Tuesday, September 1, 2015

Sitta ataka akutanishwe na Lowassa

MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) na Mbunge wa Urambo aliyemaliza muda wake, Samuel Sitta ametaka uandaliwe mdahalo kwenye vyombo vya habari kati yake na mgombea urais wa Chadema, Edward Lowassa uelezwe ukweli juu ya ukweli wa sakata la Richmond.
Sitta ambaye alikuwa Spika wa Bunge wakati Lowassa alipojiuzulu kutokana na sakata hilo, alisema katika mdahalo huo, ataeleza ukweli juu ya uhusika wa Lowassa katika sakata hilo na atatoa vielelezo kueleza taifa ufisadi uliokuwa ukifanyika.

Alisema hayo jana kwenye ufunguzi wa kampeni za CCM mkoa wa Shinyanga katika mkutano uliofanyika mjini hapa ambao wagombea wa udiwani na ubunge wa majimbo yote ya mkoani hapa walitambulishwa.
Katika mkutano huo, alisema kujiuzulu kwa Lowassa mwaka 2008, kulitokana na Kamati Teule iliyoongozwa na Dk Harrison Mwakyembe, kugundua kwamba fedha za walipa kodi zilikuwa zikipotea bure.

Alisema yuko tayari kusimulia kwa umma utajiri wa mgombea huyo wa Chadema. Makundi, urafiki Sitta ambaye ni Waziri wa Afrika Mashariki, ambaye pia alikuwa kwenye kinyang’anyiro cha kutaka kuteuliwa kugombea urais kupitia CCM, alisema wanamwamini Dk John Magufuli katika utendaji wake wa kazi na pia ni kiongozi asiye na makundi au urafiki.

“Kweli lazima uwapime viongozi, kwani anayetaka urais lazima achaguliwe kwa kufuata utaratibu, achambuliwe usiogope moshi kama unapikia kuni...lakini mwenzetu Lowassa hakukubaliana na hayo, akaona kaonewa kwa madai anafaa kuwa rais mbona sisi tulikubali?,” alihoji Sitta.
Aliendelea kusema, “hali hiyo, ilionesha ndani ya CCM kulikuwa na vyama viwili ambavyo ni ‘CCM Katiba’ na ‘CCM Maslahi’ ambayo alikuwa anaongoza Lowassa na mfuasi wake, Mgeja (aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga ambaye pia alihamia Chadema hivi karibuni).
Wanachama mapandikizi Sitta alisema CCM ilikuwa imejaa wanachama walio mapandikizi tofauti na sasa ambapo alidai wamekwisha jionesha na kimekuwa chama kizuri kama ilivyokuwa enzi za hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.
Alisisitiza kwamba kitazidi kuimarika na waliobaki wataendelea kutetea ilani na kuhakikisha chama kinaendelea kushika dola. Kwa mujibu wa Sitta, wakati wa mchakato, baada ya kumaliza vikao, Lowassa alikuwa akiitisha vikao vya kundi lake alilolibatiza CCM Maslahi na kuwaagiza wapambe wake kuitisha vyombo vya habari kushambulia watu ambao hawako kwenye mlengo wao.
Wakati huo huo mjumbe huyo wa NEC, alikumbusha umati uliohudhuria mkutano huo kwamba, uchaguzi wa mwaka huu unatumia Katiba ya zamani ya mwaka 1977 ambayo inatamka matokeo ya rais hayahojiwi hata kama aliyeshinda, amezidi kura moja.
Sitta ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Bunge Maalumu, alisema alishauri wabunge wasitoke nje ya Bunge hilo waweze kutumia katiba hiyo iliyokuwa na kipengele cha kuhoji matokeo ya rais sasa imekula kwao.
Lusinde ahoji
Kwa upande wake, Mbunge wa Mtera, ambaye pia mjumbe katika kampeni ya uchaguzi Livingstone Lusinde , alihoji sababu za Lowassa kulalamikia kukatwa akisema ameonewa. “Mbona kaingia Chadema siku moja, ya pili kaingia kwenye nafasi ya urais; mbona na yeye huko kawaonea wenzake aliowakuta,” alihoji Lusinde.
Wanaomtumia Nyerere
Aliyewania ubunge kupitia kura za maoni ndani ya chama, jimbo la Shinyanga Mjini , Hassan Athumani alieleza kushangazwa na wanaogeuza kauli ya Baba wa Taifa, Nyerere kwa kuleta maudhui tofauti juu ya dhana ya mageuzi.
Alisema kauli ya Nyerere kwamba Watanzania wakikosa mageuzi ndani ya CCM watayapata nje ya CCM, hakuwa na maana kama inavyofikiriwa na waliohama chama kwamba wakikosa udiwani, ubunge na urais, waende upinzani.
UVCCM na Richmond
Wakati huo huo Kaimu Katibu Mkuu wa UVCCM, Shaka Hamdu Shaka katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, alisema wameshangazwa kuona mgombea wa Chadema, Lowassa akishindwa kuzungumzia ufisadi, kutaja walioshindwa kuwajibika, kukiuka maadili ya uongozi wakiwamo wa sakata la Richmond.
“Tumeshangaa kumuona akishindwa kuzungumzia masuala ya ufisadi na kutowataja wezi waliopora rasilimali za umma na maliasili za nchi, waliofuja uchumi, wala rushwa, watu waliokosa kuwajibika na kutochukuliwa hatua za kisheria kwa masuala mazima ya kukiuka maadili ya uongozi ikiwemo sakata zito la mradi wa kufua umeme wa dharura kupitia kampuni hewa ya Richmond,” alisema.
HABARI LEO

No comments: