Monday, February 2, 2015

BARABARA YA IGAWA – UBARUKU KUJENGWA KWA LAMI


Waziri wa Ujenzi Dkt. John Pombe Magufuli amesema serikali itajenga barabara ya Igawa hadi Ubaruku KM 18 kwa kiwango cha lami ili kuinua fursa za uchumi za wilaya ya Mbarali na kuwezesha magari makubwa kupita kwa urahisi kufuata mazao katika eneo hilo.

Waziri Dkt. Magufuli amesema hayo katika ziara yake inayoendelea mkoani Mbeya ambapo leo ameweka jiwe la msingi ujenzi wa barabara ya igawa-ubaruku yenye urefu wa KM 18 na kusisitiza barabara hiyo ni muhimu kwa uchumi wa mkoa wa Mbeya na taifa kwa ujumla.
"Nitahakikisha barabara hii inajengwa kwa kiwango cha lami na kukamilika mapema ili kuunga mkono juhudi za wananchi wa Mbarali wanaotekeleza sera ya kilimo kwanza kwa kuzalisha mpunga na mahindi kwa wingi", amesisitiza waziri Magufuli.

Amewataka wananchi waliojenga katika hifadhi ya barabara kupisha eneo la barabara ili kuwezesha kazi ya ujenzi huo kufanyika kwa haraka na kumalizika kwa wakati.
Amemwagiza Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara Nchini TANROADS Eng. Patrick Mfugale kufanya usanifu ili kuwezesha madaraja kumudu kupitisha magari yenye uzito wa tani 40 yatakayochukua mazao katika maeneo ya Rujewa na Ubaruku.

Eng. Mfugale amesema barabara ya Igawa-Ubaruku kwa sasa ni barabara ya mkoa na ujenzi wake utazingatia vigezo vya barabara za mikoa ili kukidhi mahitaji ya uzito wa magari yatakayopita katika barabara hiyo.
Kuhusu barabara ya Igawa –Madibira yenye urefu wa KM 153 ambayo upembuzi yakinifu na usanifu wake umekamilika waziri Magufuli amesema Serikali inatafuta fedha ili kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami na hivyo kuifungua kiuchumi wilaya ya Mbarali.

Amesisitiza umuhimu wa umoja,mshikamano na uaminifu kwa wananchi wa Mbarali na kuwataka vijana watakaopata kazi wakati wa ujenzi wa barabara hiyo kuwa waaminifu.
Naye mkuu wa mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro amemshukuru Waziri wa Ujenzi kwa kuamua kujenga kwa lami barabara za Mpemba hadi Isongole wilayani Ileje ,Igawa hadi Ubaruku wilayani Mbarali na Kikyusa hadi Matema wilayani Kyela na kusisitiza barabara hizo zitakapokamilika zitaimarisha usafiri na kuibua fursa za ajira na uchumi kwa wakazi wengi wa mkoa wa Mbeya.

No comments: