengine yakisubiriwa ambako uchaguzi uliahirishwa, ni dalili za wazi kwamba, Ukawa bado ni muungano wa mashaka kwa sababu kama wangeungana na kuachiana maeneo ni kweli wangeweza kufika mbali.
“Hebu jiulizeni na ninyi, kama kweli UKawa ulitumika vema, ni kwa nini kwenye karatasi za matokeo ya uchaguzi huu, kila chama kina mtu wake na idadi ya kura alizopata? Kwa nini zisiwe za mgombea mmoja wapo wa Ukawa?… Hii inamaanisha ndoa hii ya ukawa bado sana”, alisema Nape.
Nape aliwashukuru wananchi nchini kote kwa kuendelea kuiamini CCM, na kuchagua wagombea wake, huku akivipongeza vyama vya upinzani kwa maeneo waliyochaguliwa, akiwataka kuchapa kazi vinginevyo siku za baadaye wananchi watawahukumu kwa kuwatosa.
 Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye akizungumza na waandishi wa habari, leo katika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba jijini Dar es Salaam, kutoa tathmini ya matokeo ya awali uchaguzi wa Serikali za mitaa uliofanyika juzi nchini kote.
Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye (kushoto), akizungumza na waandishi wa habari, leo katika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba jijini Dar es Salaam, kutoa tathmini ya matokeo ya awali uchaguzi wa Serikali za mitaa uliofanyika juzi nchini kote.

No comments: