Ndugu zangu,
Katika ulimwengu huu kuna tabia na hulka. Hivi viwili vina tofauti. Kuna sifa na uwezo, navyo ni viwili tofauti.
Tabia ya
mwanadamu yaweza kubadilika, lakini si hulka yake. Na mwanadamu anaweza
kuwa na sifa za kufanya jambo lakini akakosa uwezo, na kinyume chake.
Na kibaya
zaidi ni pale majungu na fitna yanapogubika sifa na uwezo wa mtu.
Kwamba badala ya mwanadamu kupimwa kwa sifa na uwezo wake, majungu na
fitina dhidi ya mwanadamu huyo yanawekwa mbele na hivyo kufanywa kuwa
kipimo.
Ndio,
kuna wanadamu wenye kuishi kwa kupika majungu na fitna dhidi ya wanadamu
wenzao. Tofauti na tabia, hizo ni hulka za wanadamu hao, haziwezi
kubadilika.
Ndio,
nyani hata akizeeka haachi hulka yake. Kupalamia miti ni hulka ya nyani.
Hivyo, nyani hata akizeeka, hafikiri hata siku moja kukaa chini ya mti
na kupumzika, atahakikisha anapalamia hata mti mfupi wa mpapai, alimradi
akae juu ya mpapai. Hapo atajiona ametimiza unyani wake.
Naam,
Wahenga walitwambia; kiumbe mzito. Mwenyezi Mungu ametuumba wanadamu kwa
usawa kwenye mambo mengi. Wala hakutaka kubagua; ona unyayo wa
mwanadamu, uko sawa, iwe kwa tajiri au masikini.
Wewe na
mimi tumepata, ama wenyewe au kusikia mtu akilalamika kuwa soli ya kiatu
chake imechakaa, kwamba anakwenda kwa fundi viatu kubadilisha soli.
Lakini,
wewe au mimi hatujapata kumsikia mwanadamu mwenzetu akilalamika kuwa
unyayo wake umechakaa, anataka kwenda kwa fundi awekewe unyayo mwingine!
Ndio,
wewe na mimi ama tumeshuhudia au kusikia kuwa upepo umeangusha mti,
nyumba, ghorofa, gari na hata meli. Lakini, jiulize, je, umepata kumwona
mwanadamu mwenzako anayetembea kwa miguu akiangushwa kwa upepo?
Kamwe
mwanadamu haangushwi na upepo, hata awe mwembamba kiasi gani. Na
ukimwona mwanadamu mwenzako anayumba na kuanguka barabarani, basi, ama
ni mgonjwa, au ni mlevi. Na hilo la mwisho haliwezi kuwa na maana ya
mwanadamu huyo kaangushwa na upepo, bali kaangushwa na pombe zake
alizokunywa.
Naam, kiumbe mzito.
Naam, kiumbe mzito.
Ni Neno La Leo.
Maggid.
Iringa.
Maggid.
Iringa.
No comments:
Post a Comment